Tuesday, July 15, 2014

MFUMO WA UTAWALA TAZARA KUFUMULIWA

Serikali za Tanzania na Zambia zimedhamiria kufanya mabadiliko makubwa ya kiutendaji katika Reli ya Mamlaka ya Tanzania na Zambia (TAZARA), kutoka mfumo wa awali kwenda wa kibiashara ili iweze kujiendesha kwa faida na kuleta tija.
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Alikuwa akielezea maazimio ya mkutano wa mawaziri wa Uchukuzi, Fedha na wa Viwanda na Biashara wa Tanzania na Zambia uliofanyika Julai 4 Lusaka, Zambia.
Alisema wanaendelea na mchakato wa kubadilisha sheria iliyoanzisha Tazara ili ijiendeshe kibiashara.
Kwa upande wa Tanzania, sheria hiyo imekamilika, lakini kwa upande wa Zambia bado, hivyo wanategemea kukutana  tena mwezi ujao ili kuwasilisha mapendekezo yao.
Alisema katika mkutano huo, pia waliazimia kwamba Tazara itapata viongozi wake wa kudumu na watapeleka madaraka ya Tazara kutoka Tazara makao makuu na kwenda mikoa, ambayo ni Tanzania na Zambia.
Alisema mkoa wa Tanzania, utaanzisha huduma ya treni kutoka Dar kwenda Zambia kwa kuanzia na safari za mara mbili kwa wiki, ambayo itakuwa ni Jumanne na Ijumaa ;na abiria wakiwa wengi wataongeza safari zaidi.
Pia, alisema wameamua kuanzisha Treni Maalum kati ya Makambako kwenda Mlimba ambayo itakuwa na mabehewa matano ya abiria na mawili ya mizigo na pia itaanza kwa majaribio na safari mbili kwa kipindi chamiezi mitatu.
“Katika kikao hicho pia tulidhamiria kufufua migodi ya Tazara ili ifanye kazi kibiashara, ambapo kwa Tanzania tunaanza na juhudi zinazohusisha TRL, RAHCO na Mamlaka ya Bandari, ambapo tunajenga reli kutoka Kiwira kwenda Ziwa Nyasa kwenye Bandari ndogo,” alisema.
Alisema serikali zote mbili, zinaelewa mazingira magumu ya Tazara hivyo kwa pamoja wametoa dola milioni 2.8 kwa ajili ya mishahara ya miezi miwili kwa mkupuo kwa ajili ya wafanyakazi wa Tazara.
Alisema baada ya mabadiliko hayo kukamilika Tazara itajiendesha kibiashara na kama watafanya kazi kwa makini na bidii hawatahitaji tena kuchangiwa fedha na itaimarika kwa kipindi kifupi.
Aidha, Mwakyembe alisema katika mkutano huo unaotarajiwa kufanyika Agosti mwaka huu na kuwakutanisha mawaziri hao pia watapokea taarifa na mapendekezo ya utafiti uliofanywa na China katika reli hiyo.
Taarifa kutoka shirika hilo zilizopatikana baadaye zilieleza kuwa, uboreshaji wa miundombinu kuwezesha huduma za usafiri wa treni ya Tazara ndani ya mipaka ya kimkoa kwa upande wa Tanzania, itafanyika kwa kushirikiana na Kampuni ya Reli Tanzania (TRL), Mamlaka ya Bandari na wadau wengine muhimu.

No comments: