Friday, November 8, 2013

BOSI WA ZAMANI TBS APANDISHWA KIZIMBANI KWA UBADHIRIFU...

Charles Ekelege.
Aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango nchini (TBS), Charles Ekelege, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka mawili.

Ekelege anayekabiliwa na mashitaka ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia TBS hasara, alifikishwa mahakamani hapo juzi na kusomewa mashitaka  mbele ya Hakimu Mkazi Agustina Mmbando.
Katika kosa la kwanza ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Janeth Machuya, Machi 28, mwaka 2008 na Agosti 7, mwaka 2009 katika ofisi za TBS jijini Dar es Salaam, akiwa Mkurugenzi Mkuu alitumia madaraka vibaya na kwa nia ovu alizipunguzia ada kampuni mbili kwa asilimia 50.
Kampuni hizo ni Jaffar Muhamed Ali Garage na Quality Motors ambapo asilimia hizo ni sawa na Sh 68,068,800 bila idhini ya Bodi, jambo ambalo limedaiwa kuwa  kinyume na taratibu za TBS .
Katika mashitaka ya pili, Ekelege anadaiwa kuisababishia TBS hasara ya kiasi hicho cha fedha.
Alikana mashitaka na yupo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti. Alitakiwa kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika waliotakiwa kusaini hati ya dhamana ya Sh milioni 35.
Machuya alidai upelelezi wa kesi hiyo umekamilika, na kuomba tarehe kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali. Hakimu Mmbando aliahirisha kesi hiyo mpaka Desemba 12, mwaka huu.

No comments: