Maonesho ya 38 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es
Salaam maarufu kama Maonesho ya Sabasaba yanayotarajiwa kufanyika kwa siku kumi
kuanzia Juni 28, mwaka huu katika Uwanja wa Maonesho wa Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam yanatarajiwa kuongozwa
na kaulimbiu ya `Tunaunganisha Uzalishaji na Masoko’.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa
Bodi ya Maendeleo ya Biashara nchini
(TanTrade), Jacqueline Mneney Maleko, kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutumika
kuonesha uhusiano uliopo kati ya Uzalishaji na Masoko na umuhimu wa
mnyororo wa uzalishaji, ambao ni chimbuko la upatikanaji wa bidhaa zenye
ushindani katika soko.
Alisema kwa mwaka huu, TanTrade imetenga
eneo kubwa zaidi kwa ajili ya wazalishaji wa ndani ya nchi.
Alibainisha kuwa maeneo yatakayotumiwa na
wazalishaji hao kuwa ni Jengo Namba C.19 na eneo la wazi, lililo nyuma ya ofisi
za Mkurugenzi wa Utafiti, Mipango na Uwezeshaji kwa ajili ya bidhaa za kilimo
na bidhaa zinazotengenezwa Tanzania.
Kuhusu ushiriki wa mataifa mengine katika
maonesho hayo, alifafanua kuwa tayari nchi 31 zimethibitisha kushiriki, zikiwemo
Afrika Kusini, Jamhuri ya Czech, China, Ghana, Indonesia, India, Iran, Finland,
Ugiriki, Italia, Japan, Jordan,
Kenya,
Korea Kusini, Malaysia, Marekani, Misri na Ujerumani. Nyingine ni Nigeria,
Pakistan, Rwanda, Saudi Arabia, Singapore, Sudan, Syria, Uganda, Uingereza,
Burundi, Sweden, Vietnam na Zimbabwe.
Jumla ya washiriki waliothibitisha kushiriki kutoka ndani ya nchi ni
1,700.

No comments:
Post a Comment