Saturday, June 21, 2014

GARI LATUMBUKIA MTONI NA KUUA, KUJERUHI WATU 6


Mtu mmoja amekufa na wengine sita wamejeruhiwa baada ya gari walilokuwa wamepanda kutumbukia kwenye Daraja la Kinyerezi jijini  Dar es Salaam.
Tukio hilo lilitokea Juni 19 ambapo gari lenye namba za usajili T142 BJM Scania, likiwa na tela namba T111 ALD, likiendeshwa na dereva ambaye hajafahamika, lililokuwa likitokea Pugu Kinyamwezi kuelekea Kinyerezi na mzigo wa tofali ukiwa ndani ya Kontena.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi alisema gari hilo lilitumbukia katika daraja hilo baada ya daraja kuvunjika  kutokana na gari hiyo kupita kwa nguvu.
Alisema  gari hilo,  lilitumbukia kutokana na dereva kukaidi amri ya walinzi wa daraja, ikiwa ni pamoja na alama za magari yanayoruhusiwa kupita.
Gari hilo lilikuwa na zaidi ya tani 30. Katika tukio hilo mbeba mizigo anayekadiriwa kuwa na miaka kati ya 20 na 25, alikufa papo hapo na wengine sita, watano kati yao ni wabeba mizigo na mmoja ni fundi walijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili.
Majeruhi hao ni Simon Kamai (22), Raphael George (20), Lameck Maliki(22), Chande Mohamed (23), Said Makame (25) na Simon Ennel (24) ambaye ni fundi ujenzi. Majeruhi walitibiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na waliruhusiwa. Maiti amehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Hali ya usalama imeimarishwa kwa kushirikiana na Kampuni inayojenga daraja hilo, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara, viashiria kwa daraja kama halitumiki kwa sababu ya kushindwa kulitoa gari hilo jitihada za kumtafuta dereva aliyekimbia baada ya tukio zinaendelea.

No comments: