Sunday, July 13, 2014

BINTI WA MIAKA 10 ABAKWA NA WANAUME KWA ZAMU

Jeshi la polisi mkoani Ruvuma linawatafuta wakazi wawili wa kijiji cha Silo kata ya Linda wilaya ya Nyasa kwa tuhuma za kumbaka  msichana  wa miaka 10 , mwanafunzi  wa darasa la pili katika shule ya Msingi Luhekitiki  wilayani humo.
Kamanda wa polisi mkoani hapa, Mihayo Msikela alimtaja mtuhumiwa wa kwanza kwa jina moja la Damas ambaye kwa kushirikiana na mwenzake ambaye  hakufahamika walimbaka mwanafunzi huyo nyakati za usiku katika kijiji hicho. 
Tukio hilo lilitokea juzi  usiku ambapo Damas akiwa na mwenzake, walimrubuni mtoto huyo kwa pipi na kumvuta kichakani kabla ya kumbaka.
Alisema mwanafunzi huyo alikuwa katika sherehe za ngoma kijijini hapo.
Alieleza kuwa watuhumiwa  hao baada ya kufanikisha lengo lao hilo  walikimbia na kumuacha mtoto huyo kichakani  akipiga kelele kabla ya kuchukuliwa na wasamaria ambao walitoa taarifa kwa babu yake (jina limehifadhiwa) ambaye naye alitoa taarifa ya tukio hilo polisi.Baada ya polisi kufika kijiji hapo na kumchukua mtoto huyo walimfikisha hospitalini kwa ajili ya uchunguzi na aligundulika kufanyiwa kitendo hicho.

No comments: