KESI YA WALIONASWA NA KONTENA LENYE MENO YA TEMBO JANUARI 16...

Polisi wakikagua kontena hilo mara baada ya kukamatwa Zanzibar hivi karibuni.
Upelelezi wa kesi ya kukutwa na meno ya tembo yenye thamani ya Sh bilioni 7.5 inayowakabili watu sita waliokamatwa Zanzibar, bado haujakamilika.

Wakili wa Serikali Flora Massawe alidai hayo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakati kesi hiyo ilipotajwa.
Hakimu Mkazi Nyigulila Mwaseba aliahirisha kesi hiyo hadi Januari 16 mwakani, itakapotajwa  tena na washitakiwa wataendelea kukaa rumande.
Washitakiwa hao ni Mohamed Mussa, Mohamed Haji, Juma Makame, Mohamed Mashaka, Omary Ally na Haider Abdallah. Wameshitakiwa chini ya Sheria ya Uhujumu Uchumi na Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori.
Ilidaiwa kuwa kati ya Oktoba mosi na Novemba 13 mwaka huu katika maeneo mbalimbali Kinondoni jijini Dar es Salaam na Mjini Magharibi Zanzibar, washitakiwa walipanga njama za kutenda kosa hilo.
Aidha, ilidaiwa siku hiyo hiyo katika Bandari ya Zanzibar, washitakiwa hao walikamatwa na kontena lenye nyara za Serikali, ambazo ni vipande 1,023 vya meno ya tembo yenye kilo 2,915 na thamani ya Sh bilioni 7.5 bila kuwa na kibali cha kumiliki kutoka mamlaka husika.
Hata hivyo, hawakuruhusiwa kujibu mashitaka na kunyimwa dhamana kwa kuwa Mahakama hiyo haina mamlaka kisheria kusikiliza kesi hiyo isipokuwa Mahakama Kuu.

No comments: