Friday, August 24, 2012

PAPAA MSOFFE AUGUA, ASHINDWA KUTOKEA MAHAKAMANI...

Mfanyabiashara maarufu jijini Dar es Salaam, Marijani Abdubakari Msoffe (50) maarufu kwa jina la ‘Papa Msoffe' ameshindwa kufika mahakamani katika kesi yake inayomkabili ya mauaji akidaiwa kuwa ni mgonjwa. Kesi ya Papa Msoffe ilipangwa jana kutajwa ambapo mshitakiwa huyo alitakiwa kuletwa mahakamani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu lakini badala yake hakuonekana mahakamani.
Wakili wa serikali Mwanaisha Kombo aliiambia Mahakama mbele ya Hakimu Mkazi, Agnes Mchome kuwa kesi imekuja kutajwa lakini mshitakiwa hajaletwa mahakamani.
"Kesi imekuja kutajwa lakini Mheshimiwa mshitakiwa hajaletwa mahakamani," alidai mwendesha mashitaka.
Hata hivyo ilidaiwa kuwa maofisa wa magereza wameleta mahakamani hapo cheti cha mshitakiwa huyo kwa sababu ni mgonjwa hivyo amebaki gerezani.
Kesi hiyo mahakama iliahirishwa hadi Septemba 5 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.
Msoffe ambaye ni mkazi wa Mikocheni, anakabiliwa na kosa moja la mauaji ambalo ni kinyume na kifungu cha 196 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.
Anadai kuwa Novemba 6 mwaka 2011 huko Magomeni Mapipa, Papa Msoffe anayetetewa na wakili wa kujitegemea, Majura Magafu alimuua Onesphory Kitoli.
Papa Msoffe ambaye jina lake limekuwa likitajwa mara kwa mara kwenye nyimbo zinazopigwa na Bendi za Miziki ya Dansi nchini hii siyo mara ya kwanza kufikishwa katika mahakama hiyo kwa makosa mbalimbali ya jinai.

No comments: