Thursday, May 31, 2012

WASICHANA 49 WAJERUHIWA KATIKA TAMASHA LA JUSTIN BIEBER NORWAY...


Meya wa Jiji la Oslo amezindua uchunguzi kuhusu tamasha la mwimbaji Justin Bieber nchini Norway usiku wa kuamkia leo ambapo wasichana 49 walijeruhiwa kwenye msongamano mkubwa na 14 kati wakachukuliwa kwa gari la wagonjwa kukimbizwa hospitali kupatiwa huduma ya dharura.
Hakuna aliyeumia vibaya sana, lakini Meya Fabian Stang alisisitiza, "Nimeagiza Taasisi ya Mipango ya Dharura kuchunguza tamasha zima kuanzia mpangilio wa jukwaa hadi uwezeshaji wa tamasha hilo. Tunatakiwa kujua wapi kulikuwa na dosari na kwanini hili likatokea."
Meya Stang alisema hali ilikuwa mbaya sana, alilazimika kujificha kwenye moja ya miti wakati fulani kukwepa madhara.
Baadhi ya watu walilazimika kutumia kila njia kuweza kufika kwenye jukwaa.

NMB YAZINDUA PROMOSHENI YA "JENGA MAISHA NA NMB"...


Mkuu wa Idara Masoko na Mawasiliano wa Benki ya NMB, Iman Kajula akiongea na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa Promosheni ya "Jenga  Maisha Yako na NMB" iliyozinduliwa Dar es Salaam leo. Kulia ni Meneja Masoko wa benki hiyo, Shilla Senkoro.

MWANAFUNZI ASHINDA PROMOSHENI YA "VUMBUA DHAHABU CHINI YA KIZIBO"...

Meneja wa bia ya Serengeti, Allan Chonjo (katikati) akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo katika droo ya Promosheni ‘Vumbua Dhahabu Chini ya Kizibo' ambapo mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine cha Mwanza, Mariam Karumba alijishindia Bajaji. Kulia ni  Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya kubahatisha, Abdallah Hemedy na Tumainiel Malisa, kutoka PWC Consultant.

MCHUNGAJI AFA KWA KUGONGWA NA NYOKA KANISANI...



Mchungaji mchezea nyoka amekufa baada ya nyoka wake kumng’ata wakati akiendesha misa kanisani.
Mchungaji huyo wa Kanisa la Pentekosti, Mark Wolford (44) alikuwa akiendesha misa nje ya Kanisa katika eneo la kituo cha Usimamizi wa Wanyamapori cha Panther jimboni hapa Jumapili, ambayo kabla aliitangaza sana katika mtandao wake wa Facebook. 
“Nataka kuwa na siku kubwa Jumapili hii,” Wolford aliandika Mei 22 kwa mujibu wa gazeti la Washington Post. “Itakuwa siku njema na ya furaha kama zilivyokuwa siku za zamani.” 
Robin Vanover, dada wa Wolford, aliiambia Washington Post kwamba dakika 30 za misa hiyo, Wolford alikuwa akipita na nyoka huyo mwenye sumu kali ambaye baadaye alimng’ata.
“Alimlaza chini,” Vanover alisema katika mahojiano, “naye akakaa chini karibu na nyoka huyo, na akang’ata pajani.” 
Vanover alisema Wolford baadaye alikimbizwa katika nyumba ya mwanafamilia yake mjini Bluefield umbali wa takriban maili 80 kwa ajili ya huduma ya kwanza. Lakini hali ilibadilika na kuwa mbaya, akakimbizwa hospitalini ambako baadaye alifariki dunia.
Jim Shires, mmiliki wa mochari ya Gravens-Shires iliyoko Bluefield, aliiambia ABC kwamba Wolford alifariki dunia Jumatatu. Kanisa lake, Nyumba ya Mitume ya Mungu Yesu lililoko Matoaka, leo litauonesha mwili wake na maziko kufanyika kesho asubuhi   kwenye uwanja wa familia ya Hicks mjini Phelps, Kentucky.
Maofisa katika kituo cha Panther, hawakuwa na taarifa na kilichotokea Jumapili, hadi walipojulishwa na waumini waliopiga simu baada ya misa ile. 
“Hatukujua kuwapo kwa tukio hilo, na kama tungejua mapema kuhusu hilo au kama tungeombwa ruhusa, ruhusa hiyo isingetolewa,” Hoy Murphy, Ofisa Habari wa Idara ya Maliasili ya West Virginia aliiambia ABC.
Hoy alisema jimbo la West Virginia linazuia wanyama zaidi ya mbwa na paka kuingia katika eneo hilo na binadamu.
Wakati umiliki wa nyoka ni halali jimboni hapa,  majimbo mengine ya Appalachian yakiwamo ya Kentucky na Tennessee, yanazuia hali hiyo hasa katika maeneo ya umma.
Wolford alipata kuiambia Washington Post mwaka jana, kwamba anaendeleza mila ya wahenga ya kucheza na nyoka.
“Yeyote anaweza kufanya hivi kama anaamini,” Wolford alisema. “Yesu alisema, ‘Ishara hizi zitawafuata wanaoamini.’ Ishara hii inaonesha watu kwamba Mungu ni muweza.”
Wolford alisema alishuhudia baba yake akifa akiwa na umri wa miaka 39, baada ya kung’atwa na nyoka katika misa kama hiyo. 
“Aliishi kwa saa 10 na nusu,” Wolford aliiambia Washington Post. “Alipong’atwa, alisema alitaka afie kanisani. Saa tatu baadaye, mapafu yake yalifunga. Baada ya muda, moyo wake ukasimama. Nilichukia kumwona akiondoka, lakini alifia alichokiamini.
“Najua ni uhalisia; ni nguvu za Mungu,” Wolford alisema mwaka jana. “Kama nisingefanya hivyo,  kama nisingejihusisha na hili, ingekuwa sawa na kukana nguvu za Mungu na kusema hakuna uhalisia.”

MKE AHISI DAWA ZA KULEVYA SABABU ZA KIFO CHA JOHNNY TAPIA...


Mke wa bingwa wa zamani wa ndondi duniani, Johnny Tapia anaamini mumewe alitumia dawa zilizopigwa marufuku kisheria wiki moja kabla ya kifo chake, hii ni kwa mujibu wa vyanzo vya habari vya kisheria.
Katika nakala ya maelezo ya polisi yaliyochukuliwa muda mfupi baada ya kugundulika mwili wa Tapia nyumbani kwake New Mexico wiki iliyopita na kwa mujibu wa nyaraka, mashaka hayo ya Teresa yametokana na tatizo sugu alilokuwanalo mumewe la matumizi ya dawa za kulevya. Teresa amekiri kutokuwa na vidhibiti kuongezea nguvu madai yake hayo.
Polisi hawakukuta ushahidi wowote wa dawa zilizokatazwa kisheria kwenye nyumba ya Tapia, lakini wakakuta kasha lililofungwa likiwa limejaa dawa mbalimbali za tiba zikiwamo Hydrocodone (generic Vicodin) na Quetiapine (dawa zinazotumika kutibu maradhi ya akili).
Askari wamesema wamekuta pia vidonge vya Hydrocodone kando ya mwili wa Tapia.
Wanafamilia wamewaeleza polisi kwamba Tapia alikuwa akilalamika maumivu ya tumbo masaa kadhaa kabla ya kifo chake.
Uchunguzi wa kifo cha Tapia ulikamilika jana. Matokeo ya uchunguzi huo yanatarajiwa kutangazwa wiki kadhaa zijazo.

TYLER PERRY AKANUSHA KUKIMBIWA NA BINTI WA WHITNEY HOUSTON...

Tyler Perry amekanusha vikali ripoti zilizozagaa kuwa binti wa Whitney Houston, Bobbi Kristina ameingia mitini kuandaa Onesho lake la Televisheni "For Better Or Worse" akiziita tetesi hizo kuwa 'hazina ukweli wowote.'
Bobbi Kristina ana nafasi ndogo ya kucheza kwenye onesho hilo, lakini taarifa zimekuwa zikizunguka kwamba amejiondoa kabla ya msimu kuanza, huku akimwaga machozi wakati wa maandalizi.
Sasa Tyler, mbunifu wa shoo hiyo ametumia tovuti yake kukanusha tetesi hizo akiandika, "Hakuna uwezekano wowote wa yeye kutoka sababu tumeshamaliza zoezi la upigaji picha."
Tyler ameandika, "Kulikuwa na wakati mgumu kwake? Ndio. Si kwa sababu ya kuigiza au kazi yoyote inayofanana na hilo lakini sababu ya ukweli kwamba ndio ametoka kufiwa na mama yake."
Aliongeza, "Hivyo ndio alikuwa akisononeka, lakini alisononeka pembeni, ila alimudu kumaliza majukumu yake na alifanya kazi nzuri kwa wakati huo huo."

JUSTIN BIEBER AFANYA KUFURU NORWAY...



Polisi nchini Norway wamekiri kuwa katika wakati mgumu hivyo kulazimika kuomba msaada wa dharura mjini Oslo, kufuatia mashabiki zaidi ya elfu kumi kuwazidi nguvu polisi hao na kujazana mitaani wakati wa mapokezi ya mwimbaji Justin Bieber, na kwamba sasa wamelazimika kuomba msaada kutoka kwa mwimbaji huyo.
Bieber amepanga kucheza nyimbo zake mpya nne usiku wa kuamkia leo mjini Oslo ikiwa ni sehemu ya kipindi chake maalumu cha televisheni "Around the World" na imeelezwa mashabiki waliopagawa wa Justin kutoka bara lote la Ulaya wamevavia jiji hilo kwa ajili ya kushuhudia onesho hilo.
Imeelezwa umati ulifurika kupita kiasi kwa ajili ya kumpokea Bieber, kiasi cha polisi kushindwa kabisa kudhibiti na hivyo kulazimika kumuomba mwimbaji huyo kuanza kutumbuiza mapema kabla mambo hayajaharibika.
Kwa kufahamu kuhusu hali hiyo, Bieber alituma ujumbe katika mtandao wa Twitter akisema, "...ili onesho lifanyike kila mmoja lazima wafuate maagizo ya polisi. Wote tunahusika kwa usalama wenu na ninataka kuwapatia kile kilicho bora kwenu. Tafadhali sikilizeni."
Kwa sasa Bieber yuko kwenye sehemu ya faragha na atatua kwa helikopta jukwaani.

KWA WANAOJUA KIMOMBO...

Inakuwaje kwa maelekezo ya bango hili?

ZIRO PLUS...

CHEKA TARATIBU...

Baada ya kazi ngumu za siku hiyo mwili ukiwa umejipumzisha ndipo viungo vikaanza malumbano kwa kila kimoja kudai kina majukumu mazito kuzidi vingine. Baada ya kila kimoja kutaja ugumu wa majukumu yake ikaonekana vyote viko sawa kwa uzito wa majukumu yao. Wakati kila kimoja kikiamini hivyo, ndipo makalio yakaongezea, "Pamoja na umuhimu wangu wote, lakini mimi ndio ninatandikwa viboko bila hatia kwa makosa ama ujinga wa watoto majumbani na mashuleni!" Duh...

NGUO ZILIZOPOTEA CHUMBANI KWA WHITNEY ZAPATIKANA...

