Uamuzi wa ombi la marejeo
lililowasilishwa na washitakiwa tisa wa kesi ya mauaji ya watu 27, yaliyotokana
na kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16, utatolewa Juni 27 mwaka huu katika
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
Washitakiwa hao wanaiomba Mahakama
Kuu ipitie uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwanyima dhamana
bila kupewa haki ya kusikilizwa ili kujiridhisha na usahihi na uhalali. Pia
ipitie uamuzi wa kubadilishwa kwa mashitaka kutoka kuua bila kukusudia na kuwa
ya kuua kwa kukusudia.
Shauri hilo lilitajwa jana mbele ya Jaji
Salvatory Bongole ambaye alisema atatoa uamuzi wa ombi hilo pamoja na pingamizi
la awali lililowasilishwa na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) baada ya kupitia
hoja za maandishi zilizowasilishwa na pande zote mbili.
Katika ombi lao washitakiwa wanadai
upande wa Jamhuri ulibadili mashitaka bila kuijulisha Mahakama mazingira
yaliyosababisha wabadilishe, hivyo wanaiomba Mahakama itupilie mbali hati ya
mashitaka mapya ya kuua kwa makusudi badala ya kuua bila kukusudia na iamuru
wapewe dhamana.
Hata hivyo DPP amewasilisha pingamizi
akidai ombi hilo halipo sahihi kisheria,
Mahakama Kuu haina mamlaka ya kusikiliza ombi ambalo kesi yake ya msingi
ipo katika hatua ya awali pia ombi hilo linaungwa mkono na hati ya kiapo ambayo
ina mapungufu ya kisheria.
Washitakiwa waliowasilisha ombi hilo ni
Raza Ladha, Godluck Mbaga, Wilbroad Mugabisyo, Ibrahim Kisoki, Charles Ogare,
Zonazea Oushoudada, Michael Hemed, Albert Mnuo na Joseph Ringo. Awali walikuwa
wanakabiliwa na mashitaka ya kuua bila kukusudia, wakabadilishiwa mashitaka na
kuwa kuua kwa kukusudia.
Inadaiwa kuwa Machi 27 mwaka jana katika
mtaa wa Indira Gandhi, washitakiwa waliwaua watu 27 kwa kukusudia kutokana na
kuporomoka kwa ghorofa 16. Mshitakiwa mwingine ni aliyekuwa Mkurugenzi wa
Manispaa ya Ilala Gabriel Fuime ambaye hajawasilisha ombi hilo.

No comments:
Post a Comment