UTAFITI: VINYWAJI VYA KUONGEZA NGUVU MWILINI NI HATARI KWA AFYA...

Vinywaji baridi vyenye lengo la kuongeza nguvu vinadaiwa kuwa hatari kwa afya ya watumiaji baada ya kubaini baadhi ya kemikali husababisha madhara mwilini.

Watumiaji wa vinywaji hivyo wamehadharishwa ikielekezwa utafiti mbalimbali uliofanyika kwa miaka 10, inaonesha athari za matumizi ya vinywaji hivyo.
Katika mitandao ya Yahoo na The Dailymeal, iliwekwa orodha ya vinywaji vinavyodaiwa kuwa na kemikali hatari, miongoni mwake ikiwamo Red Bull na Monster, vinavyotumika kwa wingi nchini. Vingine vilivyo katika orodha hiyo ni VPX Redline,  DynaPep na  Rockstar Cocaine.
Akizungumza na mwandishi jana, Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA), Gaudensia Simwanza  alitaja kinywaji cha Red Bull ambacho kimetajwa kuwa miongoni mwa vinywaji hatari kuwa ni salama kwa matumizi ya binadamu.
Hata hivyo, alisema vinywaji vingi vyenye kemikali vikiwamo vya aina hiyo vinaweza kuwa na madhara endapo vitanywewa kwa kiwango kikubwa.
Alisema vinywaji vingi vina athari ikiwa vitanywewa bila mpangilio. Aliongeza kuwa vipo vinywaji ambavyo lazima vifikie viwango vya mataifa ndipo viruhusiwe kuingia sokoni.
Simwanza  alikuwa akizungumza na mwandishi aliyemhoji kuhusu hatari ya vinywaji hivyo na iwapo zipo hatua zilichukuliwa za kuangalia athari zake kwa watumiaji.
Alisema endapo upo utafiti uliofanywa kuona si salama, ni vema watafiti hao wakashirikisha mamlaka hiyo ili kubaini ukweli.
"TFDA imesajili Red Bull baada ya kujiridhisha kuwa ni salama kwa matumizi ya binadamu, endapo wametafiti na kuona si salama, watushirikishe na sisi katika utafiti waliofanya ili tufanyie kazi na kuchukua hatua," alisema.
Akielezea suala zima la usalama, alisema wakati mwingine huenda soko likawa limevamiwa  na watu wasio waaminifu ambao wanazalisha vinywaji hivyo vikiwa na madhara kwa watumiaji.
Alisema Mamlaka huwa inafanya utafiti wa bidhaa katika masoko mara kwa mara, ikiwa ni pamoja na ukaguzi kwa lengo la kujiridhisha ubora na usalama wake. “Ikitokea kuna taarifa zenye shaka kuhusu bidhaa huwa tunafuatilia na kuzifanyia kazi," alisema.
Hata hivyo, taarifa hiyo ya kwenye mtandao, imepokewa kwa hisia tofauti wakiwamo wanaotetea vinywaji hivyo na kuchukulia kuwa propaganda za kibiashara.
Kulingana na utafiti, inadaiwa vinywaji hivyo vya kusisimua mwili, zimo kemikali zinazosababisha magonjwa ya moyo na kukosesha usingizi.
Aidha, inaelezwa kuwa vinywaji hivyo vyenye mchanganyiko wa kemikali za L-phenylalanine, inositol na citicoline  si salama hasa vinaponywewa kwa wingi.
Kwa upande wa Red Bull, inatajwa kujaa kemikali za kusisimua mwili na nyingine kusababisha meno kuoza kutokana na wingi wa sukari iliyomo.
Kinywaji cha Monster kimeshawahi kuchunguzwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Marekani (FDA)  kutokana na kuonekana kuleta madhara  makubwa kwa watumiaji.  Inadaiwa  kusababisha matatizo ya usingizi.
Kinywaji kingine kilichoko kwenye orodha ni VPX Redline ambayo imetengenezwa kupunguza hali ya kutetemeka, inadaiwa kuleta mwako katika mafuta. Inatakiwa inywewe kidogo mhusika akiwa amekula.
Aidha, DynaPep ina kemikali aina ya methylhexanamine; kisisimua mwili ambacho wengine wanasema  kinapoteza mwelekeo wa mtu na wakati mwingine huongeza kasi ya mapigo ya moyo.
Rockstar ina gramu 62 za sukari na 280 za nishati. Full-Throttle, inatajwa kwamba unywaji wake wa kupitiliza unaweza kuleta maumivu ya tumbo, upotevu wa kumbukumbu na ongezeko la mapigo ya moyo.
Cocaine inadaiwa kuwa na kemikali inayosisimua mara tatu zaidi ya Red Bull. Pia husababisha hatari ya magonjwa ya moyo.

No comments: