Thursday, October 24, 2013

MGAWANYO WA HALMASHAURI WAIBUA MGOGORO RUKWA...

Moshi Chang'a.
Mgawanyo wa halmashauri ya Sumbawanga wenye lengo la kufikisha huduma za Serikali karibu na wananchi, umeibua mgogoro baada ya halmashauri mpya ya wilaya ya Kalambo, kudai kuhujumiwa na halmashauri mama.

Mkuu  wa  Wilaya  ya Kalambo  mkoani  Rukwa, Moshi Chang’a,  ameng’aka  na kudai  kuwa halmashauri mpya ya wilaya ya Kalambo imehujumiwa katika ugawaji  wa  mali, madeni na rasilimali watu na kuelezea msimamo kuwa ni kutaka mgawo  huo  ufanyike  upya.
Chang’a  alitoa  lawama  hizo wakati akifungua kikao cha Baraza la Madiwani  wa halmashauri  hiyo, kilichofanyika  juzi  mjini Matai, yalipo makao  makuu  ya wilaya  hiyo.
“Wala sitaona  aibu  kusema  haya  ukweli  ni kwamba halmashauri  hii  mpya ya  wilaya  ya Kalambo  tumepigwa bao…hatukupewa  chochote katika mgawo  wa rasilimali baada ya halmashauri mama  ya wilaya  ya Sumbawanga kugawanywa na kuzaliwa  hii  yetu.
“Sasa badala  ya ujio  wa halmashauri  hii mpya kuwa baraka,  umegeuka kuwa  adhabu  tena ni sawa sasa na jehenamu  kwani  fedha zote za utekelezaji  wa  miradi  ya maendeleo  ya  halmashauri  hii  zimebakia  katika halmashauri  ya wilaya  ya Sumbawanga,“  alisisitiza Chang’a.
Changamoto nyingine aliyosema Chang’a ni miradi ya maendeleo katika halmashauri  hiyo mpya ya Kalambo ambayo imebainika  kutekelezwa chini  ya  kiwango,  ambayo alidai kuwa  mikataba  yake  ilisainiwa  kabla  ya kugawanywa kwa halmashauri  mama na kuzaliwa kwa halmashauri hiyo mpya ya Kalambo.
“Hata  mamilioni  ya  fedha  za  usimamizi  wa  miradi  ya  maendeleo  ya halmashauri  hii  mpya ya  wilaya ya Kalambo,  yapo  katika  halmashauri ya  wilaya ya Sumbawanga.
“Tunaomba  yasiendelee  kutunzwa huko kwani  kuna taarifa  zimeanza  kuliwa na  wajanja  kwa  kuhonga  wanawake  mjini Sumbawanga,“ alidai Chang’a.
Alisema hata waraka unaoonesha mgawo  wa rasilimali hizo halmashauri  ya Kalambo haijapatiwa  kwa maelekezo kuwa haupo.
Aliwaeleza madiwani  hao  kuwa  Ofisi  ya Mkuu  wa Mkoa  umeshataarifiwa  juu ya kadhia  hiyo, sasa kinachofuata  ni  Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kutaarifiwa  juu  ya  kero  hiyo ili ipatiwe ufumbuzi wa haraka.
Wakati  huo huo,  madiwani  wa halmashauri  hiyo  ya Kalambo walimchagua  diwani wa kata  ya Msanzi, Faustine Mwanisenga (CCM)  kuwa Makamu  Mwenyekiti  wa halmashauri hiyo akiwa mgombea  pekee baada ya  Chadema  kuamua kukwepa kuweka mgombea.
 Uchaguzi  huo ulifanyika kutokana na kufariki  dunia  kwa  aliyekuwa Makamu  Mwenyekiti wa halmashauri  hiyo,  Henry Kacheche, Septemba 13, mwaka  huu.

No comments: