JAMBAZI LAUA WATATU AKIWAMO MKUU WA UPELELEZI WILAYA YA NEWALA...

Kamanda Zelothe Stephen.
Habari zilizotufikia hivi punde zinasema kuwa watu watatu akiwamo Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Newala wameuawa kwa kupigwa risasi na mtu anayesadikiwa kuwa ni jambazi muda mfupi uliopita.

Kwa mujibu wa mashuhuda, jambazi huyo aliyekuwa na bunduki aina ya SMG iliyokatwa kitako, alifika kwenye kituo cha mafuta cha Camel Oil mjini humo akijifanya anataka kununua mafuta.
Baada ya kupatiwa huduma, jambazi huyo alikwenda moja kwa moja kwenye ofisi ya karani wa kituo hicho ambapo alimwonesha bunduki na kumwamuru ampatie fedha.
Mashuhuda hao wamedai kuwa jambazi huyo alifanikiwa kupatiwa takribani Shilingi milioni tatu na kisha kutokomea vichakani.
Baada ya polisi kutaarifiwa tukio hilo, Mkuu huyo wa Upelelezi alifika eneo la tukio akiwa na askari wawili, ndipo ghafla jambazi hilo likaanza kufyatua risasi zilizowapata Mkuu huyo wa Upelelezi na askari polisi mmoja ambao walifariki papo hapo. Mtu mwingine aliyefariki ni raia mkazi wa mjini humo aliyetambulika kwa jina moja la Mustapha. Askari mwingine pia alijeruhiwa vibaya kifuani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Zelothe Stephen aliyefika eneo la tukio baada ya mauaji hayo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.
Mbali na hilo, Kamanda huyo alitangaza kuanzishwa kwa msako mkali ili kuweza kumtia mbaroni jambazi huyo pamoja na silaha yake hiyo.

No comments: