Idadi ya watu
waliokufa kutokana na ajali ya moto wa lori lililopinduka na kisha kulipuka
baada ya watu kulivamia kwa lengo la kujipatia mafuta, imeongezeka na kufikia watano
kutoka vitatu vya awali.
Hayo
yamethibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman
Kova.
Alisema
katika ajali hiyo iliyotokea juzi usiku eneo la Mbagala, watu 16 walijeruhiwa
baada ya kuungua maeneo mbalimbali ya miili yao.
Ajali hiyo
ilihusisha lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 347 BXG mali ya Moil
Transporter lililokuwa likitarajiwa kusafirisha mafuta kuelekea Kampala, Uganda
likiwa na kemikali aina ya petroli lita 38,000 inayokadiriwa kuwa na thamani ya
dola 36,000 (Sh milioni 60).
Aliwataja
waliokufa kuwa ni Hassan Mohammed (25), mkazi wa Mbagala Kimbangulile, Masoud
Masoud (33), Mohammed Ismail (19), Ramadhani Khalfan (36) na Maulid Rajabu,
wakazi wa Mbagala Charambe.
Majeruhi
waliotambuliwa ni Hamis Ally (35), mkazi wa Mbagala Kiburugwa, Rajabu Selemani
(28), mkazi wa Tandika, Idd Said (28), Janney Mathayo (25), mkazi wa Mbagala
Kizuiani, Mathayo Daniel (21), mkazi wa Mbagala Charambe na askari polisi,
Koplo Thomas aliyejeruhiwa na jiwe kwenye paji la uso wakati akijaribu kuzuia
vibaka kuchota mafuta kabla ya kulipuka.
Alisema
majeruhi wengine 10 wamelazwa katika hospitali ya Taifa Muhimbili na Hospitali
ya Wilaya ya Temeke wakiendelea na matibabu na wengi wao hali zao siyo za
kuridhisha.
Kamanda Kova
aliongeza kuwa, mbali ya kusababisha vifo na majeruhi, ajali hiyo pia
ilisababisha kuungua kwa nyumba ya kulala wageni iitwayo United yenye vyumba
32, mali ya Deus Kasigwa (42), mkazi wa Mtoni Mtongani. Moto huo uliteketeza
pia maduka matano yenye vitu vyenye thamani ya Sh milioni 197 na pipikipiki
saba ziliteketea kabisa na moto.
Naye Ofisa
Uhusiano wa Hospitali ya taifa ya Muhimbili, Doris Ishenda alisema majeruhi 11
wanaoendelea kutibiwa hospitalini hapo, huku akiongeza kuwa, hali zao sio nzuri
kwa kuwa waliunguzwa vibaya na moto na kwamba madaktari wanaendelea kuwapatia
matibabu.
‘’Majeruhi
wote wamelazwa katika wadi namba 22 ya Sewa Haji wanaendelea na matibabu,
lakini hali zao sio nzuri kabisa kwani waliungua sana,’’ alisema Ishenda.
Wakati huo
huo, Paulo Milanzi (35), mkazi wa Chanika katika manispaa ya Ilala
anayetuhumiwa kushiriki katika mauaji ya Ofisa Usalama wa Taifa, Sylvanus
Mzeru, amefariki dunia baada ya kupigwa risasi katika majibizano na polisi.
Kova alisema mtuhumiwa huyo alikuwa akitafutwa na polisi
kwa muda mrefu kuhusu matukio mbalimbali ya mauaji na unyang’anyi wa kutumia
silaha jijini Dar es Salaam na mikoa ya jirani.