Thursday, June 19, 2014

BENKI YA DUNIA YATOA SHILINGI BILIONI 74 KUBORESHA MAJI



Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya Dunia, imeidhinisha msaada kwa Tanzania zaidi ya Sh bilioni 74 kusaidia upatikanaji wa huduma ya maji safi, salama na maji taka kwa familia masikini za mijini na vijijini.
Fedha hizo sawa na Dola za Marekani milioni 44.9 ziliidhinishwa  kama mkopo  ikiwa ni fedha za ziada za kuboresha Mradi wa Kusaidia Sekta ya Maji (WSSP). 
Mradi wa WSSP uliidhinishwa na Bodi mwaka 2007, na umechangia awamu ya kwanza ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Tanzania (WSDP) wa miaka 20 kuanzia mwaka 2006 hadi 2025. 
Mradi huo unaendeshwa na Serikali, wadau wa maendeleo na wadau wengine na tayari umekuwa na matokeo chanya, kama vile ukamilishwaji wa miradi ya maji katika vijiji 918. 
Miradi mingine ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa vituo vya maji 26,468 inayolenga kunufaisha wananchi milioni 6.7 wa vijijini, kusaidia upatikanaji wa huduma ya maji kwa wakazi milioni 2.8 wa mijini na kusaidia serikali za mitaa kwa ajili ya kuboresha mfumo wa maji taka kwa kaya 180,000.
"WSSP inatoa fursa sawa ya huduma ya maji safi na maji taka, ambayo ni mambo muhimu kwa afya bora na kuboresha maisha ya jamii masikini za mijini na vijijini nchini Tanzania," alisema Mkurugenzi Mwakilishi wa Benki ya Dunia Tanzania Philippe Dongier kupitia taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari.
Chini ya mradi huo wa WSSP, uboreshaji wa  huduma ya maji  utahusu ujenzi wa  vituo vya maji katika vijiji 628 ukilenga kunufaisha watu 234,624. 
"Kwa kuleta huduma za maji kwa jamii masikini katika vijiji na maeneo ya mijini, WSDP itawezesha wasichana na wanawake kutumia muda kidogo kuchota maji kwa ajili ya familia zao na muda mwingi kwenye elimu na shughuli za kiuchumi," alisema kiongozi wa mradi kutoka Benki ya Dunia, Yitbarek Tessema.
Hivi karibuni, Bunge lilidhinisha Sh 520,906,475,000 kwa ajili ya Wizara ya Maji, na asilimia 94 ya fedha hizo zitatumika kwenye miradi ya maendeleo zikiwamo Sh bilioni saba zilizotengwa kwa ajili ya kulipa fidia wananchi ili kupisha mradi wa Bwawa la Kidunda litakalotumiwa kukabili adha ya maji jijini Dar es Salaam.

No comments: