Thursday, July 3, 2014

ASILIMIA 30 YA WATAHINIWA NBAA WAFAULU

Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) imesema asilimia 30.2 ya watahiniwa waliofanya mitihani ya Bodi wamefaulu.
Wengine asilimia 40.8 watarudia masomo waliyoshindwa, huku asilimia ambayo hawakufaulu ni 31.7.
Aidha, watahiniwa 478 wamefaulu mtihani wa Shahada ya Juu ya Uhasibu (CPA),  idadi ambayo inafanya watahiniwa waliofaulu  mitihani  hiyo kufikia 5,646 tangu  kuanza kwa mitihani hiyo mwaka 1975.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Uhasibu na Wakaguzi, Mussa Assad alisema hayo jana wakati akizungumzia matokeo ya mitihani ya NBAA, iliyofanyika Mei mwaka huu. Aliongeza kuwa watahiniwa waliofanya mtihani huo, walikuwa 4,395.
“Katika ngazi ya mwisho  watahiniwa 467 kati ya 1,625 waliofanya mtihani huo wamefaulu na wengine 790 watarudia somo moja na watahiniwa 368 hawakufaulu,” alisema Assad.
Alisema  kiwango cha ufaulu kwa taaluma hiyo, kimeendelea kuimarika, tofauti na ilivyokuwa awali ambapo ufaulu ulifikia kati ya asilimia 17 na 18.
Kuhusu uwiano wa waliohitimu kwa jinsi alisema, wanawake waliofanya mtihani   walikuwa asilimia 31.5  na kusisitiza kuwa kwa kawaida wanawake, hufanya vizuri  kazi za uhasibu, tofauti na ilivyo kwa wanaume.

No comments: