MAPIGANO YA WAKULIMA NA WAFUGAJI YAIBUKA SAME



Kumezuka mapigano baina ya wafugaji na wakulima katika kijiji cha Jiungeni Lolokai, kata ya Ruvu wilayani Same na tayari wakulima wanne wamejeruhiwa vibaya na silaha za jadi, na mmoja kukimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC kwa matibabu zaidi.
Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba askari wake wamepelekwa eneo la tukio kudhibiti vurugu.
Awali, Diwani wa Kata ya Hedaru, Gerald Mgwena jana alikieleza kikao cha Baraza la Madiwani cha Halmashauri ya wilaya hiyo kwamba hali ni tete katika kata yake na kata ya Ruvu wanakoishi wafugaji wa jamii ya Kimasai.
"Mheshimiwa mwenyekiti ni siku ya pili mfululizo kuna mapigano, watu waliojeruhiwa ni Juma Julius, Haruna Mashaka na mwingine aliyetambuliwa kwa jina mola la Hamisi...kuna mwanamke naye amepigwa na haijulikani alipo hadi sasa, ninaomba tamko katika hili," alisema.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa wilaya hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya, Herman Kapufi, alithibitisha kuwapo kwa mapigano hayo na kuongeza kuwa, tayari ametuma askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kwa ajili ya kudhibiti hali hiyo.
Aidha mkuu huyo wa wilaya alisema lengo la kupeleka askari ni kuhakikisha wakulima wenye vibanda vyao katika kata ya Ruvu kwa ajili ya kusimamia kilimo wasidhurike wakati kesi ya msingi kuhusu umiliki halali wa eneo hilo itakapoamuliwa na mahakama ya ardhi.
Akizungumzia mgogoro huo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Same, Christopher Irira alisema baraza linakemea kuwapo kwa mapigano hayo na kutaka wenyeviti wa vijiji, watendaji na madiwani wa kata hizo mbili kuwatuliza wananchi wao kuepuka mapigano.

No comments: