Mfuko wa Taifa wa Bima
ya Afya (NHIF) unaandaa vitambulisho
vipya vya wanachama wake vya kielektroniki.
Lengo la hatua hiyo ni kukabiliana
na matumizi mabaya
ya vitambulisho vya sasa,
ambavyo wanachama wasio
waaminifu wanavikodisha kwa
watu wengine kwa gharama
kubwa kinyume cha
utaratibu.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu
wa NHIF, Hamis Mdee alibainisha
hayo hivi karibuni katika ufunguzi
wa mkutano wa wadau wa NHIF, uliofanyika
mjini Sumbawanga.
Alisema baadhi
ya wanachama wa mfuko huo
wasio waaminifu, wamekuwa
ama wakiuza vitambulisho
hivyo au kuvikodisha, hususan
kwa watu wanaosumbuliwa na magonjwa makubwa, yakiwemo nyonga, figo na wale
wanaohitaji huduma ya
usafishaji wa damu.
Kwa mujibu wa Mdee,
gharama za matibabu
ya baadhi ya magonjwa hayo makubwa, hufikia zaidi ya Sh milioni 3.6
kwa mwaka.
Alisema baadhi
ya wanachama wa mfuko huo wasio waaminifu, huthubutu
kukodisha vitambulisho vyao
kwa zaidi ya Sh milioni
moja .
Alizitaka halmashauri
za wilaya na manispaa,
kutengeneza sheria ndogo
ili kujiunga katika Mfuko
wa Afya ya Jamii (CHF) iwe ni
lazima badala ya
hiari. Alisema hatua hiyo itaboresha
uhamasishaji kwa wananchi.
Sambamba na mkutano huo
wa wadau, pia NHIF ilitoa
msaada wa mashuka 180,
ambapo mashuka 80
yalitolewa kwa Hospitali Teule ya
Manispaa ya Dk Atman na 100 kwa
Hospitali ya Mkoa mjini Sumbawanga.
Kwa upande wake, Mkuu
wa Wilaya ya Sumbawanga, Mathew
Sedoyeka aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa
Rukwa, Stella Manyanya alibainisha
kuwa takwimu zinaonesha kuwa hamasa
ya wananchi kujiunga na CHF,
siyo ya kuridhisha mkoani humo.
“Lakini kwa upande wa pili,
inawezekana pia watoa huduma
mmekuwa ni chanzo cha kuwakatisha tamaa wananchi
wanaojiunga na CHF, hivyo
kusababisha wengine wasite kujiunga kutokana na huduma zisizoridhisha," alibainisha Sedeyeka.
Akifafanua, aliongeza kuwa ni kaya 20,157 kati ya 173,972 , sawa na asilimia 11.6
zimejiunga na CHF mkoani humo
hadi kufikia Machi 30, mwaka huu.

No comments:
Post a Comment