Aliyekuwa mpenzi wa Whitney Houston, Ray J.
Saa chache kabla ya mbunifu wa mavazi kumshitaki mwimbaji Ray J kufuatia nguo za mbunifu huyo kupotea kwenye chumba alimofia Whitney Houston Februari, mwaka huu, imeelezwa kuwa mwimbaji huyo ameziona.
Iliripotiwa masaa kadhaa yaliyopita kwamba Ray J amefunguliwa mashitaka na mbunifu wa mavazi wa Los Angeles, Marc Littlejohn, ambaya anadai alimkodisha Ray J mavazi mbalimbali yenye thamani ya Dola za Marekani 2,880 kwa ajili ya Tuzo za Grammy, na kwamba alikuwa hakuzirejesha.
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, waliziacha chumbani kwenye Hoteli ya Beverly Hills ambako Whitney alifariki na tangu hapo hazikuonekana tena.
Lakini sasa mwakilishi wa Ray J amesema utata huo umekwisha tangu jana usiku pale mmoja wa washirika wa Whitney alipokabidhi nguo hizo kwa Ray J.
Vyanzo vimesema vitu hivyo vilitolewa kwenye chumba cha Whitney pamoja na vitu vingine vya marehemu. Imeelezwa watu hao wa Whitney walishindwa kumpata Ray J kutokana na mwimbaji huyo kubadili namba yake ya simu.
Vitu hivyo vilivyokuwa vimepotea ni pamoja na suti mbili na jaketi moja.

JICHO LA TATU...

ASILI YA MAJINA YA MAENEO MBALIMBALI...

Moja ya majengo ya serikali yaliyopo katika eneo la Kiponzelo, mkoani Iringa.
Kiponzelo ni moja ya maeneo maarufu katika mkoa wa Iringa. Lakini naamini wengi hawafahamu asili ya jina hili. Kaa chini nikupe simulizi ambayo hatimaye ikazaa jina la Kiponzelo. Wakati wa upanuzi wa barabara kuu iendayo Zambia ambayo inapita katika mkoa wa Iringa, mzungu mmoja akiwa sambamba na Waswahili kadhaa walikuwa makini wakichukua vipimo kadhaa kwa kutumia mashine zao. Ikafika wakati wakiwa kwenye eneo ambalo sasa linajulikana kama Kiponzelo, Mzungu akasimama upande mmoja huku akiangalia kwenye kamera yake maalumu kwa upimaji na Mswahili mmoja akiwa na fimbo yake maalumu kwa kazi hizo akipokea maelekezo kutoka kwa Mzungu. "Keep On Zero! Hey, Keep On Zero," alipiga kelele yule Mzungu mara kwa mara akimaanisha Mswahili achomeke ile fimbo mahali inaposomeka Sifuri! Wakati wakiendelea hivyo, ndipo Mnyalu mmoja akakatiza akielekea kilabuni na kusikia yale maneno. Bila hiyana akayafikisha kwa washikaji wake kwamba kamuona Mzungu Kiponzelo, akimaanisha lile eneo walipokuwa wakifanya upimaji. Nakutakieni siku njema...

ZIRO PLUS...

Wednesday, May 30, 2012

MARY J. BLIGE AJUTIA 'MADUDU' YA TAASISI YAKE...


Mary J. Blige amejifunza somo muhimu kuhusu kujitolea tangu taasisi yake iliposhitakiwa kwa kushindwa kurejesha mkopo wa Dola za Marekani 250,000 akieleza kuwa alifanya makosa kuiacha huru na kusababisha ufujaji mkubwa wa fedha na kwamba sasa analipa kwa makosa yake.
Imevujishwa kwamba, Mary J. Blige and Steve Stoute Foundation for the Advancement of Women Now (FFAWN)inashitakiwa na Benki ya TD kwa kushindwa kurejesha mkopo wa Dola za Marekani 250,000 iliyochukua Juni, 2011.
Benki ya TD inadai kuikopesha FFAWN pesa Juni, 2011 na FFAWN ilikubali kulipa ifikapo Desemba, 2011, lakini mpaka sasa, benki hiyo imepokea kiasi cha Dola za Marekani 368.33 tu.
Sasa, Mary amesema, "Kama mwanzilishi na Mtendaji Mkuu wa FFAWN, nawajibika kwa kila kitu kilichokwenda hovyo. Tatizo ni kwamba sikuwa na watu sahihi katika maeneo mwafaka ili kufanya vitu sahihi. Hii haikutakiwa kuruhusiwa kutokea, lakini imetokea na sasa tunarekebisha."
Mwimbaji huyo amesema anafanya kazi bila kuchoka na timu yake mpya ya wataalamu 'kuirejesha Taasisi hiyo kwenye mstari, kulipa madeni mbalimbali na na kusimamia kikamilifu majukumu ya FFAWNS.'

BARUA YA MICHAEL JACKSON KUELEZA KINACHOMSIBU YAANIKWA...


Barua ya Michael Jackson aliyoandika kwenda kwa Lisa Marie Presley akilalamika kuhusu tatizo ambalo pengine ndilo lililosababisha kifo cha Mfalme huyo wa Pop Duniani imetua rasmi mezani mwa kampuni ya mnada.
Lisa Marie hakusema kwanini anataka barua hiyo inadiwe, lakini ni dhahiri kwamba Michael alikuwa akisumbuliwa na matatizo ya kukosa usingizi kwa miaka mpaka alipopata suluhisho la haraka kwa kutumia dawa aina ya Propofol.
Barua hiyo iliyoandikwa kati ya mwaka 1993 na 1996, inasomeka kama ifuatavyo: "Nusa hapa (mshale ukielekeza kwenye kisanduku). Lisa nahitaji kwa dhati mapumziko. Sijapata usingizi kwa siku nne sasa. Nahitaji kuwa mbali na simu na wafanyabiashara. Lazima nichukue tahadhari kuhusu afya yangu kwanza, napagawa kwa ajili ya penzi lako."
Julien' Auction ya mjini Beverly Hills, kampuni ileile iliyouza Nyaraka za siri za Elvis Presley imekabidhi kwa hiari kwa binti wa Elvis.
Mmiliki wa kampuni hiyo, Darren Julien ameeleza, "Nafikiri ni kitu binafsi, na tulitaka kuheshimu ombi na kuendeleza mahusiano mazuri na Lisa."

JICHO LA TATU...

UJEURI NA KIBURI CHA DENNIS RODMAN WAFIKIA TAMATI...

Ujeuri na kiburi cha mwigizaji na mchezaji mpira wa kikapu nyota, Dennis Rodman umefikia ukingoni pale alipochimbiwa mkwara mzito, "kama hautafanya Jaji atakushukia kama nyundo."
Jaji wa Mahakama ya Orange County alikuwa akisikiliza kesi ya madai dhidi ya Rodman kukwepa kulipia fedha kiasi cha Dola za Marekani 808,935 za kusaidia matunzo ya watoto wake wawili, mmoja wa miaka 9 na mwingine 10, na ziada ya malimbikizo Dola za Marekani 51,441.
Rodman amewekwa chini wa uangalizi wa miaka mitatu na kuamriwa kufanya kazi za kusaidia jamii jumla ya masaa 104.
Wakati akiwa chini ya uangalizi, Rodman anatakiwa kuwa karibu na malezi ya watoto hao na kugharimia mahitaji yao. Haikuwekwa wazi jinsi atakavyotumikia adhabu hizo.
Siku zilizopita Rodman alijibu madai hayo ya mke wake wa zamani, Michelle kwa kusema hawezi kulipa sababu walikwishatengana.
Kwa mujibu wa Dennis, madai Michelle yanahusisha amri ya malipo ya Dola za Marekani 50,000 kila mwezi kwa ajili ya matunzo ya watoto aliyokuwa akidai.
Rodman amekuwa akipambana tangu mwana 2010 kupinga hilo.
Ni dhahiri kwamba, Jaji hakununua kile alichokuwa akiuza Dennis!

KWA WANAOJUA KIMOMBO...

Unataka kuanza kupiga maji sehemu, kisha unatupa macho na kukutana na bango kama hili kwenye kona...

NGWASUMA WALIPOSHAMBULIA MAKUMBUSHO...


Linapofikia suala la kushambulia jukwaa, vyeo yote huwekwa kando! Hapa Rais wa FM Academia, Nyoshi El Saadat akionesha umahiri wake wa kusakata Ngwasuma sambamba na wenzake katika onesho la bendi hiyo lililofanyika Jumamosi iliyopita kwenye Kijiji cha Makumbusho Kijitonyama, Dar es Salaam. (Video ya ziro99blog).

ZIRO PLUS...

LADY MADONNA AUPONDA WIMBO WA LADY GAGA...


Mwimbaji mashuhuri duniani, Lady Madonna alipiga wimbo wa Lady Gaga uitwao "Born This Way" wakati wa mazoezi kujiandaa kwa tamasha mjini Tel Aviv, nchini Israel.
Madonna hakufanya hivyo kwa nia nzuri bali alitaka kukumbushia mashabiki wake madai kwamba wimbo huo ni marudio aliyofanya Lady Gaga kutoka katika wimbo wa Madonna uitwao "Express Youself".
Wakati wimbo wa "Born This Way" ukiingizwa mitaani, Madonna aliuponda hadharani akiita kuwa ni 'marudio ya kushangaza' ya wimbo wake wa 'Express Youself' kisha kuuita usiokuwa na maana.
Upande wake, Lady Gaga ameita maoni ya Madonna kuwa 'yamepitwa na wakati'.

CHEKA TARATIBU...

Wajinga wawili Juma na Jeba walikuwa wakichimba mtaro wakati wa jua kali sana. Juma akamwambia mwenzake, "Kwanini sisi tuko hapa kwenye mtaro wakati bosi wetu kajificha kwenye kivuli cha mti?" Jeba akajibu, "Sijui bwana." Juma akasema, "Nakwenda kumuuliza."
Akaenda moja kwa moja kwa bosi wake na kuuliza, "Kwanini sisi tunachimba mtaro juani wakti wewe umejificha hapa kivulini?" Bosi akajibu, "Werevu." Juma akauliza, "Unamaanisha nini Werevu?" Bosi akasema, "Vizuri, nitakuonesha. Nitaweka mkono wangu kwenye mti huu nataka upige ngumi kwa nguvu zako zote." Juma akavuta kasi na kurusha ngumi kwa nguvu akijaribu kupiga mkono wa bosi. Yule bosi akaondoa mkono wake pale na ngumi ya Juma ikatua kwenye mti. Kisha bosi akasema, "Huu ndio Werevu!"
Juma akarudi kwa mwenzake. Jeba kamuuliza, "Kasemaje?" Juma akajibu, "Kasema tupo hapa juani sababu ya Werevu." Jeba akauliza, "Werevu ndio nini?" Juma akajiziba uso wake kwa mikono na kusema, "Chukua chepeo lako halafu piga mikono yangu hapa kwa nguvu zako zote!" Duh… hebu pata picha kilichotokea. Ama kweli ujinga gharama...

ZIRO PLUS...

WAZAZI WA WATOTO 6 WALIOTEKETEKEA MOTO WATIWA MBARONI...

Bwana na Bibi Philpott wakiwa na watoto wao kabla ya tukio. KULIA: Wakiangua kilio wakati wa mkutano na waandishi wa habari baada ya kukamatwa jana.
Baba na mama wa watoto sita waliokufa baada ya nyumba yao kuteketea kwa moto wamekamatwa jana wakituhumiwa kwa mauaji ya watoto hao.
Katika mwendelezo wa aina yake, Mick Philpott mwenye miaka 55 na mkewe Mairead mwenye miaka 31 wanashikilia na polisi wakihojiwa na wapelelezi kuhusiana na tukio hilo la kutisha.
Takribani wiki mbili zilizopita wanandoa hao, wote wenyeji wa Derby, walishindwa kujizuia na kumwaga machozi kwenye mkutano uliovuta hisia na waandishi wa habari huku wakati maofisa wa polisi wakielezea jinsi petroli ilivyomwagwa na kuwashwa moto.
Jade Philpott mwenye miaka 10 na wenzake John mwenye miaka 9, Jack mwenye miaka 7, Jessie mwenye miaka 6, na Jayden mwenye miaka mitano, wote walifariki dunia baada ya moto na moshi kuzuka kwenye nyumba yao ya Halmashauri ya Jiji huko Allenton, mjini Derby.
Kaka yao Duwayne mwenye miaka 13 alifariki akiwa hospitalini kutokana na majeraha siku chache baadaye huku wazazi wake wakiwa wamemzunguka kitandani.
Mkuu Msaidizi wa Polisi Konstebo Steve Cotterill alisema jana: "Nahisi kuna watu wamebaki na taarifa muhimu ambao bado hawajajitokeza kuongea nasi.
"Katika mtazamo wa kukamatwa, ningeshauri ambao wamenyamaza na taarifa, wakiwa hawapendi kusikika maoni yao hadharani au hawajiamini, wafanye hivyo sasa.
"Binafsi nawahakikishia kwamba tutazifanyia kazi taarifa zao kwa umakini mkubwa.
"Bado tunahitaji taarifa za kutusaidia katika tukio hili.
"Kukamatwa hawa wa mwanzo ni hatua moja tu mbele katika uchunguzi.
"Ni muhimu sana kama unajua chochote kinachoweza kutusaidia, jitokeze sasa, usiendelee kusubiri tena.
"Ni muhimu kwamba tunatafuta haki ya hawa watoto sita."
Cotterill amefafanua kwamba uchunguzi bado unaendelea na kwamba ni mlolongo mrefu sana.
Aliongeza: "Japokuwa moto ulitokea zaidi ya wiki mbili zilizopita, hili ni tukio lenye utata na itatuchukua muda mrefu kuliunganisha pamoja tukio hili kuanzia jioni ya janga lenyewe.
"Nafahamu kesi hii imeigusa mno jamii na wakazi wanahitaji majibu jinsi lilivyotokea na kwa sababu gani.
"Lakini ningewataka wawe watulivu na kuendelea kuonesha ushirikiano waliotupa mpaka sasa. Uchunguzi wetu ni wa kina na kuumiza na itawachukua muda mrefu."
Wiki moja iliyopita, polisi waliondoa basi dogo na trela lake linalodhaniwa lilikuwa likitumiwa kama makazi ya ziada kwa familia hiyo, huku bwana na bibi Philpott mara moja moja wakilala humo nje ya nyumba.

Tuesday, May 29, 2012

MAOFISA MAGEREZA 59 WAVALISHWA NISHANI ZA MWENGE WA UHURU...


Kamishna Mkuu wa Magereza, Augustino Nanyaro (kulia) akimvisha nishani, SSP Polisi Matata Kirangi.

Kamishna Mkuu wa Magereza, Augustino Nanyaro (kulia) akimvisha nishani, SSP George Ng’honono Mpangalimi.
Kamishna Mkuu wa Magereza, Augustino Nanyaro (kulia) akimvisha nishani, SP Evangelina Kauseni Lyimo.
Baadhi ya Maofisa wa Magereza waliovishwa nishani hizo wakifuatilia kwa makini sehemu ya matukio.
Kamishna Mkuu wa Magereza, Augustino Nanyaro (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Maofisa wa Magereza muda mfupi baada ya kuwavisha Nishani ya Mwenge wa Uhuru Daraja la Nne.

UCHUNGUZI WA KIFO CHA BONDIA TAPIA WAANZA RASMI...


Mamlaka leo zilitarajiwa kufanya uchunguzi kuhusu Johnny Tapia, ikiwa siku mbili baada ya bondia huyo kukutwa amekufa nyumbani kwake, imefahamika.
Vyanzo vya kisheria vimeeleza kuwa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa New Mexico ilipanga kufanya uchunguzi wa kifo hicho ikiwamo matumizi ya dawa za kulevya kujua sababu hasa za kifo chake.
Kama ilivyoripotiwa awali, mwili wa bingwa huyo mara tano wa dunia ulikutwa na ndugu zake Jumapili iliyopita jioni. Polisi walisema hakuna aliyekamatwa kuhusiana na kifo hicho.
Tapia amefariki akiwa na umri wa miaka 45.

KUTOKA MAGAZETINI LEO...

              HABARI ZILIZOSISIMUA             

KANISA LACHOMWA ZANZIBAR
Kanisa Katoliki Parokia ya Mpendae limechomwa moto jana na watu wasiojulikana ikiwa ni mfululizo wa matukio ya kuchomwa makanisa Visiwani Zanzibar baada ya lile la Assemblies of God wiki iliyopita.
Kiongozi wa Kanisa hilo, Ambaros Mkenda, alidai kwamba Kanisa hilo lilichomwa moto na kusababisha uharibifu mkubwa.

Alidai Kanisa hilo lilichomwa moto jana saa 8.30 mchana na watu wanaohisiwa kuwa wafuasi wa Jumuiya ya Kiislamu ya Uamsho, waliokuwa wakitoka katika Mahakama ya Mwanakwerekwe kusikiliza kesi ya wenzao waliokamatwa juzi. Habari zaidi pata nakala yako sasa! 
-HABARILEO Mei 29.


AMUUA BABA, AMJERUHI MAMA YAKE
Polisi wa Mpanda mkoani Katavi inamshikilia Leocadus Maembe (41), wa kijiji cha Kasinde, tarafa ya Kabungu kwa madai ya kumwua baba yake mzazi, kwa mapanga kwa kinachodaiwa ni ugomvi wa shamba.
Pia inadaiwa kuwa mshitakiwa huyo alimshambulia na kumjeruhi pia mama yake mzazi, Olievetha Mwaisanga aliyeingilia ugomvi huo ili kuwasuluhisha baba na mwanawe.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi, Joseph Myovela alisema jana kuwa mauaji hayo ya Anthony Costantino ‘Kajalanga’ (69), yalifanyika Mei 19 saa 2 usiku jirani na nyumba ya marehemu huyo kijijini hapo. Habari zaidi pata nakala yako sasa!
-HABARILEO Mei 29.

KWA WANAOJUA KIMOMBO...

Inakuwaje unapokutana na bango kama hili?

ZIRO PLUS...

APIGWA RISASI AKITAFUNA USO WA MWENZAKE HADHARANI...

Tukio la polisi kumpiga risasi na kufa mtu aliyekuwa kitafuna uso wa mwenzake huku akiwa uchi limenaswa kwenye kamera za CCTV.
Picha hizo zinaonesha miguu ya wanaume wawili ikichomoza kwenye daraja la waenda kwa miguu mjini Miami wakati gari la polisi likiwasili eneo la tukio.
Polisi walimpiga risasi mtu huyo wakifikiri kufanya hivyo kutamaliza shambulio hilo, lakini aliendea kumng'ata mtuhumiwa wake jambo lililowashawishi kuendelea kumpiga risasi karibu mara 12 mpaka alipokufa.
Mwanaume huyo alifariki dunia mara alipofikishwa kwenye hospitali ya jirani kufuatia majeraha makubwa aliyopata kutokana na shambulio hilo.
Si mwanaume aliyekuwa uchi au mtuhumiwa wake aliyeweza kutambuliwa.
Mwanamke mmoja alimtaarifu polisi aliyekuwa karibu kwamba ameona wanaume wawili wakipigana, vyanzo vya habari zimesema.
Mfululizo wa milio ya risasi ilisikika eneo la MacArthur Causeway kando ya Mtaa wa North 13th.
Polisi alipowakuta wanaume hao, mwanaume aliyekuwa uchi alikuwa katika harakati za kumtafuna mwenzake usoni, ambaye pia hakuvaa nguo yoyote, imeripotiwa.
Ofisa wa Polisi alimtaka mwanaume aliyekuwa uchi kuacha alichokuwa akifanya.
Lakini alipokaidi kusikiliza na kuendelea kumtafuna mwenzake, ofisa huyo akamfyatulia risasi, kwa mujibu wa vyanzo vya habari.
Licha ya kupata jeraha la risasi, mwanaume huyo hakuacha hivyo polisi akalazimika kumpiga risasi zaidi ya sita.
Kwa mashambulizi hayo ya risasi, mwanaume aliyekuwa uchi akawa amekufa, akiwa ameelekeza kichwa chake ardhini.kwenye njia ya watembea kwa miguu jirani kabisa na maegesho ya magari ya Ofisiza gazeti la The Herald.
Msemaji wa Polisi, Javier Ortiz alisema kwamba kwa mujibu wa taarifa alizopokea, polisi aliyefyatua risasi 'ni shujaa na ameokoa maisha'.
Mtuhumiwa alisafirishwa kwenda Hospitali ya Jackson Memorial Ryder Trauma Center na kusema amekuwa akiugulia majeraha makubwa.
Wachache sana wanafahamu sababu zilizopelekea shambulio hilo, lakini polisi wanahisi kuwa mwanaume huyo aliyekuwa uchi hakuwa na sehemu ya kuishi.
Shahidi Larry Vega alisema: "Nilimsimamisha polisi wa Jiji la Miami na kumtaarifu kwamba mtu mmoja wa mitaani anamuua mtu kwa kumng'ata na kumrarua usoni."
"Polisi alimkabili mtu huyo na kama mbwa kichaa jamaa huyo akamgeukia polisi. Hapo polisi akampiga risasi mara nne," aliongeza.
Hakuna silaha yoyote iliyokutwa jirani na watu hao wawili, ikiongeza imani kuwa mshambuliaji alitumia nguvu yake binafsi kumdhuru mtuhumiwa wake.

ZIRO PLUS...

MWIMBAJI MARY J. BLIGE SASA 'AGEUKA TAPELI'...

Taasisi inayomilikiwa na mwimbaji Mary J. Blige inapokea zaidi kuliko kuchangia, hii ni kwamujibu wa benki moja inayodai kuikopesha taasisi hiyo Dola za Kimarekani 250,000 lakini ikaambulia kulipwa Dola za Kimarekani 400 tu.
Imebainika Taasisi ya 'Mary J. Blige and Steve Stoute Foundation For The Advanced Of Women Now' inashitakiwa na Benki ya TD kutokana na mkopo wa Dola za Kimarekani 250,000 ilizokopa tangu Juni, 2011.
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka zilizopatikana mapema mwezi huu mjini New York, Taasisi hiyo iliahidi kulipa pesa hizo kabla ya Desemba 2011, lakini ulipofika wakati kulipa pesa hizo taasisi hiyo iliingiza kwenye akaunti kiasi cha Dola za Kimarekani 368.33 pekee.
Benki inadai ilitaka kuhakikishiwa malipo kwa maandishi Februari 7 na 29, lakini haikupata majibu yoyote kutoka kwa taasisi hiyo.
Kesi hii ni moja tu ya mlolongo wa madai mengi yanayoikabili taasisi hiyo. Mwaka 2010 imeshindwa kulipa kodi ya serikali huku pia ikidaiwa na mwanamuziki tangu mwaka 2011 anayedai malipo yake kwa kutumbuiza katika tamasha la kuchangisha fedha akisema ilipofika muda wa kudai chake, taasisi hiyo ikaingia mitini.
Mwakilishi wa Blige alisema, "Mary J. Blige and Steve Stoute Foundation For The Advanced Of Women Now, Inc. (FFAWN) ipo kwenye pilika za kubadili menejimenti yake na makao makuu."
Aliongeza, "Tumebakiwa na jukumu pekee la kusaidia wanawake kuweza kujiamini na ujuzi muhimu kuweza kumudu vipaumbele vyao."

CHEKA TARATIBU...

Mmasai mmoja kaalikwa kwenye harusi ya Waarabu. Wakati wakiwa ukumbini waalikwa wote pamoja na yule Mmasai wakapewa tende na haluwa. Baada ya kula, wakati wa kwenda kuwapongeza maharusi, Mmasai akatumia nafasi hiyo kumnong'oneza bwana harusi, "Aisee rafiki, hii ugali yenu tamu sana ila muchusi yake iko chungu mno!" Akimaanisha tende zilikuwa tamu ila haluwa balaa…

JICHO LA TATU...

Monday, May 28, 2012

MSANII LULU AFIKISHWA MAHAKAMA KUU KUSIKILIZA KESI YAKE YA MAUAJI...

Msanii wa filamu Elizabeth Michael (Lulu) akiwa amezungukwa na walinzi kwenye Mahakama Kuu Dar es Salaam leo kusikiliza mashitaka dhidi yake ya tuhuma za kumuua mwigizaji maarufu marehemu Steven Kanumba. (Na Mpigapicha Maalumu).  

MACHINJIONI YAANZA TENA KUSAKA ROHO ZA WATU...


Ajali mbaya imetokea mchana huu kwenye makutano ya Barabara za Chang'ombe na Mandela eneo maarufu kwa ajali la 'Machinjioni' ambapo daladala aina ya Mitsubishi  Rosa lenye namba za usajili T 987 BDH linalofanya safari kati ya Mwenge na Temeke na gari dogo aina ya Suzuki Grand Vitara mali ya Legal Sector Reform Program lenye namba T 305 AEN. Cha ajabu kwenye makutano hayo kuna taa za kuongozea magari ambazo zilifanya kazi kwa siku mbili tu na kisha zikazimwa. Baada ya hapo kila mara zimekuwa zikitokea ajali mfululizo kutokana na kila dereva kujiona ana haki! Kituko ni kwamba baada ya ajali kutokea ndipo akaja askari wa usalama barabarani na kuanza kazi ya kuongoza magari. Uzembe huu mpaka lini?
Mmoja wa mashuhuda akilitazama gari dogo lililoharibiwa vibaya katika ajali hiyo. (Picha zote na mpigapicha maalumu).

GF TRUCKS YAIKABIDHI MITAMBO YA UJENZI HALMASHAURI YA NJOMBE...


Spika wa Bunge, Anne Makinda ambaye pia ni Mbunge wa Njombe Kusini (wa pili kushoto) akikabidhiwa mfano wa funguo ya mitambo mbalimbali ya ujenzi wa barabara na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya GF Trucks, Imran Karmali ikiwa kama ishara ya makabidhiano ya mitambo hiyo kwa ajili ya ujenzi wa barabara za Halmashauri ya Njombe wenye thamani ya shilingi milioni 716. Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni hiyo, Mehboob Karmali na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Njombe, George Mkindo.
Mbunge wa Njombe Kusini, Spika Anne Makinda akijaribu moja ya mitambo iliyokabidhiwa kwa Halmashauri ya Njombe na Kampuni ya GF Trucks leo jijini Dar es Salaam. Anayeshuhudia ni Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Imran Karmali.

TBL YAZINDUA CASTLE LITE YA KOPO...

Meneja Mawasiliano na Mahusiano wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), Edith Mushi akizungumza na waandishi wa habari mapema leo kuhusu bia ya Castle Lite ya kopo wakati wa uzinduzi uliofanyika Dar es Salaam. Kushoto ni Meneja wa Bia hiyo, Pamela Kikuli. 
Huu ndio muonekano wa Castle Lite mpya ya kopo. (Picha zote na Mpigapicha Maalumu).

TWIGA STARS WAREJEA DAR...

Wachezaji na viongozi wa timu ya Taifa ya soka ya Wanawake (Twiga Stars) wakiwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam mchana huu wakitokea nchini Ethiopia walikocheza na wenzao wa huko jana na kufungwa mabao 2-1.

BONDIA JOHNNY TAPIA AFARIKI DUNIA...


Bondia Johnny Tapia ameripotiwa kufariki dunia jana.
Wanafamilia wamesema Polisi wa Albuquerque waliitwa nyumbani kwa Tapia majira ya saa 1:45 usiku baada ya wanafamilia kugundua mwili wake.
Polisi wamesema kifo chake ni cha kawaida, lakini sababu rasmi ya kifo chake bado haijajulikana.
Tapia, ni bingwa wa dunia mara tano. Mke wake ameshitushwa na janga hilo. Baba wa Tapia aliuawa wakati mama yake akiwa na ujauzito wake. Na Tapia alipokuwa na miaka nane, mama yake alitekwa nyara, kubakwa na kunyongwa.
Tapia alilazwa hospitali mwaka 2007 akiwa katika hali mbaya kutokana na kutumia dozi kubwa ya cocaine. Siku moja baada ya kulazwa, shemeji yake na mtoto wa dada yake walikufa kwenye ajali ya gari wakiwa njiani kwenda kumtembelea hospitalini.

JUSTIN BIEBER ASAKWA KWA KUMDUNDA PAPARAZZI...


Mwimbaji Justin Bieber anasakwa kwa tuhuma za kumshushia kisago mpigapicha aliyekuwa akijaribu kupata picha ya Bieber wakati akiwa kwenye Duka la The Commons, mjini Calabasas anakoishi.
Imeelezwa baada ya kurushiana maneno ndipo Justin akamvaa mpigapicha huyo na kuanza kumshushia masumbwi kabla ya kutokomea na mpenzi wake kusikojulikana.
Mpigapicha huyo alipiga simu polisi ambao hata hivyo walifika wakati Bieber na mpenzi wake, Selena Gomez wakiwa wameshakimbia eneo la tukio.
Mpigapicha huyo alikuwa akilalamika maumivu sehemu mbalimbali mwilini na ikalazimu kuchukuliwa kwa gari la wagonjwa kupelekwa hospitali kwa matibabu. Alitibiwa na muda mfupi baadaye kuruhusiwa.
Wakati polisi wanachunguza tukio hilo, imeelezwa na baadhi ya mashuhuda kwamba wanasheria walimfuata mpigapicha na kushawishi kwamba anaweza kutengeneza pesa nyingi kutokana na tukio hilo na kwamba wakamtaka aripoti polisi na kuita gari la wagonjwa.
Mashuhuda waliongeza kwamba mpigapicha huyo alikuwa amelizuia gari la Bieber wakati akijaribu kuondoka. Mwimbaji huyo akashuka kwenye gari na kumtaka mpigapicha huyo kupisha njia lakini akagoma na mzozo kuanza.

BURUDANI WIKIENDI HII...



Kufuatia maombi yenu wasomaji wetu, tumewasikia na kuwaletea utamu zaidi: Katika pitapita yetu wikiendi hii kamera yetu ikaweza kukunasia kidogo burudani ya kufa mtu pale bendi ya FM Academia maarufu kama Wazee wa Ngwasuma walipofanya kufuru ndani ya Kijiji cha Makumbusho, Kijitonyama, Dar es Salaam, usiku wa Jumamosi. Pata burudani na bila kusahau wiki ijayo utaona shoo ya  Wazee wa Kibega, si wengine bali ni Mashujaa Musica LIVE ON STAGE!  (Video ya ziro99blog).


JICHO LA TATU...

MHAMIAJI HARAMU AKATISHA MAISHA YA WASTAAFU 'MAKINI'...

JUU: Eduard Mereohra (kushoto).  KATIKATI: Wastaafu David na Dorothy Metcalf enzi ya uhai wao. CHINI: Eneo la ajali ambapo gari la wastaafu hao likiwa nyang'anyang'a (lenye rangi ya bluu). KULIA: Mtoto wa wastaafu hao, Clive Metcalf.
 Familia ya wanandoa waliouawa na mhamiaji haramu aliyekuwa akiendesha gari huku amelewa imelaumu mamlaka za Uingereza zinazohusika na ulinzi wa mipaka.
Mhamiaji Eduard Mereohra mwenye miaka 26 alifukuzwa nchini humo mwaka 2009 lakini akarejea tena miezi michache baadaye.
Katika sherehe moja ya Mwaka Mpya, alikuwa akinywa pombe kwenye sherehe siku moja kabla ya kulibamiza gari lake kwenye gari lililobeba wazee David na Dorothy Metcalf na kuwaua wote na kutenganisha familia hiyo kwa vilio.
Juzi, baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka tisa jela, familia ya wanandoa hao ilisema wangekuwa bado wako hai sasa kama mfumo wa uhamiaji usingewaangusha.
Wamewataka maofisa kuchunguza jinsi gani raia huyo wa Moldova aliweza kukwepa mamlaka husika mipakani.
Mahakama imeelezwa kwamba Meheohra hakuwahi kupata kibali cha kufanya kazi wala namba ya bima ya taifa kwa jina lake halisi, lakini usiku wa jana yake hii ikafahamika kwa Wizara ya Mambo ya Ndani na Idara ya Kazi na Pensheni.
Nje ya Mahakama, kijana wa wanandoa hao Clive alisema: "Mama na Baba walikuwa wachapakazi, walipakodi waaminifu waliojipanga vizuri kwa kustaafu kwao na wangeweza kuwa na miaka 20 zaidi ya kuburudika pamoja.
"Wakati tukimshikilia Mereohra kutokana na kuhusika na tukio hili, tunahisi kwamba mama yetu na baba wangekuwa hai leo kama mfumo usingeshindwa kwa kumruhusu mtuhumiwa kuingia Uingereza.
"Tulikuwa karibu sana na familia na tumepotea bila wao. Hakuna hukumu inayoweza kutosha kwa mtu aliyebadilisha maisha yetu milele katika Siku ya Mwaka mpya 2012, alipochukua uhai wa wazazi wetu na mababu wa watoto zetu, kupitia kukosa fikra, hatari na vitendo vya uvunjaji sheria."
Meheohra aliwasili Uingereza Oktoba 2008, na kuomba uraia mwaka uliofuata. Maombi yake yalikataliwa na kurejeshwa Austria, ambako baadaye aliomba uraia Desemba 2009.
Lakini Aprili 2010 alireudi kwa njia za panya nchini humo kwenye lori lililokuwa likiendeshwa na raia wa Romania.
Wakati wa ajali alikuwa akiishi Burley, mjini Leeds na kufanya kazi kama kibarua. Siku ya Mwaka Mpya, alikunywa bia, wiski na shampeni kwenye tafrija usiku wa kuamkia siku ya ajali, akiendesha gari lake aina ya Volvo C70.
Mashabidi wamemuelezea alikuwa akiendesha kwa spidi kubwa kwenye barabara kuu nje ya Leeds, kwa fujo akilazimisha magari mengine yampishe njia.
Akaishia kujibamiza nyuma ya gari la Metcalf aina ya Fiat Panda akiwa kwenye mwendokasi unaofikia kilometa 100 kwa saa na kuruka juu umbali wa futi 10 kabla ya kutua chini kwa kishindo.
Bwana Metcalf mwenye miaka 68 kutoka Leeds aliyekuwa akiendesha, alitupwa nje ya gari na kufa papo hapo. Mkewe mwenye miaka 65 alikutwa akining'inia kwenye dirisha la nyuma na lifariki baadaye.
Mereohra aliyekuwa Ć¢melewa mara mbili ya kiwango kinachoruhusiwa, alijaribu kukimbia lakini akadhibitiwa na watu waliokuwa jirani.
Baadaye alijaribu kulaumu tukio hilo kwamba limesababishwa na Metcalf, mhandisi ukarabati mstaafu.
Juzi kwenye Mahakama ya Leeds alihukumiwa kifungo cha miaka tisa jela kwa kusasababisha vifo kutokana na uendeshaji wake wa hatari, ambapo alikiri mashitaka hayo katika hatua za awali za kesi hiyo.
Akitoa hukumu, Jaji Geoffrey Marson alisema Meheohra alifanya 'makusudi kuendesha kwa kasi' na alitumia gari lake kama silaha.
Baadaye Clive Metcalf alisema: "Tumekuwa tukiambiwa kwamba ameomba radhi, lakini hatukubali kwamba hizo ni taarifa rasmi za kuomba radhi.
"Aliamua kuja nchini kinyume cha sheria; aliamua kunywa usiku mzima na kuendesha gari; aliamua kuendesha gari kwa mwendo mkali sana akivunja sheria za barabarani; aliamua kujaribu kukimbia eneo la ajali mbaya na kukana hakuwa dereva na kugomea kupimwa kama alikuwa kalewa.
"Kufuatia yote hayo, tunadhani kitu pekee anachoomba msamaha ni kwamba amekamatwa."