MBATIA ATETEA KITI CHAKE NCCR-MAGEUZI KWA KISHINDO...

James Mbatia.
Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ametetea nafasi yake na kuibuka mshindi katika uchaguzi wa ndani wa chama hicho kwa kumbwaga mpinzani wake Charles Makofila kwa kura 201 kati ya kura 228.

Akizungumza na mwandishi, Dar es Salaam jana Msimamizi wa Uchaguzi huo na Mbunge wa Kasulu Mjini,  Moses Machali alisema katika mkutano mkuu uliofanyika juzi, Mbatia aliibuka mshindi kwa kupata kura hizo 201 wakati Makofila alipata kura 26 huku kura moja ikiharibika.
Aidha, alisema katika mkutano huo, katika uchaguzi wa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho upande wa Zanzibar, Haji Ambari Hamis alitetea nafasi yake kwa kupata kura 201 kati ya kura 228 zilizopigwa huku kura 22 zikiharibika.
"Katika nafasi hii, Hamis aligombea mwenyewe hakuwa na mpinzani alishinda lakini pia kura tano zilipigwa zikisema hapana," alisema Machali.
Alisema katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti upande wa Bara, aliyeshinda nafasi hiyo ni Leticia Musore, aliyepata kura 192 kati ya 228, hivyo kuwabwaga wapinzani wake, Anyimike Mwasakalali na Rukia Abubakari. 
Machali pia alisema katika mkutano huo, walichaguliwa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama hicho, ambao ni wajumbe 10 watano wanawake Zanzibar na watano bara, wajumbe watatu kutoka makundi maalum na wajumbe 4 kutoka kundi la vijana.
Alisema pia wajumbe wengine waliochaguliwa ni wajumbe 10 wanaume watano kutoka bara na watano kutoka Zanzibar ambapo jumla wa wajumbe wote ni 28.
Aidha, jana ulifanyika mkutano wa NECkwa ajili ya kuchagua Katibu Mkuu, ambapo wagombea ni Katibu Mkuu wa sasa, Samuel Ruhuza anayepambana na Mosena Nyambabe.
Wagombea wengine katika uchaguzi wao uliofanyika jana ni wa nafasi ya Naibu Katibu Mkuu, ambapo wagombea ni Faustine Sungura na Machali na pia uchaguzi wa Baraza la Wadhamini.

No comments: