Friday, June 20, 2014

SERIKALI YATANGAZA BEI ELEKEZI YA PAMBA


Serikali kupitia Bodi ya Pamba imetangaza bei elekezi ya ununuzi wa  pamba ambayo ni Sh 750 kwa kilo  katika msimu wa mwaka 2014/15.
Makamu Mwenyekiti wa Bodi hiyo, George  Wasira alisema msimu uliopita bei elekezi ilikuwa Sh 700 kwa kilo na kwamba ongezeko hilo la Sh 50 limefikiwa na wadau wa zao la pamba nchini kutokana na kuporomoka kwa bei ya zao hilo katika Soko la Dunia.
Bei hiyo ilitangazwa juzi wakati wa uzinduzi wa msimu mpya wa ununuzi wa pamba uliofanyika kitaifa katika kijiji cha Isole  wilayani Sengerema mkoani Mwanza.
 “Baada ya tathmini ya kina kufanyika iliyolenga kulinda maslahi ya wadau wote yaani wakulima na wanunuzi, bei elekezi itakuwa Sh 750,” alisema Wasira
Hata hivyo bei hiyo elekezi haikupokewa kwa furaha na wakulima wa zao hilo wilayani Sengerema kwa madai kuwa wamekuwa wakitumia gharama kubwa katika uzalishaji halafu wanauza kwa bei ndogo.
Miongoni mwa waliozungumza kwenye uzinduzi huo, walisema wamekuwa  wakitumia gharama kubwa kwenye uzalishaji kuanzia kulima, dawa za kunyunyuzia pamoja na palizi hivyo bei hiyo elekezi inawanyonya.
Akizindua msimu  wa ununuzi wa pamba 2014/2015, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Baraka Konisaga  alionya wanunuzi wa pamba wanaowaibia wakulima kwa kutumia mizani.
Aidha taarifa zinaonesha uzalishaji wa zao hilo nchini  unatarajiwa kuongezeka msimu huu kutoka kilo milioni 245 mwaka 2013/2014  hadi kufikia kilo milioni  250.

No comments: