Friday, November 8, 2013

SHEKHE PONDA ATINGA MAHAKAMANI BILA WAKILI WAKE...

Shekhe Ponda Issa Ponda.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro imeshindwa kuanza kusikiliza kesi inayomkabili Katibu wa Jumuiya ya Waislamu Tanzania, Shekhe Ponda Issa Ponda, kutokana na jalada la kesi hiyo kuitwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.

Hata hivyo, Shekhe Ponda naye alijikuta akiwa mahakamani  hapo tangu saa nne asubuhi, baada ya kuletwa na basi la Magereza chini ya ulinzi wa askari Polisi na askari Magereza, lakini bila Wakili wake, Juma Nassoro, anayemtetea kwenye  kesi hiyo.
Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mary Moyo  ambaye amechukua nafasi ya  Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama Mkoa, Richard Kabate aliyehamishiwa kikazi mkoani Dodoma, kabla ya kuanza kusikiliza kesi hiyo, alimwuliza Shekhe Ponda kuhusu wakili wake na yeye alijibu hakuwa na taarifa zozote kuhusu wakili huyo.
Akitoa maelezo ya awali Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama  hiyo , alisema kesi hiyo imefika hapo  kwa ajili ya kuanza kusikilizwa na kuuliza upande wa mashitaka  iwapo umeleta mashahidi wake.
Upande wa mashikata ukiongozwa na Wakili  Mwandamizi wa Serikali , Sunday Hyera  akisaidiana na Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Zabron Msusi, walimfahamisha hakimu kuwa walimleta shahidi wa kwanza,  askari Kingazi kwa ajili ya  kutoa ushahidi upande wa Jamhuri.
Hata hivyo, hakimu huyo alisema asingeweza kuanza kusikiliza kesi hiyo, kwa vile jadala halisi la kesi hiyo, liliitishwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam tangu Oktoba 15, mwaka huu na  bado lilikuwa halijarejeshwa mahakamani hapo.
Alisema kesi hiyo itaanza kusikilizwa iwapo jadala halisi, lililopelekwa Mahakama Kuu kupitiwa na Jaji, litarudishwa na   kwa sasa itakuwa ikitajwa tu mahakamani hapo.
Hakimu huyo  aliahirisha kesi hiyo hadi Novemba 21, mwaka huu itakapofikishwa tena mahakamani hapo kwa ajili ya  kutajwa  ;na aliamuru Shekhe Ponda arudishwe rumande.
Mahakamani  hapakuwa na wafuasi wake wengi, kama ilivyo kawaida ya siku za kesi hiyo, kwani baadhi yao walidhani  kuwa Shekhe Ponda asingeletwa mahakamani jana, kwa madai yao kuwa kuna kesi nyingine ya rufaa Mahakama Kuu, Dar es Salaam.
Mara ya mwisho kesi hiyo kufikishwa mahakamani hapo ilikuwa Oktoba mosi mwaka huu, Wakili Nassoro aliwakilishwa  na Wakili  Yahya Njama, aliyeiambia  Mahakama kuwa  Nossoro alienda nchini India kwa matibabu ya macho na  anatarajiwa kurejea Oktoba 25, mwaka huu baada ya  afya yake kutengemaa.
Ponda amefunguliwa kesi namba 128/2013 katika mahakama hiyo na  anakabiliwa na  mashitaka matatu, anayodaiwa kuyatenda Agosti 10, mwaka huu,  eneo la Kiwanja cha Ndege katika Manispaa ya Morogoro.
Kosa la kwanza anadaiwa kusema: “Ndugu Waislamu msikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti, kwani kamati hizo zimeundwa na Bakwata (Baraza la Waislamu Tanzania) ambao ni vibaraka wa CCM na Serikali.
“Kama  watajitokeza kwenu watu hao na wakajitambulisha kwamba wao ni kamati za ulinzi  na usalama za misikiti, fungeni milango na madirisha ya misikiti yenu na muwapige sana.”
Kauli hiyo inadaiwa iliumiza imani za watu wengine, na kwamba  ni kinyume cha hukumu ya Mahakama  ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam iliyotolewa na Hakimu Nongwa, Mei 9,  mwaka huu. Hukumu hiyo ilimtaka ndani ya mwaka mzima kuhubiri amani.
Katika shitaka la pili, Shehe Ponda anadaiwa kuwa Agosti 10 mwaka huu katika eneo la Kiwanja cha Ndege, Manispaa ya Morogoro,  mshitakiwa alitoa maneno yenye nia ya kuumiza imani nyingine za dini.
Maneno hayo anayodaiwa kusema ni: "Serikali ilipeleka Jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana  na gesi kwa kuwaua, kuwabaka, na kuwatesa wananchi kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Waislamu.
“Lakini Serikali haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo walipokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wake ni Wakristu."

No comments: