MKE ADUNDWA NA KUTIMULIWA KWA KUASI KANISA ANALOSALI MUMEWE...

Biblia Takatifu.
Bila  yeye mwenyewe  kutarajia,  mke wa  ndoa  amejikuta  akicharazwa bakora na kutimuliwa  nyumbani  na  mumewe baada ya  mama  huyo kuacha kuabudu katika  madhehebu  ya Katoliki  alikofunga  ndoa  na mumewe  aitwaye Martin Kikondo (50) na kuamua kubatizwa  na kuanza kusali  katika  Kanisa  la Assemblies (EAGT).

Mama  huyo  aitwaye  Redempta Saulo (38)  mkazi  wa kijiji  cha Kasokola wilayani  Mlele, mkoani  Katavi  alikumbwa  na   dhahama  hiyo  hivi karibuni  baada  ya  yeye  na  watoto  wake  watatu  'kuasi’  Kanisa Katoliki  na kuanza  kusali   katika  kanisa   hilo  la  EAGT bila  idhini ya  mumewe huyo.
Mwenyekiti wa  Kijiji hicho cha Kasolola, Dominico Fungameza akisimulia  mkasa huo alieleza kuwa wanandoa hao  walitengana hivi  karibuni   mwanzoni mwa wiki iliyopita  baada ya Martin kubaini  kuwa  mkewe na watoto wake watatu wamebadili madhehebu  bila kumshirikisha.
Alisema  mume  huyo baada ya  kugundua kuwa mkewe amebadili dhehebu  lake  la awali  pamoja na watoto wake bila ridhaa yake alihamaki  na  kuanza  kumpiga mkewe  huyo  ambaye  alikimbilia Kituo  cha Polisi ili kujisalimisha na baadaye alikimbizwa  katika  Hospitali  ya Wilaya  mjini  hapa kwa matibabu.
“Hata  hivyo  Polisi  waliwashauri  wanandoa  hao  wamalize  mgogoro wao  kifamilia …  lakini  ushauri  huo  ulipingwa  na  viongozi  wa  kiroho  wa kanisa hilo  la EAGT,” alisema  Fungameza.
Kwa mujibu  wa Mwenyekiti  huyo, Mchungaji  wa kanisa hilo aliyemtaja  kama  Jacob  Mizengo  alilazimika  kumfuata  Martin nyumbani kwake ambako alihoji  kulikoni  amechukua uamuzi  wa kumpiga mkewe  kisa  amejiunga na kanisa  la EAGT.
Inadaiwa ndipo  Martin na  mchungaji  huyo  kuanza  kutupiana  maneno  ya kutishiana  na kusababisha  zogo lililofanya  majirani kusogea  nyumbani hapo  ili kujua kilichokuwa kikiendelea  akiwemo  mwenyekiti  wa kijiji hicho  katika  jitihada za kuwasuluhisha.
Ndipo  majirani hao waliokusanyika  nyumbani  kwa  wanandoa  hao  waliamua kifanyike  kikao cha usuluhishi  kilichowahusisha baadhi ya wazee  na wanandugu wa pande hizo mbili  za mwanandoa hao kilichoongozwa  na  Mwenyekiti  wa kijiji  hicho, Fungameza.
Hata hivyo wakati kikao hicho  kikiendelea  ndipo  Martin  aliingia ndani ya nyumba yake na kisha alitoka akiwa  ameshikilia  picha ambazo alizionesha  mbele  ya  wajumbe  wa  kikao hicho  jinsi  mkewe na watoto wake walivyo kuwa wakibatizwa  na Mchungaji Mizengo,  ubatizo ambao  uliofanyika  mtoni  kijijini  Kasokola.
Inadaiwa  kuwa  baada ya kuwaonesha picha hizo mbele ya  wajumbe  wa kikao hicho   wakiwemo  ndugu zake , Martin  aliwaeeleza  kuwa yeye hayuko  tayari  tena kuendelea kuishi na  mkewe  huyo kwa  kuwa amebadili dhehebu hivyo hataki kumwona nyumbani kwake tena.
Kufuatia  msimamo huo  wa Martin  mbele  ya kikao  hicho   kwa  kuhofia usalama wa wanandoa hao kikao hicho  kiliridhia kuwa  mke wa Martin  aende  akaishi nyumbani kwa wazazi wake kijijini  humo mpaka hapo watakapo suluhishwa  na ndugu  zao  wa pande  hizo  mbili.

No comments: