TAARIFA YA MKAGUZI MKUU YAMNG'OA MADARAKANI MEYA WA BUKOBA...


Dk Anatory Amani.

Meya wa Manispaa ya Bukoba, Dk Anatory Amani amejiuzulu wadhifa huo baada ya kuguswa na taarifa ya ukaguzi uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Amefanya hatua hiyo baada ya kushauriwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyemtaka apime mwenyewe ama kwa kujiuzulu au asubiri kupigiwa kura na Baraza la Madiwani za kutokuwa na imani naye.
Taarifa ya ukaguzi wa CAG uliofanyika kwa siku 35, ilitolewa ikionesha tuhuma zaidi ya 30 zilimgusa Meya huyo na baadhi ya watendaji wa Manispaa hiyo akiwemo aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Hamisi Kaputa.
“Nimeafiki na kukubali maamuzi na maelekezo yaliyotolewa na Serikali mimi ni mtu mzima nimejiuzulu,” alitamka amani kwa ufupi.
Taarifa ya ushauri kutoka kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ilitolewa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Serikali za Mitaa Tawala za Mikoa (TAMISEMI), Aggrey Mwanri wakati wa kikao kilichofanyika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, mjini hapa.
Alisema baada ya kuonekana kuna tuhuma za makosa mengi ya kiutendaji ikiwemo  matumizi mabaya ya fedha ya umma, kusaini mikataba kinyume bila kuwashirikisha baraza la madiwani na kuikosesha mapato Manispaa, Serikali imeamua kutoa maagizo ya kumtaka `ajipime’.
Aidha, Mwanri alisema Waziri Mkuu ameagiza Kiputa ambaye kwa sasa ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Momba mkoani Mbeya, avuliwe madaraka mara moja.
Alisema wengine wanaopaswa kuvuliwa madaraka mara moja ni Mhandisi wa Manispaa ya Bukoba, Steven Nzihirwa, Ofisa Manunuzi wa Manispaa, Baraka Marwa na Mweka Hazina wa Manispaa, Hamduni Ulomi ambaye kwa sasa inadaiwa yuko masomoni nje ya mkoa wa Kagera.
Pia imeagizwa kuwa, kitengo cha ukaguzi wa ndani katika Halmashauri hiyo kiimarishwe ili kiweze kufanya kazi ipasavyo na  pia itaundwa kamati ambayo itashirikiana na Serikali za mitaa kufanya wa ukaguzi wa mambo mengine ambayo yamebainika kuhitaji ukaguzi zaidi kikiwemo uuzwaji wa kiwanja cha michezo  cha shule ya msingi Kiteyagwa.
Maagizo yote hayo yametakiwa kutekelezwa ndani ya wiki moja na taarifa yake kufika Ofisi ya Waziri Mkuu.
Baadhi ya miradi iliyoibua utata na hata kusababisha ukaguzi wa CAG na hatimaye kumng’oa meya ni ujenzi wa kituo cha mabasi Kyakailabwa, mradi wa viwanja 5000 na viwanja 800, mradiwa ujenzi wa kituo cha kuoshea magari cha machinjioni. Aidha, Meya anatuhumiwa kusaini mkopo wa Sh mil. 200 bila kufuata utaratibu na kutofuata taratibu wa kuwapata wakandarasi na kuutowashirikisha madiwani wa manispaa hiyo.

No comments: