Katika kukabiliana na tatizo la ufinyu
wa bajeti katika Jeshi la Magereza na kuipunguzia mzigo Serikali, jeshi hilo
linakusudia kuanza kuchimba madini ili lijitegemee, baada ya utafiti wa jeshi
hilo kubaini baadhi ya maeneo inayoyamiliki yanaweza kuwa na aina mbalimbali za
madini.
Tayari jeshi hilo limeshapata leseni
102 za uchimbaji wa madini ya aina mbalimbali nchini ili liweze kupata fedha za
kujiendesha.
Hayo yalisemwa jana na Kamishna
Jenerali wa Magereza nchini, John Minja katika hotuba yake aliyoisoma mbele ya
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe wakati wa Maadhimisho ya Siku
ya Magereza nchini yaliyohudhuriwa pia na wakuu wa vyombo vya ulinzi na
wastaafu wengine wa jeshi hilo.
Alisema jeshi lake linakabiliwa na
changamoto mbalimbali zikiwamo ufinyu wa bajeti, miundombinu ya magereza, uhaba
na uchakavu wa vyombo vya usafiri na mawasiliano, vitendea kazi, ukosefu wa
pembejeo pamoja na msongamano magerezani.
“Katika kukabiliana na changamoto ya
ufinyu wa bajeti, Jeshi la Magereza limefanya jitihada mbalimbali ili kuongeza
tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu, tumefanyia utafiti maeneo yetu
na tayari tumekwisha pata leseni 102 za uchimbaji madini, sasa tunatafuta
wawekezaji,” alisema Kamishna Minja.
Alisema leseni hizo ni za uchimbaji wa
madini ya ujenzi kama chokaa, mawe, kokoto, mchanga na moram katika maeneo
mbalimbali ya Magereza nchini. Aliongeza kuwa, jeshi hilo linaendelea kuomba
leseni nyingine katika maeneo yanayoonekana kuwa na madini.
Mbali na hilo Kamishna Minja alisema
Magereza imeingia pia ubia na Mfuko wa Pensheni wa Akiba ya Wafanyakazi (GEPF)
kwa ajili ya uwekezaji wa miradi mbalimbali kwa ubia katika maeneo ya Magereza
ikiwa ni pamoja na ujenzi wa majumba makubwa ya biashara (Mall).
Alisema katika kukabiliana na tatizo
la makazi ya watumishi, Jeshi linafanya jitihada za kuhamasisha ujenzi wa
nyumba za kujitolea kwa kutumia rasilimali zinazopatikana katika maeneo husika.
“Jitihada hizi zimeonesha mafanikio
makubwa kwani hadi sasa nyumba nyingi za kujitolea zimejengwa na kukamilika na
nyingine ziko katika hatua mbalimbali za ujenzi na pia tunaendelea na ukarabati
wa nyumba za zamani,” alisema Kamishna Minja.
Aidha alisema wamefungua kiwanda cha
ushonaji katika Gereza la Butimba mkoani Mwanza kwa lengo la kupunguza wingi wa
kazi za ushonaji uliokuwepo kiwanda cha Ukonga ambapo ni fursa nzuri kwa
wafungwa pia kujifunza shughuli za ushonaji kama sehemu ya urekebishaji.
Alisema kiwanda kingine kimefunguliwa
Ruanda, Mbeya na kiwanda cha samani kiko mbioni kukamilika katika Gereza la
Lilungu mkoani Mtwara.
Alisema Jeshi hilo katika kuhakikisha
wanaimarisha uzalishaji wa mazao ya kilimo, wameingia ubia na baadhi ya kampuni
za ndani na nje ili kushirikiana katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji.
“Hii ni jitihada za kulifanya Jeshi la
Magereza linakuwa la kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake na pia
kushukuru taasisi zisizo za kiserikali kuona maeneo ya shughuli mbalimbali
tushirikiane, kutushauri na mapendekezo ili kuboresha utendaji kazi,” alisema
Kamishna Minja.
Awali Waziri Chikawe alifungua duka la
bidhaa zisizotozwa ushuru katika Magereza ya Keko jijini Dar es Salaam ambapo
Kamishna Minja alisema duka hilo ni moja kati ya maduka kadhaa yaliyopo mikoa
mbalimbali na kwamba Jeshi la Magereza kwa kushirikiana na wabia wengine
wataendelea kufungua maduka mengine.
No comments:
Post a Comment