![]() |
| Kikao cha Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania kikiendelea mjini Dodoma. |
Hadhi
ya Bunge ambalo ni moja ya mihimili muhimu ya Dola, sasa imeanza kutiliwa shaka
na wasomi na wananchi wa kawaida, kutokana na mwenendo wa wabunge uliokosa
staha na ustaarabu wa uendeshaji wa vikao.
Wananchi
wasomi na wa kawaida, walionesha hofu hiyo jana walipozungumza na mwandishi
kuhusu mwenendo wa Bunge juzi na jana, uliooneshwa kwa wananchi moja kwa moja
kupitia televisheni ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).
Baadhi
ya wasomi walionesha hofu kuwa muhimili huo unaweza kugeuka wa kihuni, huku
watu wa kawaida wakilifananisha na kipindi cha futuhi cha ze komedi.
Wakizungumzia
hali ya Mkutano wa 10 wa Bunge hasa vikao vya juzi na jana, wasomi walieleza
kuwa ni matokeo ya siasa za kibabe,
jazba na inatishia usalama wa muhimili huo.
Mkuu
wa Idara ya Uchumi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Adolf Mkenda,
akizungumzia hali hiyo alisema: “Hakuna kitu muhimu kama kufuata kanuni, Spika
na wabunge wa pande zote wanapaswa kutii kanuni, ubabe haujengi na kupiga
kelele si suluhisho.”
Akifafanua
kuhusu kauli yake, Dk Mkenda alisema Bunge halipaswi kuwa la kishabiki, kwamba
Mbunge akifanya kitu cha ovyo, kwa kuwa ni wa upande fulani basi bila kujali
maslahi ya wananchi, anaungwa mkono.
Aliongeza
kuwa matokeo ya ushabiki wa aina hiyo, yatalipeleka Bunge kugeuka la kihuni.
“Wabunge hawapaswi kufanya mambo kwa ushabiki, hoja za msingi ni vizuri
zikafanyiwa kazi na wananchi wanataka kuona matokeo yake, si ushabiki.
“Wataishia
kupigana kama mabunge ya wenzetu tunayoyashuhudia, hili suala la kanuni
halimhusu mtu mmoja bali ni wabunge wote,” alisisitiza Dk Mkenda.
Alisema
kanuni zingezingatiwa, hali ya kelele bungeni juzi isingepata nafasi na
kuongeza kuwa wapinzani ambao waliongoza zaidi kupiga kelele, kutokana na
kuondolewa kwa hoja binafsi ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), walipaswa kuwa
waungwana.
Dk
Mkenda alisema kelele zao zinawaweka katika hatari ya kuonekana wahuni, huku
mhimili mzima ukiwa katika hatari hiyo pia.
Alisema
hoja za msingi kama vile ya Mnyika ya tatizo la maji katika Jiji la Dar es
Salaam, hazipaswi kuchukuliwa kama kitu cha mzaha na kuishia kwenye vurugu bila
mwafaka mzuri.
Profesa
Mwesiga Baregu, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustine (SAUT), alisema
kilichotokea bungeni ni matokeo ya mambo yanayotokea katika jamii,
yanayodhihirisha watu wamechoshwa na mambo yasiyotekelezwa.
“Kwa
mwenye akili finyu, zile ni vurugu lakini ukiwa na mtazamo mpana yanafanana na
yanayotokea katika jamii zetu leo, kama Mtwara, Iringa na kwingineko.
“Hali
hiyo haijatokea tu Tanzania, historia ya mabunge ya dunia iko hivyo, cha muhimu
ni kuondoa matabaka yanayosababisha wengine wadhani wanaonewa,” alisema Profesa
Baregu.
Kama
alivyoshauri Dk Mkenda, Profesa Baregu naye alishauri kanuni zifuatwe na
kuzingatiwa kuliko kitu chochote.
Pia
aliongeza kuwa, hoja za msingi zinazogusa maisha ya watu wanaowakilishwa katika
mhimili huo na wabunge, zinapaswa kuchukuliwa kwa uzito mkubwa.
Wananchi
wa kawaida na baadhi ya wafanyabiashara wa kituo cha mabasi cha Mwenge, Dar es
Salaam kwa nyakati tofauti walisema hawashangai kuona vurugu hizo zimehamia
bungeni.
Wananchi
hao walidai kuwa wanasiasa hao wamezoea kuwatumia katika kuongoza vurugu
mitaani kwa kisingizio cha kudai haki ndio maana hawashangai kuona zimehamia
bungeni.
“Kwa
kweli mimi sishangai kuhusu yaliyotokea bungeni, unajua bwana, baadhi ya watu
wanatumiwa na wanasiasa hao hao, sasa wananchi kwa muda mrefu tumekuwa
tukiumia, acha na wao siku moja ‘wadundane’ (wapigane) ili wajengeane heshima,”
alisema Nazir Mohamed, mfanyabiashara wa nguo Mwenge.
Huku
akiungwa mkono na vijana wenzake waliokuwa wanamsikiliza, Mohamed alisema Bunge
la Tanzania hivi sasa, linaelekea kupoteza mwelekeo na kuwa kama futuhi.
Hata
hivyo, katika hali ya kushangaza, Mohamed alisema aina hiyo ya Bunge ndiyo
inayovutia wengi hasa vijana kwa kuwa
wamechoka na maisha.
Hata
hivyo, mfanyabiashara mwenzake aliyejitaja kwa jina Jacob Mserera, alikuwa
kinyume na wenzake na kueleza kusikitishwa na utovu wa nidhamu uliooneshwa na
baadhi ya wabunge.
Mserera
alishauri wabunge wakongwe waliomo bungeni, watoe mafunzo ya maadili kwa
wabunge vijana, ili kuwarithisha mema.
Juzi,
wabunge wengi wao wakiwa wa upinzani, walisimama bungeni wakati Naibu Spika Job
Ndugai akiwa amesimama, kinyume cha kanuni za Bunge.
Kanuni
hizo ziliweka bayana kwamba, Spika, Naibu Spika au Mwenyekiti anapokuwa
akiongoza kikao cha Bunge, akisimama mbunge yeyote aliyesimama anapaswa kukaa
chini kusikiliza anachosema aliyekuwapo kwenye Kiti.
Kutokana
na ukiukwaji huo wa kanuni, huku wabunge hao wakipiga kelele kama darasa la
watoto watukutu, Ndugai aliahirisha
Bunge na kuagiza Kamati ya Bunge ya Uongozi ikutane kujadili hali hiyo.
Jana
Spika, Anne Makinda alitoa maelezo kuhusu uamuzi wa Kamati, ikiwa ni pamoja na
kulifikisha suala hilo katika Kamati ya Haki na Maadili na Madaraka ya Bunge,
ili lifanyiwe kazi.
Hatua
hiyo ilisababisha baadhi ya wabunge, kurudia walichofanya juzi na kupiga kelele
hali iliyosababisha Spika kuahirisha Bunge hadi leo.
Spika
Makinda aliamua kuahirisha Bunge na kusitisha kujadili hoja binafsi katika
mkutano huo kutokana na utovu wa nidhamu uliooneshwa juzi bungeni na
kumlazimisha Ndugai, kuahirisha shughuli za Bunge kabla ya wakati.
Hoja
binafsi iliyokumbwa na hatua hiyo, ni ya Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua
Nasari (Chadema) ambayo ilitakiwa kuwasilishwa jana ikiitaka Serikali iunde
kamati ndogo kuchunguza Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) namna linavyoathiri
elimu nchini.
Akitangaza
taarifa ya Kamati ya Uongozi bungeni jana, Spika Makinda alisema, uamuzi wa
kutojadili hoja hizo ulifikiwa na Kamati ya Uongozi ya Bunge iliyokutana kwa
dharura juzi na kujadili vurugu zilizoibuka bungeni kwamba zilitokana na
kujadili hoja binafsi.
“Kwa
masikitiko makubwa sote tulishuhudia vurugu zilizojitokeza katika Bunge hili
hasa wakati wa mjadala wa hoja binafsi za wabunge, kimsingi huu ulikuwa ni
utovu wa nidhamu wa hali ya juu kutokea katika historia ya Bunge letu.
“Taasisi
ya Bunge inalaani vitendo vilivyojitokeza jana vilivyovunja kanuni ya 60 (2)
inayokataza Mbunge kuzungumza kabla ya kuruhusiwa na Spika na Kanuni ya 60 (12)
inayowataka wabunge kukaa chini wakati wowote Spika anaposimama kutaka
kuzungumza,” alisema.
Katika
vurugu hizo za juzi, mvutano uliibuka wa kutumia kanuni kati ya Mbunge wa
Singida Mashariki, Tundu Lissu na Ndugai kuwa alimruhusu Waziri wa Maji,
Profesa Jumanne Maghembe kutumia muda mwingi wakati ulitakiwa kutolewa kwa mtoa
hoja, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema).
Katika
vurugu hizo, wapinzani walikuwa wakidai Kiti cha Spika hakitendi haki
kinaipendelea Serikali hivyo walisimama na kuimba CCM, CCM, kitendo ambacho
kiliishia kwa kupiga kura na kuiondoa hoja ya Mnyika kwa kigezo kwamba haikuwa
na uzito, kwani tayari Serikali ilishawekeza fedha nyingi katika miradi ya maji
inayotekelezwa Dar es Salaam.
Spika
Makinda alisema kutokana na vurugu hizo, Kamati ilifikia uamuzi wa kuzikemea
kwa nguvu vurugu hizo ili kulinda heshima ya Bunge na kuhakikisha kwamba
vitendo hivyo haviachwi vikaendelea na kusababisha madhara makubwa hata ya
kupigana bungeni.
Kamati
ilikubali pia suala la vurugu hizo lipelekwe kwenye Kamati ya Haki, Maadili na
Madaraka ya Bunge ili ichunguze na kuleta mapendekezo bungeni kabla ya mkutano
huu kumalizika.
Akitoa
ufafanuzi alisema, tangu Januari 30 hadi Februari 4 Bunge liliamua kuruhusu
kuwasilisha bungeni hoja binafsi za wabunge ambazo ziliahirishwa katika mkutano
wa tisa kwa nia njema ya kujadiliana masuala makubwa ya kitaifa.
Alitaka
wabunge wa kambi ya upinzani wasome kanuni za Bunge kwani, hoja binafsi za
wabunge zinaongozwa na kanuni kuanzia ya 53 hadi 58 na ya majadiliano kuanzia
59 hadi 71 ambazo kwa ujumla wao zingefuatwa kama inavyotakiwa, vurugu
zisingetokea bungeni.
Alisema,
Kanuni za Bunge ya 54(1)-(2), zinaeleza wazi kuwa Mbunge anaweza kutoa hoja
bungeni ili kupendekeza jambo lolote lijadililiwe na pendekezo hilo linatakiwa
liwe limekamilika ili lipate uamuzi bayana wa Bunge.
Alisema kifungu cha 53 (6) c kinaonesha wazi ikiwa
hoja ni ya Serikali, msemaji wa kambi ya upinzani atapewa nafasi ya kutoa maoni
juu ya hoja hiyo, na kama hoja si ya Serikali, basi Msemaji wa Serikali atapewa
nafasi ya kutoa maoni ya shughuli za Serikali juu ya hoja hiyo kama Profesa
Maghembe alivyopewa.
Kanuni
ya 62 inabainisha kuwa muda utakaotumiwa
na wazungumzaji mtoa hoja ana dakika 30 na anayetoa maoni ya upande wa pili anapewa muda wa dakika 30 kama ilivyofanyika
kwa Profesa Maghembe kutoa maoni ya shughuli za Serikali.
Kuhusu
madai kwamba Kiti kinatoa upendeleo wa wazi kwa Serikali dhidi ya upinzani,
alisema jambo hilo si kweli, hata hivyo, alisisitiza kuwa kama uamuzi
unaofanywa na Kiti una kasoro kanuni zinaruhusu mbunge ambaye hakuridhika na
uamuzi huo, kukata rufaa kwenye Kamati ya Kanuni za Bunge kwa mujibu wa Kanuni
ya 5 (4).
Mbunge Nassari alihoji kutojadiliwa hoja yake
kwa kutumia kanuni namba 58 kwamba imeondolewa na Kamati ya Uongozi, lakini
kikanuni inatakiwa iondolewe na mbunge husika, hoja ambayo Spika aliipangua kwa
kusema Kamati ya Uongozi ina wajibu wa kupanga ratiba na ndivyo ilivyopanga.
No comments:
Post a Comment