BIBI HARUSI MTOTO WA MIAKA MINANE AFARIKI KWA KUVUJA DAMU NDANI YA MWILI...

Moja ya sherehe za ndoa za utotoni nchini Yemen.
Bibi harusi mtoto mwenye miaka minane amekufa nchini Yemen kutokana na kutokwa damu ndani kwa ndani wakati wa usiku wa harusi yake baada ya kuwa amelazimishwa kuolewa na mwanaume aliyemzidi umri mara tano, wanaharakati wamedai.

Binti huyo, aliyetambuliwa tu kama Rawan, alifariki kwenye eneo la kikabila la Hardh huko kaskazini-magharibi mwa Yemen, mpakani na Saudi Arabia.
Wanaharakati sasa wanataka mume huyo, ambaye anaaminika kuwa na takribani miaka 40, na familia ya binti huyo kukamatwa ili waweze kukabiliana na mkono wa sheria kwenye mahakama.
Wanasema kukamatwa kutasaidia kukomesha mazoea hayo ya kuozesha wasichana wadogo kwa wanaume watu wazima katika eneo hilo fukara.
Mwanablogu mmoja alituma ujumbe akisema: "mwanaume huyo ni mnyama anayestahili kuadhibiwa vibaya mno kwa makosa yake."
"Wote waliosaidia kosa hilo wanatakiwa pia kuadhibiwa," aliongeza.
Mwanablogu mwingine aliandika: "Familia ya Rawan sio binadamu. Hawastahili kuwa na watoto."
Mwingine alisema: "Familia yake na mumewe walitakiwa kusubiri kwa kipindi fulani kabla ya kufunga ndoa hii."
"Haikuwa haki kabisa na ndoa haikustahili kufungwa hata kama baadhi ya makabila wanaamini kwamba ni mila nzuri."
Zoezi la kuoa wasichana wadogo limetapakaa nchini Yemen na limeibua mvuto mkubwa wa makundi ya kimataifa ya haki yakitaka kushinikiza serikali hiyo kukomesha ndoa za watoto.
Zaidi ya robo ya wanawake wa Yemen wanaolewa kabla ya umri wa miaka 15, kwa mujibu wa ripoti ya mwaka 2010 iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Jamii.
Mila za kikabila pia zinachangia, ikiwamo imani kwamba bibi harusi mdogo anaweza kufanywa kuwa mke mtiifu, kuzaa watoto wengi na kuwekwa mbali na vishawishi.
Septemba mwaka 2010, bibi harusi wa Yemen mwenye miaka 12 alifariki baada ya kuteseka kwa siku tatu chumba cha uzazi kujifungua mtoto, taasisi moja ya haki za binadamu nchini humo ilisema.
Yemeni iliweka umri wa chini wa kuolewa miaka 15, lakini bunge likabatilisha sheria hiyo katika miaka ya 1990, likisema wazazi wanatakiwa kuamua lini binti zao waolewe.

No comments: