Friday, June 20, 2014

BABA NUSURA AMNYONGE MWANAWE KWENYE MWEMBE


Mkazi wa Kijiji cha Nyamuswa, wilayani Bunda Mkoa wa Mara,  Sumera Sungura (28), anashikiliwa na Polisi akituhumiwa kutaka kunyonga mtoto wake wa kufikia kwa kumning’iniza kwenye mti wa mwembe.
Polisi imetaja mtoto aliyetaka kuuawa ni Adamu Adamu (5). Kwa mjibu wa Mwenyekiti wa Dawati la Jinsia wa Kituo Kikuu cha Polisi Wilaya ya Bunda, Ritha Charles, tukio hilo ni la Juni 6, mwaka huu kijijini hapo.
Inadaiwa baba huyo alitaka kufanya kitendo hicho  wakati mama wa mtoto huyo, Nyabakira Adamu alipokuwa amelazwa hospitalini.
Ofisa huyo wa Polisi alidai, baba huyo alikamatwa juzi na kwamba leo atafikishwa mahakamani, kujibu tuhuma ya kukusudia kuua mtoto huyo.
 Taarifa zinadai  mtoto huyo ambaye mama yake alimzaa kabla kuolewa na mtuhumiwa huyo, alinusurika kifo baada ya mchungaji wa ng’ombe wa mtuhumiwa, kumkuta akining’inia kwenye mwembe povu likimtoka mdomoni. Alimnusuru kwa kukata kamba.
Akizungumza kwa tabu na mwandishi wa habari hizi, mtoto huyo alisema siku ya tukio baba yake huyo alimkuta barabarani na kumkamata na akaanza kumpiga akihoji sababu za kucheza barabarani.
Alieleza kwamba, baada ya kupigwa alifungwa kamba shingoni na kuning’inizwa mtini, na kisha baba yake alitokomea.
“Hakunipeleka hospitali, alikuwa ananipaka dawa ya ng’ombe hapa (anaonesha alama za majeraha) akinitishia kunipiga tena nikisema kwa watu,” alisema mtoto huyo.
 Aidha, ilielezwa kuwa baada ya tukio hilo mama mzazi wa mtuhumiwa huyo alipotaka kumchukua, ili akatoe taarifa Polisi juu ya unyama huo,  mtuhumiwa alimtishia na ndipo alipotoa taarifa kwa mama yake mdogo amfuate.
Bibi wa mtoto huyo, Nyanzara Mwikwabe , alisema alipata taarifa kutoka kwa majirani, na baada ya kumuona ana michubuko shingoni alimchukua na kumpeleka nyumbani kwake na kisha akatoa taarifa Polisi.
Ofisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Bunda, Beatrice Gwamagobe, alikiri kuwepo tukio hilo na kuongeza kuwa mtoto huyo juzi alifikishwa ofisini kwao na Mwenyeti wa Dawati la Jinsia kutoka Polisi Bunda.

No comments: