ASKARI CHUO CHA MAFUNZO ATUHUMIWA KWA WIZI WA FEDHA DUKANI...


Kamanda Mkadam Khamis Mkadam.
Jeshi la Polisi mjini hapa linamshikilia askari wa Chuo cha Mafunzo (Magereza) kwa tuhuma za wizi wa Sh 1,635,000 katika duka lililopo eneo la Makadara. 

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, jana alimtaja askari huyo kuwa ni Sajini Meja Hassan Iddi Hassan (45) wa Chuo cha Mafunzo Makao Makuu. 
Kamanda Mkadam alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 11 jioni wakati askari huyo akiwa amevaa kiraia, alipofika dukani hapo, mali ya Rashid Hamad Rashid mkazi wa Mwanakwerekwe, kama mteja wa kawaida na wakati mwuzaji wa duka hilo akimhudumia mteja mwingine upande wa pili, aliingia ndani na kwenda kwenye droo ya pesa na kuzichukua na kuondoka. 
Alisema wakati akichukua fedha hizo, alionwa na baadhi ya wateja na kumshitua mwuzaji huyo na kupiga kelele za mwizi akafukuzwa na wananchi na kwa vile eneo hilo lilikuwa karibu na kituo cha Polisi, askari walimwahi haraka na kumkamata kabla ya kupata kipigo kutoka kwa wananchi.
Kamanda Mkadam, alisema fedha zote alizokuwa ameiba mtuhumiwa huyo ziliokolewa na Polisi na kuhifadhiwa kama kielelezo mahakamani. Hilo ni tukio la tatu kutokea mjini Zanzibar mwaka huu ambapo tukio la kwanza ni jaribio la wizi katika maghala ya Bakhressa eneo la Fuoni nje kidogo ya mjini hapa, ambapo watuhumiwa watatu walikamatwa wakiwa na silaha aina ya gobori, linalotumia risasi za shotgun. 
Katika tukio lingine, watuhumiwa wanne wa  ujambazi akiwamo ofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini, wakiwa na silaha tatu zikiwamo bastola mbili na SMG moja, walikamatwa baada ya kumvamia mfanyabiashara na kumpora Sh milioni 11.5 eneo la Rahaleo. 
Matukio hayo yote yakiwa na jumla ya watuhumiwa wanane na silaha nne yalikabiliwa kwa haraka na Polisi kwa msaada wa wananchi waliotoa taarifa za haraka na pia kujitolea kusaidiana na askari kuwakabili watuhumiwa na kufanikisha ukamataji salama.

No comments: