Sunday, December 8, 2013

HIVI NDIVYO YATAKAVYOKUWA MAZISHI YA MZEE NELSON MANDELA...


Gari maalumu likiwa limebeba mwili wa Mzee Nelson Mandela (kulia).

Kwa Waxhosa wa Afrika Kusini, kifo kwa jadi si kitu cha kuzungumzia au kupanga, hata kama kipo au kinakaribia.

Lakini walio karibu na Nelson Mandela hawakuwa na chaguo wakati kiongozi mweusi wa kwanza wa Taifa hilo, akiwa amelazwa katika hospitali ya Pretoria na kisha nyumbani kwake Johannesburg akisaidiwa na mashine.
Katika maisha yake ya mwisho, mipango iko hadharani kati ya Serikali, Jeshi na familia yake wakati wakijiandaa kwa hafla ya kumuaga shujaa huyo.
Ifuatayo ndiyo mipango iliyo katika siku 10 zijazo za maandalizi ya maziko  ya kitaifa ambayo yatatangazwa moja kwa moja kwa mamilioni ya watu duniani lakini pia tukio la faragha la kumuaga litakalofanywa na walio karibu naye.
Lakini kama ilivyo kwa matukio makubwa kama haya, mipango inaweza kubadilika kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, usalama na sababu zingine. Lakini kwa sasa, haya ndiyo ambayo Mamlaka husika na familia wanatarajia kutokea.  
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari, vinavyohusika na mipango hiyo,  siku hizo 10 za maombolezo zitahusisha mila za kimagharibi na za kithembu za ukoo wa Mandela.
Mandela alifariki dunia Alhamisi saa 2.50 (saa 3.50 saa za Afrika Mashariki) usiku, akiwa amezingirwa na familia yake, Rais Jacob Zuma alisema. CNN inaeleza kuwa wakati wa saa zake za mwisho, Mandela pia alikuwa amezingirwa na wazee wa kithembu. La muhimu wakati fulani- ama nyumbani kwake au mochari-wazee wa kimila wangekutana kufanya sherehe ya awali, kimila inaitwa ‘kufumba macho’.
Katika sherehe hiyo, watakuwa wanazungumza na Mandela, lakini pia na mizimu yake ya kimila, kuelezea kinachotokea kila hatua ili kurahisisha safari ya kuachana na maisha ya kawaida na kuingia mengine.  Baada ya sherehe hizo, mwili wa Mandela  utawekwa dawa za kuuzuia kuharibika ndani ya mochari.
Hakuna matukio yoyote kwa umma yatakayofanyika hadi siku tano baada ya kifo hicho ambapo maelfu kwa maelfu ya waombolezaji watakusanyika katika uwanja wa michezo wa FNB, unaojulikana kama Soccer City ulioko Soweto kwa ajili ya kumbukumbu yake ya kitaifa. Ni katika uwanja huo, ndipo Julai 2010, Mandela alionekana kwa mara mwisho hadharani wakati wa fainali za soka za Kombe la Dunia.
Watazamaji siku hiyo walisimama, wakashangilia huku sauti zao pia zikimezwa na zile za vuvuzela ikiwa ni ishara ya kumpa heshima kiongozi huyo wakati huo akiwa na umri wa miaka 92 ambapo baadhi ya watu walidhani asingeweza kupata nguvu za kujitokeza hadharani.
Siku hii ya tano itaonekana kugubikwa na majonzi makubwa wakati huo Taifa  litakapokuwa likiomboleza kuondoka kwa Madiba.  Baadhi ya viongozi wa kimataifa wanatarajiwa kuhudhuria tukio hilo.
Ofisa wa Ikulu ya Marekani (White House) aliiambia CNN kwamba Utawala unashughulikia mipango ya Rais Barack Obama kwenda Afrika Kusini kuhudhuria tukio hilo muhimu.
Kwa mujibu wa vyanzo, mwili wa Mandela utawekwa katika majengo ya Serikali ya Union jijini Pretoria kwa siku tatu, mahali yaliko makao makuu ya Serikali.  
Siku ya kwanza itakuwa maalumu kwa wageni. Wananchi wengine wataruhusiwa kupita pembeni mwa jeneza lake siku ya saba na ya nane. Saa za kutoa heshima za mwisho zitakuwa mchana tu. Inatarajiwa foleni ndefu kuanza mapema asubuhi.
Ni katika majengo hayo ya kihistoria ambako Mandela aliapishwa kuwa Rais Mei 10, 1994. Siku hiyo adhimu, makundi ya watu yatakusanyika katika majengo hayo kushuhudia historia ikijiandika. Siku hiyo, mfungwa huyo wa zamani wa kisiasa, ambaye hakutarajiwa lakini akaja kuwa kiongozi mweusi wa kwanza baada ya ubaguzi wa rangi kumalizika.
Siku tisa baada ya kifo cha Mandela, ndege ya kijeshi yenye mwili wa Mandela itaondoka katika kituo cha anga cha Pretoria na kwenda Kusini hadi Mthatha, mji mkuu wa jimbo la Eastern Cape. Wazee wa kithembu na familia ya Mandela watafuatana na jeneza lenye mwili wa Mandela.
Maelfu ya waombolezaji wanatarajiwa kujipanga pembeni mwa barabara kutoka uwanja wa ndege Mthatha kushuhudia Jeshi likisafirisha mwili wa Mandela kwenye gari maalumu hadi kijijini Qunu.
Njiani msafara unatarajiwa kusimama kidogo kwa maombi ili kuruhusu watu wa kawaida kutoa heshima zao.
Mwili ukifika nyumbani kwa Mandela, Jeshi litakabidhi majukumu kwa familia yake. Bendera ya Afrika Kusini ambayo itakuwa imefunika jeneza inatarajiwa kuondolewa na kufunikwa blanketi la jadi ya Waxhosa, ikiwa ni ishara ya kurejea nyumbani kwa mmoja wao.
Jioni, viongozi wa ANC, machifu na familia ya Mandela wanatarajiwa watakusanyika kwa ajili ya mkesha wa faragha kabla ya kesho yake kufanyika maziko.
Maziko yatafanyika kwenye viwanja vya nyumbani kwa Mandela. Inatarajiwa maelfu ya watu wakiwamo wakuu wa mataifa mbalimbali duniani, watakusanyika kwa ajili ya maziko hayo ambayo yatafanywa chini ya hema kubwa katika vilima ambako Mandela alikuwa akicheza enzi za utoto wake.
Ulinzi mkali wa kijeshi unatarajiwa kuwapo, kwa lengo la kuondoa hofu ya usalama. Tukio lote litarushwa moja kwa moja kwa mamilioni ya wasikilizaji na watazamaji duniani kote.
Mchana-wakati huu ambao jua la kiangazi linamulika kutoka  angani- Mandela atazikwa katika ardhi hiyo yenye miamba. Eneo la makaburi limejengwa maalumu kwa ajili yake; marehemu wengi wa familia ya Mandela wamezikwa hapo.
Rais Jacob Zuma wa nchi  hiyo alisema kiongozi huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 95, ambaye alirudishwa nyumbani kwa gari la wagonjwa Agosti kumalizia siku zake hapo, “alifariki dunia kwa amani akiwa na familia yake.”
Mke wake wa tatu, Graca Machel (68), alikuwa pembeni, sambamba na baadhi ya wanawe, wajukuu, watoto wa kambo, mchungaji na wazee wa kabila lake la Wathembu.
Binti wa Mandela, Makaziwe Mandela-Amuah na mabinti zake, Tukwini na Ndileka, nao walikuwa na babu yao huyo hadi mwisho wa pumzi yake.
Lakini hakukuwa na dalili zozote za Winnie Madikizela-Mandela, ambaye ni mkewe wa pili aliyemwoa mwaka 1958 na kudumu naye kipindi chote cha miaka 27 aliyokuwa akitumikia kifungo gerezani kabla ndoa yao ya miaka 38 kusambaratika kwa machungu mwaka 1996.
Hali ya kiongozi huyo wa zamani ilianza kudorora tangu Juni, alipolazwa hospitalini akisumbuliwa na maambukizi na hali ilikuwa ya wasiwasi kuwa alikaribia kifo.
Hali yake ilitengemaa hata kuruhusiwa kurudi nyumbani, ambako chumba chake cha kulala kilionekana sawa na chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU).
Mwezi jana, Winnie alisema mumewe huyo wa zamani alishinda tatizo la baridi yabisi lililokuwa likimkabili, lakini alikuwa bado mgonjwa na hakuwa anaweza kuzungumza kwa sababu ya mirija aliyowekwa kwenye mapafu yake ili kutoa maji.
Alisema mumewe huyo wa zamani alikuwa akitumia ishara kuwasiliana na kwamba nyumba alimokuwa ilikuwa ikisafishwa vizuri na kupuliziwa dawa ili kuchelea maambukizi kurejea.
Wiki hii, hali ya Mandela ikabadilika tena na kuwekwa mashine ya kumsaidia kupumua na wakati mwingine alipoteza fahamu.
Jumatano, siku moja kabla baba yake hajafariki dunia, binti mkubwa Makaziwe (60) alisema: “Unaweza kumwona akipambana, lakini roho yuko pamoja naye.”
Na mjukuu wake wa kiume kwa marehemu mwanawe wa kiume, Makgatho Mandela, Ndaba Mandela (30), alisema: “Maendeleo yake hayatii moyo pale kitandani.”
Haijulikani kama Winnie, ambaye aliolewa na kiongozi huyo mwaka 1958 hadi 1996, alikuwapo wakati huo wa mwisho.
Kaka wa Ndaba, Mandla Mandela (39), anaaminika kuwa na babu yake katika saa hizo za mwisho kama ilivyokuwa kwa watoto wa Graca, Josina na Malenga Machel, ambao wana umri wa miaka 30. Mchungaji pia alikuwapo baada ya kuitwa jioni kabla ya kifo.
Naye msaidizi wake, Zelda la Grange (43), anafikiriwa naye alikuwa karibu  na familia wakati hali ya Mandela ikizidi kudorora.
Wakati wa saa za mwisho kabla ya kifo chake saa 2.50 (saa 3.50 saa za Afrika Mashariki) usiku, wazee wa kithembu waliungana na ndugu zake pembeni mwa kitanda.
Juzi asubuhi mwili wa Mandela uliondolewa nyumbani kwake ukiwa kwenye jeneza lililofunikwa bendera ya Taifa la Afrika Kusini na kupelekwa kwenye mochari ya hospitali ya kijeshi jijini Pretoria, kabla ya kuanza siku 10 za maombolezo.

No comments: