Monday, July 14, 2014

NSSF YATISHIA KUIFIKISHA KORTINI KAMPUNI YA ULINZI

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) mkoani hapa, umetoa siku 14 kwa Kampuni ya Ulinzi ya Fodey, iliyopo eneo la Uzungua Manispaa ya Arusha, kulipa deni la michango ya wafanyakazi wake zaidi ya Sh milioni 152 vinginevyo utaifikisha mahakamani.
Akizungumzia tatizo hilo jana mara baada ya wafanyakazi wa kampuni hiyo kufanya vurugu na kufunga geti la kampuni hiyo, Meneja wa Mkoa wa NSSF, Arusha, Jackton Ochieng alisema fedha hizo zinazodaiwa na mfuko huo ni michango ya wafanyakazi tangu mwaka 2009 hadi sasa katika miezi tofauti.
“Sasa tumetoa siku 14 na kama itashindwa kulipa, sisi tutaifikisha kampuni hii mahakamani sababu imekuwa kero kubwa kwa kampuni nyingi za ulinzi kuwasilisha michango kwa kusuasua, jambo ambalo linaleta usumbufu kwa wafanyakazi wao, pindi wanapoachishwa kazi,” alisema.
Pia alitaja waajiri wengine watano wanaodaiwa zaidi ya Sh milioni 500 kuwa ni Bondeni Sekondari, Naasha Junior Academy, Prime Cargo Connection, Mukidoma Sekondari na  Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industry (TPI).
Alisema ni vema wakawasilisha michango ya waajiri wao kwa wakati na kuacha ubabaishaji wa kuwasilisha kwa kuruka baadhi ya miezi, ili kuepukana na usumbufu usio na lazima.
Ochieng alisema NSSF wakati mwingine hawafahamu tatizo hadi wafanyakazi wanapofika ofisini kwao kudai madai yao na wanapofuatilia wanagundua kuwa kampuni husika ina shida. Alisema kampuni nyingi zinaanzishwa na watu wasiojali sheria za nchi.
Naye kiongozi wa wafanyakazi zaidi ya 20 wa Kampuni ya ulinzi ya Fodey, Elisaria Palangyo, akizungumza kwa niaba ya wenzake, alisema kampuni hiyo imejaa ubabaishaji kwani kila mwezi walikuwa wakikatwa zaidi ya Sh 27,000 na wengi wao wamefikia kudai NSSF zaidi ya Sh milioni tatu.

No comments: