![]() |
Bweni la wanafunzi wa Shule ya Sekondari Bomalang'ombe iliyoko wilayani Kilolo, mkoa wa Iringa. Ukosefu wa mabweni madhubuti kumekuwa kukichangia vitendo vya kubakwa kwa wanafunzi wa kike. |
Wanafunzi wa kike katika shule ya sekondari Mzindakaya kijijini Kaengesa, wameelezea vitendo hatari wanavyokabiliwa navyo vya kubakwa na kudhalilishwa kijinsia mara kwa mara, kutokana na kukosa uwezo wa kuishi katika mabweni kwa usalama.
Wakizungumza na mwandishi katika mahojiano maalumu mwishoni mwa wiki, wanafunzi hao wamedai kuwa wamekuwa wakiona aibu kuripoti visa vya ubakaji wanavyofanyiwa, kwa uongozi wa shule na kwa wazazi wao.
“Wengi wetu hatujui hatima yetu kwani tunaishi kwa hofu kubwa hususani usiku, tunakosa raha licha ya kwamba kila mmoja wetu amepanga chumba.
“Kutokana na visa vya kubakwa mara kwa mara, tumeamua kulala chumba kimoja wasichana kati ya watatu hadi sita,” alisema mmoja wao.
Kwa mujibu wa mwanafunzi huyo, wamekuwa wakiogopa na kuona aibu kutoa taarifa kwa mamlaka husika, na kubakia kukaa kimya na kujiuguza kwa siri na hata wakipiga kelele, huwa hawapati msaada.
“Tukipiga kelele, hakuna msaada mpaka kukicha ndipo majirani wanapokuja kutupa pole huku wakidai kuwa licha ya kusikia tukipiga mayowe ya kuomba msaada, wanashindwa kutoka nje kwa hofu ya kushambuliwa na watu hao wasiojulikana,“ alisema mmoja wa wanafunzi hao kwa masikitiko.
Akizungumza na mwandishi shuleni hapo hivi karibuni, Makamu Mkuu wa shule hiyo, Agatha Okumu, alikiri kuzungumza na wanafunzi wa kike wanaoishi katika nyumba za kupanga kijijini, wakamweleza kuwa kumekuwa na visa vingi vya kubakwa.
“Nyumba walizopanga hazifai kuishi, hazina usalama kutokana na milango ya vyumba kuwa mibovu na usiku wanalazimika kuegesha vinu kuzuia isifunguke.
“Sasa imekuwa rahisi kwa ‘wabakaji‘ kusukuma tu milango hiyo na kuingia ndani na kuwaingilia kimwili na kutokomea kusikojulikana,“ alisema.
Alisema visa vya kubakwa wanafunzi hao wa kike ni vingi, lakini vitatu tu ndio vimeripotiwa hadi sasa ambapo kisa cha kwanza kiliripotiwa baada ya wanafunzi watatu kubakwa, na mtuhumiwa alisakwa na kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya dola.
Kwa mujibu wa Mwalimu Okumu, visa vingine ni pamoja na mwanafunzi wa kidato cha nne shuleni hapo, aliyejiua kwa kunywa sumu ya panya, baada ya kubakwa yeye na mwenzake mwingine.
Mtu aliyewafanyia hivyo, kwa maelezo ya Mwalimu Okumu, alivamia chumbani mwao walimokuwa wakiishi watatu na kuwatishia kuwaua iwapo wangepiga kelele.
“Juzi tu wanafunzi sita waliokuwa wakiishi chumba kimoja wamenusurika kubakwa na watu wawili waliowavamia usiku wakiwa wamelala chumbani mwao.
“Hata hivyo walishindwa kuwafanyia vitendo vya udhalilishaji baada ya kukuta ni wengi na walianza kupiga mayowe, wakaishia kuwapora Sh 1,100 walizokuwa nazo, wakawapiga kwa marungu na kutokomea kusikojulikana,“ alisema Mwalimu Okumu.
Mkuu wa shule hiyo, Nicholas Thomas amewatupia lawama majirani wanaoishi karibu na nyumba walizopanga wanafunzi hao, kwa kutowapatia msaada wowote licha ya wao kupiga mayowe ya kuomba msaada.
Mwalimu Thomas aliwataka wazazi kuchangia gharama za watoto wao kuishi katika mabweni shuleni hapo, ambapo kwa mtoto mmoja kwa muhula, mzazi anatakiwa kuchangia magunia mawili ya mahindi, debe moja la maharage na Sh 40,000 za ujira wa mpishi.
Umasikini wa wazazi wao, umedaiwa kusababisha wanafunzi hao kushindwa kulipia gharama za kuishi katika mabweni ya shule hiyo, na kwa kuwa wanahitaji elimu, wakalazimika kupanga nyumba mbovu, ambazo ndizo hufanyiwa vitendo hivyo.
Mwandishi alipotembelea baadhi ya nyumba walizopanga wanafunzi hao na kushuhudia zikiwa katika hali mbaya, kwani hazina vyoo na wala hazijazungushiwa uzio kwa ajili ya usalama wao.
“Kama unavyoona choo kilichopo ni kibovu, hakina hata mlango na kiko nje meta kadhaa kutoka katika nyumba hii. Kutokana na hofu ya kutoka nje kujisaidia wakati wa usiku, tunalazimika kujisaidia kwenye makopo tunayohifadhi vyumbani kisha asubuhi tunaenda kumwaga uchafu huo chooni,” alisema.
Uchunguzi wa mwandishi umebaini kuwa kodi ya pango ya vyumba hivyo ni Sh 1,000 kwa mwezi.
No comments:
Post a Comment