Sunday, December 8, 2013

VIJANA WA CHADEMA KIGOMA WAANDAMANA KUZIA ZIARA YA DK. SLAA...


Vijana hao wameandamana kwa kile kinachodaiwa ni kupinga adhabu aliyopewa Kabwe Zitto (pichani) na uongozi wa Chadema.

Wakati Katibu Mkuu wa  Chadema, Dk Wilbrod Slaa akiendelea na ziara yake wilaya ya Kasulu mkoani hapa, wanachama na wapenzi wa chama hicho, wamefanya maandamano makubwa ya kumtaka asikanyage wilaya ya Kigoma.

Katika maandamano hayo, yaliyohusisha pikipiki za bodaboda zaidi ya 100, magari, midundiko na magari yenye vipaza sauti jana, wanachama hao walioanzia maandamano yao nyumbani kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe eneo la Mwandiga walitembea umbali wa kilometa nane hadi viwanja vya Mwanga Centre.
Wakati wote wakiwa katika maandamano hayo,  waliongozwa na askari wa usalama barabarani huku gari la Polisi lenye askari zaidi ya wanane, likiwafuatilia kulinda usalama.
Wakitoa matamko baada ya kufika kwenye viwanja hivyo, baadhi yao waliojitambulisha kuwa viongozi wa Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA) wilaya za Kigoma Mjini na Vijijini, walimtaka Dk Slaa asitishe ziara hiyo ili kuepusha walichokiita maafa makubwa.
Mtoro Jafari ambaye alijitambulisha kuwa kiongozi wa BAVICHA Kigoma Kaskazini, alisema vijana hawakubaliani na uamuzi ya Kamati Kuu ya Chadema ya kumvua Zitto uongozi na kisha Dk Slaa kufanya ziara Kigoma.
“Chadema walichofanya ni sawa na jambazi kuua mtoto wako baadaye arudi kukupa pole wakati ukijua aliyemwua ni yeye, Dk Slaa anakuja kutusanifu na hatukubaliani na hilo, tunamwomba akatize ziara yake, aende mikoa mingine si Kigoma, kama ataendelea na ubishi basi ajue kitu kibaya kitamtokea,” alisema Mtoro.
Samuel Mzigama ambaye ni kiongozi wa BAVICHA Kigoma Mjini, alisema Zitto ndiye kila kitu kwao na ndani ya Chadema walimfuata yeye na si chama, kwani kimejaa ukabila kwa watu wa Kaskazini na anapojitokeza mtu wa mikoa mingine hufanyiwa fitna na kuondolewa kama alivyoondolewa Zitto.
Baadhi ya waandamanaji walibeba mabango yenye ujumbe kwamba ‘Zitto kwanza, Chadema  baadaye’; ‘Hatutaki chama cha Wachaga kituvuruge’; ‘Kigoma ni chuo cha siasa tunajua kudai haki zetu’; ‘Zitto ni mkombozi wa Watanzania’ na ‘Wachaga mna radhi ya Nyerere’.
Stumai Omari kiongozi wa Baraza la Wanawake la Chadema (BAWACHA) Kigoma Kaskazini alisema  Zitto ataendelea kuwa mtetezi wa Watanzania na hila za Dk Slaa na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kudhoofisha juhudi zake hazitafanikiwa.
Baada ya hotuba za viongozi hao, wanachama na wapenzi walioshiriki maandamano walikusanya na kuchoma kadi na bendera za Chadema huku wakiimba kuwa chama hicho kinawavuruga. Hatimaye msafara huo wa bodaboda na mdundiko ulirudi Mwandiga nyumbani kwa Zitto.
Viongozi wa Chadema Kigoma ambao hawakushiriki ziara ya Dk Slaa kwa kutoa udhuru hawakupatikana kuzungumzia hali hiyo na ziara nzima.
Akizungumza na mwandishi, Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kigoma, Zedekia Makunja alithibitisha kuruhusiwa kwa maandamano hayo ambayo alisema yalikidhi vigezo vya ibara ya 18 (a) ya Katiba ya nchi.
Makunja alisema viongozi hao wa BAVICHA walikuwa na nia ya kufikisha ujumbe kwa viongozi wao na Polisi kwa kutekeleza misingi ya Katiba iliruhusu maandamano hayo na kuwapa ulinzi ili kuhakikisha maandamano yanafanywa kwa amani bila vurugu.
Kamanda huyo alimshauri Dk Slaa aahirishe ziara yake mkoani Kigoma ili kusubiri vuguvugu hilo la maandamano litulie na badala yake wafanye mikutano ya ndani.
Hata hivyo, alisema Polisi imejipanga kuhakikisha amani na utulivu vinadumu kama kiongozi huyo ataendelea na ziara yake.

No comments: