Friday, September 19, 2014
Thursday, September 18, 2014
MABINTI PACHA WALIOUNGANA KUHITIMU KIDATO CHA NNE MAKETE
Hatua
ya kwanza ya ndoto ya kuzama katika elimu ya mabinti pacha walioungana
kiwiliwili, Consolata na Maria Mwakikuti (18) wa Kijiji cha Ikonda wilayani
Makete mkoa mpya wa Njombe, inatarajiwa
kutimia Novemba mwaka huu, wakati mabinti hao watakapofanya mtihani wa kuhitimu
kidato cha nne.
Itakumbukwa
kwamba walipokuwa wakimaliza elimu ya msingi mwaka 2009 kijijini kwao Ikonda,
walikuwa na umri wa miaka 13 na katika ndoto zao kwa pamoja walisema wanataka
kuwa wasomi waliobobea katika utaalamu wa kompyuta. Lakini, kwa sasa, wanasema
wanatamani kufanya kazi ya Ukatibu Muhtasi.
Wanafunzi
hao ambao mwaka 2010 walichaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Wasichana
ya Jangwani, Dar es Salaam.
Kwa
sasa wanasoma katika Shule ya Sekondari ya Maria Consolata iliyopo Kidabaga
wilayani Kilolo mkoani Iringa.
Shule
hiyo inamilikiwa na Kituo cha Nyota ya Asubuhi ya Wamisionari Wakatoliki wa
Italia, kinachosaidia kuwatunza watoto wanaotoka katika mazingira magumu.
Wakizungumza
na mwandishi wa habari hii shuleni hapo hivi karibuni, walisema wanafurahi kuwa
miongoni mwa watahiniwa watakaofanya mtihani huo wa kidato cha nne mwaka huu.
"Tunafurahi,
tunajiandaa tunasoma kwa bidii, mtihani uko karibu tunataka tufaulu vizuri
masomo yetu, ili ile ndoto yetu ya kuwa Makatibu Muhtasi itimie," walisema
Maria na Consolata, ambao wanatumia baiskeli maalumu kuwapeleka darasani,
ambako pia wana kiti maalumu.
Pacha
hao wameshangaza watu wengi kwa jinsi walivyo, ambapo kila mmoja ana madaftari
yake. Wakati wa kufanya mazoezi au kuandika kazi wanazopewa, mmoja huanza
kuandika, akimaliza na mwingine huandika.
"Wala
hatupati shida tumezoea, kila mmoja anafanya kazi yake, mimi naandika kwa mkono
wa kushoto na Maria anaandika kwa mkono wa kulia," anasema Consolata,
ambaye anaonekana kuwa mchangamfu zaidi.
Shule
hiyo ina wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne. Ilianzishwa mwaka 2006 na
hivi sasa ina jumla ya wanafunzi 183. Wote wanaishi kituoni hapo na wote
wanatoka kwenye mazingira magumu.
Changamoto
kubwa iliyokuwa shuleni hapo ni ukosefu wa nishati ya umeme, ambapo uongozi wa
shule na kituo hicho unalazimika kutumia jenereta na umemejua, jambo ambalo
mapema wiki hii Wakala wa Nishati ya Umeme Vijijini (REA), imewaondolea adha kwa
kuwapelekea umeme.
Pacha
hao walizaliwa mwaka 1996 wakiwa wameungana katika Hospitali ya Ikonda wilayani
Makete mkoani Iringa.
Walifaulu
mtihani wa darasa la saba mwaka 2010, ambapo kila mmoja alipata alama 151,
ingawa walitofautiana ufaulu kwenye masomo
yao.
Katika
somo la Maarifa ya Jamii, Consolata alipata alama 29 na Maria alama 25, kwenye
somo la Kiingereza, Maria alipata alama 36 na kumzidi Consolata aliyepata alama
34, wakati kwenye somo la Sayansi, Maria alimzidi Consolata kwa kupata alama 31
dhidi ya 29.
Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi iliwapanga pacha hao kujiunga na kidato cha
kwanza katika Shule ya Sekondari Jangwani jijini Dar es Salaam.
Hata
hivyo hawakujiunga na sekondari hiyo, kutokana na hali yao na pia umbali kutoka
Iringa hadi Dar es Salaam. Ndipo Wamisionari hao wakawachukua mwaka 2011 na
kuanza kidato cha kwanza.
Walizaliwa
kwenye Hospitali ya Misheni ya Ikonda mwaka 1996. Lakini, taarifa zao
hazikufahamika hadi pale walipoandikishwa kuanza elimu ya msingi Ikonda na
kutafutiwa mlezi wa kuwaangalia, baada ya wazazi wao kufariki dunia wakiwa bado
wadogo.
MAANDAMANO YA CHADEMA MARUFUKU, VYUO VIKUU 14 VYAYALAANI
Jeshi la Polisi nchini limepiga marufuku
maandamano ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), yaliyotarajiwa
kuanza kufanyika leo katika maeneo mbalimbali nchini.
Jeshi
hilo limeonya kuwa maandamano hayo ni batili na ni kinyume cha sheria.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana makao makuu ya jeshi la Polisi Dar es Salaam,
Kamishna wa Polisi wa Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja alisema jeshi hilo
limeanza kupokea taarifa ya chama hicho, kikitaka kufanya maandamano kuanzia
leo. Lakini, alisisitiza kuwa maandamano hayo hayataruhusiwa.
“Septemba
15 jeshi lilitoa taarifa kuhusu kauli iliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema,
Freeman Mbowe akiwahimiza wafuasi wa chama chake kufanya maandamano na migomo
isiyokoma pote nchini ili kusitishwa kwa Bunge la Katiba na hivi sasa tumeanza
kupokea taarifa ya chama hicho kufanya maandamano,” alisema.
Alisema
maandamano hayo ni batili, kwa sababu Bunge la Katiba linaloendelea hivi sasa,
linafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na hakuna sheria
iliyokiukwa, hivyo kitendo cha kufanya maandamano, kushinikiza kuvunjwa kwa
Bunge hilo ni kinyume cha sheria, jambo ambalo jeshi la polisi haliwezi
kuruhusu.
Aidha,
alisema kuwa ieleweke wazi kwamba Bunge la Katiba, lipo kisheria na kila jambo
linalofanyika bungeni ni kwa mujibu wa sheria.
Chagonja
alisema jeshi la polisi lina jukumu la kulinda watu wote, wanaotekeleza
majukumu yao kwa mujibu wa sheria.
“Hata
hivyo, hivi sasa kuna kesi inayoendelea Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,
inayohoji uhalali wa kuendelea kwa Bunge hilo na kesi hiyo haijafikia mwisho na
uamuzi kutolewa, hivyo maandamano hayo yaliyopangwa na Chadema yanaingilia
uhuru wa Mahakama, jambo ambalo siyo sahihi. Mahakama kama chombo cha kutoa
haki, kiachwe kifanye kazi yake,”
alisema.
Chagonja
alitoa mwito kwa wananchi wote, kuendelea na shughuli zao na yeyote
atakayekiuka katazo hilo, jeshi la polisi halitasita kumchukulia hatua kali kwa
mujibu wa sheria.
Wakati
Chagonja akiyasema hayo, Kamanda wa Polisi mkoani Dodoma, amewaonya wafuasi wa
Chadema wanaodaiwa kutaka kuandamana hadi Viwanja vya Bunge
kushinikiza
kusitishwa kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Hata
hivyo, uongozi wa Chadema mkoani humo, umedaiwa kusisitiza maandamano yako
palepale.
Akizungumza
jana, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Emmanuel Lukula alisema
maandamano hayo, pia yamepangwa kufanyika katika wilaya zote za mkoa wa Dodoma.
Alisema
juzi walipokea taarifa kutoka kwa Uongozi wa Chadema Mkoa wa Dodoma, juu ya
kufanya maandamano ya amani kuanzia viwanja vya Nyerere Square hadi viwanja vya
Bunge kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 6 mchana.
Alisema
taarifa ya maandamano kama hayo, yanayotarajia kufanyika katika wilaya zote za
mkoa wa Dodoma, ilitolewa jana ambapo ni muda ulio kinyume na sheria ya kutoa
taarifa za maandamano ndani ya saa 48.
Alisema
katika barua ya chama hicho kwenda kwa Jeshi la Polisi, viongozi wa Chadema wa Mkoa huo, walisema wanapinga Bunge la
Katiba na wanataka kupaza sauti zao,
zisikike dunia nzima na walisisitiza kufanya maandamano hayo leo.
“Walikuja
hapa viongozi wa Chadema Mkoa, tulikaa nao kwenye mazungumzo zaidi ya saa
mbili, tuliwaambia Bunge lipo kwa mujibu wa sheria za nchi na hakuna mahakama
iliyotamka Bunge lisitishwe, lakini walisisitiza kuwa maandamano yako pale
pale,” alisema.
“Maandamano
hayo ni batili yanapinga chombo ambacho kipo kwa mujibu wa sheria, tunasisitiza
wananchi wa Dodoma wasishiriki maandamano hayo, hayana tija hata kidogo na
wananchi wasijitokeze waendelee na shughuli zao,” alisema.
Alisema
maandamano ni haki ya kikatiba, lakini wanatakiwa kufuata sheria. Alisema Jeshi
la Polisi limejipanga kudhibiti maandamano hayo katika wilaya zote, kutokana na
viongozi wa Chadema kukaidi amri ya kutaka kusitisha maandamano hayo.
Wakati
jeshi la Polisi likichukua hatua hiyo, Umoja wa Vijana Wazalendo wa Vyuo vya
Elimu ya Juu Dar es Salaam, nao umejitokeza na kulaani kauli zilizotolewa na
Mbowe za kuhamasisha maandamano na migomo nchi nzima, hata kama jeshi la Polisi
halitabariki kufanyika kwa mambo hayo.
Mwenyekiti
wa Umoja huo, Mussa Omar anayesoma Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), alisema
umoja huo ni Muungano wa vyuo 14 vya elimu
ya juu vilivyopo Dar es Salaam.
Alisema
Watanzania wengi wamekerwa na kusononeshwa na kauli ya kiongozi huyo ya
kuhamasisha maandamano, alizozitoa wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa
uchaguzi wa Chadema, mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
“Tumemsikia
akiahidi maandamano bila kikomo kwa kibali cha polisi au bila kibali cha polisi
mbele ya wajumbe na wageni ambao wengine sio Watanzania,” alisema Omar.
Aliongeza kuwa kauli kama hiyo, haiwezi
kusemwa hata na Rais ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu.
Alimtaka Mbowe afahamu dhamana kubwa ya
uongozi aliyonayo kwa wafuasi wake na Watanzania kwa ujumla, wakimtaka afuate
misingi ya sheria za nchi, katiba na utawala bora.
Pia, alisema kauli zilizotolewa na Mbowe,
hazibebeki na mtu yeyote katika taifa hili, kwani alitoa kauli mbaya kuliko
zote kisiasa, ambazo zimewahi kusemwa majukwaani.
“Watanzania tukikaa bila kuzilaani na
kuzikemea kauli zake tutakuwa hatujitendei haki sisi wenyewe na pia
hatuvitendei haki vizazi vijzvyo vya nchi yetu,” aliongeza.
Alihoji uhalali wa kutoa amri hizo kwa
wafuasi wake, ilhali ni kiongozi tu wa chama, tena ambacho hakiko madarakani.
Alisema Watanzania wanapaswa kuwakataa
viongozi wenye jazba na kutumia mabavu katika kutimiza majukumu yao, kwani
wanaweza kuiingiza nchi katika vurugu zisizo na ulazima.
Pia alivitaka vyombo vya dola,
visizivumilie kauli kama hizo, zilizotolewa na Mbowe, kwani vyombo vya dola
vina dhamana ya kulinda, kutunza na kuendeleza amani na utulivu wa nchini,
wachukue hatua kali za kisheria kwa kauli ya kutishia uvunjifu wa amani kabla
hajaingiza nchi kwenye machafuko ya kisiasa.
Wakati
huo huo, viongozi wa juu wa chama hicho, leo wamepanga kumsindikiza Mbowe
kwenda Makao Makuu ya Jeshi la Polisi nchini, ambako ameitwa kwa barua.
Katibu
Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alisema Mbowe alipokea barua, ikimtaka
afike Makako Makuu ya jeshi hilo leo saa 5:00 asubuhi.
“Mwenyekiti
wetu ameitwa Makao Makuu ya Polisi leo na hatujui kaitiwa nini, huenda
anakwenda kuhojiwa na huenda mwito huo umetokana na kauli alizotoa awali katika mkutano mkuu, ambazo
zililenga kuhamasisha maandamano ya nchi nzima kupinga Bunge la Katiba linaloendelea”,
alisema Dk Slaa.
Alitaja
watakaoongoza msafara wa amani wa kumsindikiza Mbowe kuwa ni mwanasheria wao, mbunge wa Singida Mashariki,
Tundu Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Bara), Profesa Abdallah Safari na
Mwanasheria Peter
Kibatala.
Hata
hivyo, alisema pamoja na kiongozi huyo kuitwa na polisi, bado jeshi hilo
haliwezi kuvunja ajenda ya kuandamana, kwa kuwa ilipitishwa na Kamati Kuu ya
chama hicho, na kwamba polisi wao wanapaswa kutoa kibali cha kuruhusu
maandamano hayo.
Awali,
alisema maazimio yaliyopitishwa na
Kamati Kuu ya chama hicho ni kuunganisha nguvu ya pamoja na vyama
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) .
Alisema
maazimio hayo, yataanza Desemba 14, mwaka huu, siku ambayo uchaguzi wa serikali
za mitaa unaanza.
Alieleza
kwamba chama hicho kimeunda kamati ya watu watano, itakayoangalia jinsi
ushirikiano wa Ukawa utakavyokuwa kwenye uchaguzi huo.
Hata
hivyo, alisisitiza kuwa kutoka kwao nje bungeni, kulikuwa sahihi. Alisema
katiba mpya, haiwezi kupatikana leo au kesho.
ASKARI WA DORIA WASHAMBULIWA KWA BOMU SONGEA
Siku chache baada ya majambazi kuvamia
Kituo Kikuu cha Polisi wilayani Bukombe mkoani Geita, kuua askari wawili na
kuiba silaha za moto, watu wasiofahamika wamewajeruhi askari watatu waliokuwa
doria kwa kuwarushia kitu kinachosadikiwa kuwa ni bomu.
Askari hao kwa sasa wamelazwa katika
Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma iliyopo mjini Songea wakitibiwa majeraha.
Tukio hilo limeripotiwa kutokea usiku wa
kuamkia jana majira ya saa moja na nusu jioni katika kata ya Msufini karibu na
daraja la Matarawe, wilayani Songea.
Mkurugenzi wa Upelelezi na Makosa ya Jinai
(DCI), Issaya Mngulu amethibitisha kwa njia ya simu kutokea kwa tukio hilo,
ingawa alishindwa kuingia kwa undani akisema alikuwa njiani kwenda eneo la
tukio akitokea mkoani Mbeya.
Hata hivyo, mwandishi ameweza kubaini
waliojeruhiwa kuwa ni WP. 10399 PC Felista aliyejeruhiwa mguu wa kulia kwenye unyayo na pajani, G 7351 PC Ramadhani
aliyejeruhiwa mguu wa kulia karibu na goti na tumboni upande wa kulia na G.
5515 PC John aliyepata majeraha katika mguu wa kulia chini ya goti na jeraha
dogo tumboni.
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma,
Dk Daniel Malekela, akizungumzia tukio hilo alikiri kupokea majeruhi na kueleza
kuwa ametoa vipande vya bati na misumari katika majeraha ya askari hao na mpaka
sasa wanaendelea na matibabu.
Habari zaidi zinasema jeshi la polisi
mkoani humo kwa kushirikiana na maofisa wengine kutoka makao makuu ya jeshi,
wanaendelea na uchunguzi, ikiwa ni pamoja na kujua chanzo cha tukio hilo. Bomu
hilo la kutupwa kwa mkono inasadikiwa limetengenezwa kienyeji.
Kutokana na tukio hilo, Mkuu wa Mkoa wa
Ruvuma, Saidi Mwambungu ameelezea kusikitishwa na kitendo hicho cha wahalifu
kujeruhi askari kwa makusudi na amesema Serikali kupitia vyombo vyake vya
ulinzi na usalama itahakikisha wanawasaka na kuwakamata.
WAFA KATIKA AJALI WAKITOKA KUZIKA MWENZAO MUSOMA
Watu
wawili wamekufa na wengine watano kujeruhiwa baada ya magari mawili, likiwamo
basi dogo la abiria walilokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso na lori la
mafuta.
Kwa
mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Athuman Mwambalaswa alisema
kuwa tukio hilo lilihusisha gari aina ya Toyota Coaster lililokuwa linatokea
kwenye msiba Musoma mkoani Mara kwenda Dar es Salaam na kugongana na lori la
mafuta.
Kamanda
Mwambalaswa alisema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi maeneo ya Ubena Senge katika
barabara ya Morogoro, chanzo kikitajwa kuwa ni uzembe wa gari dogo aliyehama
upande wake kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni uchovu wa safari ndefu.
Alisema
basi dogo lenye namba za usajili namba T 663 BKP lililokuwa likiendeshwa na
Ally Abdul (34), likiwa na abiria 20 liligongana na lori la mafuta aina ya
Leyland Daf lenye namba za usajili T 858 CLK na tela namba T 421 CKY, mali ya
kampuni ya Ramader ya Dar es Salaam ambalo dereva wake ametajwa kwa jina moja
la Rashid.
Aliwataja waliokufa kwenye ajali hiyo kuwa
ni Neema Mile (39) na Jane Mtani (38) ambao miili yao imehifadhiwa katika
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani, Tumbi ambako pia majeruhi wamelazwa.
MTUHUMIWA KESI YA UGAIDI ALALAMIKIA POLISI
Mtuhumiwa
katika kesi ya ugaidi, Abdallah Maginga, ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi
Arusha, kumruhusu kutohudhuria siku za kesi na abaki magereza, kutokana na
maumivu makali anayodai anayapata sehemu za siri alikominywa na polisi na
kuingiziwa mti kwenye haja kubwa.
“Mheshimiwa
Hakimu naomba mahakama yako inipe ruhusa ya kutohudhuria siku ya kesi, sababu
ninapopanda gari napata maumivu makali sana sehemu za siri kunauma kwa sababu
polisi walinitesa kwa kuniingizia mti kwenye haja kubwa na kuminya sehemu zangu
za siri,” alisema.
Alisema
mbele ya Wakili wa Serikali, Rose Sulle kuwa mbali na maumivu ya sehemu za
siri, pia mguu wake uliokatwa hospitalini, bado unamsumbua kutokana na maumivu.
Maginga
pia aliomba iagize Magereza wamruhusu akatibiwe hospitalini, kwani alitakiwa
kwenda kupata matibabu Septemba 5 mwaka huu, ila alizuiwa hadi sasa.
Akijibu
hoja hizo, Hakimu aliyesikiliza kesi hiyo, Devotha Msofe, alisema suala la kuja mahakamani ni lazima na
mahakama haiwezi kumpa ruhusa hiyo.
Pia,
alimshauri mshitakiwa huyo kuwa kama ana maelezo mengi, amweleze hakimu
anayesikiliza kesi yake, Mustapher Siyani ambaye kwa siku hiyo hakuwepo.
“Sikiliza
Maginga suala la kuja mahakamani ni lazima na sio hiyari wala majadiliano, ila
kuhusu kwenda hospitalini liwasilishe Magereza ndio mtaona kwa pamoja
mnafanyaje,” alisema.
Awali
ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washitakiwa
hao wameshitakiwa kwa makosa yaliyo chini ya Sheria ya Kuzuia ugaidi,
ambapo Sheria Namba 22 ya Mwaka 2002
inasema upelelezi ukishakamilika, Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya
kuisikiliza na kutoa uamuzi.
Washitakiwa
hao wanakabiliwa na mashitaka ya kuua, kujaribu kuua, kusajili na kusafirisha
vijana kujiunga na Al-Shabaab.
Mbali
na mashitaka hayo, pia wanahusishwa na
tukio la mlipuko wa bomu
lilitokea baa ya Arusha Night Park
jijini Arusha na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kujeruhi wengine 16.
Watuhumiwa wengine wanaokabiliwa na
mashitaka hayo ni Abdallah Athumani, Abdallah Thabiti, Ally Hamisi, Abdallah
Wambura, Rajab Hemedi, Hassan Saidi, Ally Hamisi, Yassin Sanga, Shaaban Wawa,
Swaleh Hamisi, Abdallah Yassin, Abdallah Maginga na Sudi Nassib Lusuma. Wengine
walioongezwa katika shauri hilo ni Shaaban Mussa, Athuman Hussein, Mohammed
Nuru, Jafari Lema, Abdul Mohammed na Said Michael Temba.
MWANAFUNZI AJIUA KWA KULAZWA HOSPITALINI
Katika
hali isiyotarajiwa, mwanafunzi wa Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya
Wavulana Ihungo Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera, Ezra Gerald (19), amejinyonga
hadi kufa kwa kutumia shuka ya hospitali, alikokuwa amelazwa kwa kile kinachoeleza
alikuwa anasumbuliwa na homa ya matumbo.
Hata
hivyo, ujumbe ulioachwa na marehemu huyo unaonesha alichukua uamuzi huo,
kutokana na kuchukizwa na uamuzi wa daktari aliyemhudumia wa kumlaza ili
atibiwe ugonjwa ambao hakuwa anaumwa.
Aidha,
katika ujumbe huo imeelezwa alichukizwa na kitendo cha kupotezewa muda
hospitalini wakati wenzake wakiendelea na masomo.
Tukio
hilo limethibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Gilles Muroto
aliyesema mwanafunzi huo alijinyonga Septemba 16 mwaka huu saa moja asubuhi.
Alisema
mwili wake uligundulika ukining’inia kwenye mti uliopo maeneo ya hospitali hiyo
na alipopekuliwa katika mifuko ya suruali yake, zilionekana karatasi mbili,
moja ikiwa na ujumbe uliosomeka; “Haiwezekani binadamu kuhudumiwa kama mbwa,
yaani nafika hospitali najieleza hali yangu halafu daktari ananiandikia kulazwa
bila kupima, sasa sijui wanatibu nini?
“Kwa
kweli siwezi kuvumilia wenzangu wanasoma halafu mimi nimekalishwa tu hapa
hospitali bila kujua wananitibu nini, inaniuma sana mpaka nafikia hatua hii ya
kujiondoa duniani kwa sababu naona watu wanachezea ndoto zangu, mimi siwezi
kuona ndoto yangu inazimwa wakati natakiwa niwepo shuleni nikamilishe ndoto
zangu “mjitahidi tukutane mbinguni “Respect My Family and Brother Henry.”
Kamanda
Muroto amesema hakuna aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo, lakini polisi
wanaendelea na uchunguzi.
Inaelezwa
mwanafunzi huyo aliyetajwa kuwa ni mwenyeji wa mkoa wa Tabora, alilazwa
hospitalini hapo tangu Septemba 11 mwaka huu.
Kwa
mujibu wa Katibu wa Hospitali ya Mkoa wa Kagera, Benges Justus, tukio hilo
lilitokea Septemba 16, mwaka huu, siku moja baada ya mgonjwa huyo kulazwa.
Alisema baada ya mwanafunzi huyo kupokelewa
hospitalini hapo, alifanyiwa vipimo vyote vya kitabibu na kugundulika
anasumbuliwa na malaria, ndipo akaanzishiwa tiba ya ugonjwa huo.
PINGAMIZI LA MWANASHERIA MKUU DHIDI YA TLS LATUPILIWA MBALI
Pingamizi
la Mwanasheria Mkuu (AG) dhidi ya ombi la kibali cha kufungua kesi ya kupinga
vikao vya Bunge Maalumu la Katiba vinavyoendelea mkoani Dodoma limetupiliwa
mbali katika
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es
Salaam.
Pingamizi hilo lilikuwa la
kupinga ombi lililowasilishwa na Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS)
waliofungua kesi ya kikatiba wakiomba mahakama itoe zuio la kuendelea kwa vikao
vya Bunge maalumu la katiba hadi kesi hiyo itakapokwisha.Aidha, wanaomba Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) awasilishe bungeni muswada wa marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba namba 8 ya mwaka 2011 na namba 2 ya
mwaka 2012, sura ya 83 na
ifafanue kifungu cha 25 cha sheria hiyo.
Uamuzi huo ulitolewa jana na
jopo la majaji watatu wanaosikiliza ombi hilo wakiongozwa na Jaji Augustine
Mwarija, Dk Fauz Twaib na Aloyisius Mujulizi.
Wakati huo huo, kesi nyingine
ya kikatiba iliyofunguliwa na Mwandishi wa Habari, Saidi Kubenea akihoji
mamlaka ya Bunge hilo inaanza kusikilizwa leo ambapo ilitakiwa ianze
kusikilizwa jana lakini AG aliwasilisha pingamizi ambalo pia litaendelea
kusikilizwa leo.
Katika kesi hiyo, Kubenea
anaiomba mahakama hiyo itoe tafsiri sahihi ya Mamlaka ya Bunge la Katiba, kwa
kuzingatia kifungu cha 25 (1) na (2) cha Sheria ya Mbadiliko ya Katiba namba 83
ya mwaka 2011.
Aidha, anaiomba mahakama
itamke kama bunge hilo lina mamlaka ya kubadilisha maudhui ya Rasimu ya Katiba
iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kwa kiwango gani.
WATAKA MFUKO WA NHIF UGHARIMIE NAULI ZA WAGONJWA
![](https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjcN-0h18eFCxAyh03cudgifc9QkBHuN39salJ_Jy-ZYFWvIGqDw_vfGxEdgePifasRLo9Tc0L1y8jt5vHIsGqRuCTYnmrYqlv1UuPtm2uWJadSQfksStQWpq9G_GiZHCQjAViiVHcYG-A/s1600/wataka.jpg)
Walisema
hayo walipozungumza wakati wa kikao cha pamoja baina ya wanachama wa mfuko huo
katika kijiji cha Mwamgongo, Kigoma Vijijini mkoani hapa na viongozi wa mkoa wa
mfuko huo.
Walisema
kuwa ni vizuri wanachama wanaokwenda kupata matibabu ya rufaa, wagharamiwe nauli na posho na mfuko huo.
Nassib
Ally, mtumishi katika Kituo cha Afya cha Mwamgongo, alisema licha ya sasa
malipo ya nauli na posho za safari kulipwa na mwajiri, lakini wakati mwingine
malipo hayo hayalipwi kwa wakati.
Alisema
hali hiyo huwafanya wanachama kuhangaika kufuatilia matibabu ya rufaa nje ya
vituo vyao vya kazi.
Mussa
Boniface, mwalimu wa Shule ya Msingi Mwamgongo, alitaka mfuko kugharamia huduma
za upimaji wa DNA na kugharamia huduma za matibabu ya nje ya nchi kwa wanachama
wake.
Akizungumzia
maombi hayo, Meneja wa NHIF mkoa wa Kigoma, Elius Odhiambo alisema kwa sasa
mfuko haugharamii malipo ya posho na nauli kwa wanachama wake, wanaokwenda
rufaa nje ya vituo vya kazi. Alieleza kwamba suala hilo litabaki kuwa juu ya
mwajiri.
Odhiambo
alisema kitendo cha kugharamia posho na nauli kwa wanachama, itawalazimu
wanachama hao kuchangia zaidi.
Alieleza
kwamba suala hilo linahitaji mjadala mrefu ambao utaridhiwa na wanachama wote
kuweza kutekeleza hilo.
Meneja
huyo pia alisema suala la maombi ya mfuko kugharamia matibabu ya nje ya nchi,
litabaki chini ya wizara ya afya huku upimaji wa vinasaba ukiendelea kuwa
gharama za mtu binafsi.
MBIO ZA MWENGE KUZINDUA MIRADI 72 MKOANI MWANZA
Miradi
72 ya maendeleo ya Sh bil. 23 inatarajiwa kuzinduliwa na Mwenge wa Uhuru,
utakaokimbizwa kwa siku nane mkoani hapa, ambao utapokelewa leo kutoka mkoa wa
Simiyu.
Hayo
yalielezwa jana na Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Evarist Ndikilo wakati akitoa
taarifa ya mwenge huo, iliyosomwa kwa niaba yake na Mratibu wa Mbio za mwenge
mkoani hapa, Diana Rwechungura.
Alisema
thamani hiyo inatokana na michango ya wananchi inayofikia zaidi ya Sh bil. 2.9,
Serikali Kuu Sh bil. 9.5, michango ya halmashauri Sh bil. 2.3 na michango ya
wahisani Sh bil. 8.1.
Alisema
miradi itakayozinduliwa katika mbio za Mwenge ni ya sekta za afya, kilimo,
ufugaji, maji na hifadhi ya mazingira.
Alisema ujumbe wa mwaka huu wa
Mwenge huo unasema ‘Katiba ni sheria kuu ya nchi, jitokeze kupiga kura ya maoni
tupate Katiba mpya’, ambao utaandamana na kaulimbiu za kudumu za mapambano
dhidi ya Ukimwi, rushwa, malaria na vita dhidi ya dawa za kulevya.
UTALII WACHANGIA SHILINGI TRILIONI 3 KWENYE PATO LA TAIFA
Sekta
ya Utalii nchini imekuwa ikichangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa, ambapo kwa
mwaka jana ilichangia dola bilioni 1.8 (Sh trilioni 3) katika pato hilo.
Kaimu
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Devota Mdachi alisema
hayo jijini Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu
Onesho la Kimataifa la Utalii (SITE).
Alisema
sekta hiyo imekuwa na mchango mkubwa. Alisema kutokana na ukuaji wake, wameamua
kuanzisha onesho hilo, ambalo litakuwa likifanyika kila mwaka.
“Kwa
mwaka huu maonesho hilo kubwa la kimataifa litafanyika kuanzia Oktoba mosi hadi
nne ambapo watakuwepo wageni kutoka nchi mbalimbali kwa lengo la kutangaza
utalii,” alisema.
Alisema
katika kufanikisha maonesho hayo, wamewashirikisha wadau mbalimbali, wakiwemo
TANAPA, Hifadhi ya Ngorongoro, Kampuni ya ndege ya Ethiopia, makampuni na
mashirika mengine, ambapo TTB imechangia Sh milioni 500 katika maandalizi hayo.
Alitoa
mwito kwa watanzania kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo ili kujifunza
utalii wa ndani na kujivunia vivutio vilivyopo na kutafuta soko kupitia
wadau walioalikwa katika maonesho hayo.
Mratibu
Mkuu wa maonesho hayo, Philip Chitaunga alisema lengo la maonesho hayo ni
kuwakutanisha watanzania na masoko ya nje na pia watawaleta wadau mbalimbali
wanaoandika habari za utalii na wadau wenye makampuni ya watalii.
Wageni hao pia watapata fursa ya kufanya
ziara kwenye vivutio mbalimbali, ikiwemo Zanzibar na Ngorongoro, ambapo kwa
watanzania itakuwa ni fursa kwa wenye makampuni ya watalii kujitangaza na
kutafuta soko.
WABUNIFU WA MAJENGO KUKUTANA LEO DAR
Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, leo anatarajiwa kuwa mgeni
rasmi katika ufunguzi wa mkutano wa 22 wa wataalamu wa wabunifu majengo na
wakadiriaji majenzi utakaofanyika kwa siku moja jijini Dar es Salaam.
Mbali na Mwinyi, alisema pia atakuwemo
Waziri wa Ujenzi Dk John Magufuli na wanafunzi kutoka shule mbalimbali za
sekondari.
Akizungumza na waandishi wa habari jana,
Msajili wa Bodi ya Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB), Jehad
Abdallah Jehad, alisema mkutano huo utakaohudhuriwa na washiriki wapatao 400,
mada kuu itakuwa sheria ya manunuzi namba 7 ya mwaka 2011 na athari zake katika
mazingira ya ujenzi.
Mwenyekiti wa AQRB, Ambwene Mwakyusa
alisema mategemeo yao ya baadaye katika mashindano hayo ni kuendelea
kuhamasisha wanafunzi kupenda masomo ya sayansi hususani taaluma za ubunifu na
ukadiriaji majenzi ili kukidhi pengo la upungufu uliopo ambapo hadi kufika
mwaka 2025 wanataka kuwa na wataalamu wa aina hiyo walau 6,500 kutoka 1,000
waliopo sasa.
HAWA NDIO WATAKAOCHEZESHA MECHI ZA LIGI KUU YA VODACOM
Ikiwa imebaki siku moja kufunguliwa kwa
pazia la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2014-15, mambo tayari yamenoga baada
ya kukamilika kwa safu ya waamuzi watakaochezesha mechi za ufunguzi wiki hii.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi
Tanzania, Silas Mwakibinga aliliambia gazeti hili jana, orodha ya waamuzi iko
tayari na kuwataka watakaochezesha katika michezo hiyo kutenda haki.
Katika mchezo wa Yanga dhidi ya Mtibwa
Sugar ya Mvomero, Morogoro, mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri
itachezeshwa na mwamuzi Dominick Nyamisano kutoka Dodoma.
Wakati huo, mabingwa watetezi, Azam FC
itakuwa mwenyeji wa Polisi ya Morogoro kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi,
Dar es Salaam katika mchezo utakaochezeshwa na mwamuzi Abdallah Kambuzi kutoka
Shinyanga.
Mwamuzi wa Dar es Salaam, Hashim Abdallah
atakuwa kwenye Uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga kuziamua timu mbili ngeni
katika ligi msimu huu, wenyeji Stand United na Ndanda FC ya Mtwara.
Mchezo mwingine utakuwa ni kati ya Mgambo
JKT ya Tanga dhidi ya Kagera Sugar ya Bukoba utakaochezwa kwenye Uwanja wa
Mkwakwani jijini Tanga na kuchezeshwa na mwamuzi Kennedy Mapunda wa Dar es
Salaam.
Aidha, Ruvu Shooting ya Pwani itacheza na
Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi na kuchezeshwa na
mwamuzi David Paulo wa Mtwara.
Washindi wa tatu wa ligi hiyo msimu
uliopita, Mbeya City itawakaribisha JKT Ruvu ya Pwani kwenye Uwanja wa Sokoine
jijini Mbeya katika mchezo utakaochezeshwa na Mohamed Theophil wa Morogoro.
Baada ya michezo hiyo ya Jumamosi katika mchezo
wa Jumapili, Simba watakuwa ni wenyeji wa Coastal Union ya Tanga kwenye Uwanja
wa Taifa, Dar es Salaam, na mwamuzi Jacob Adongo wa Mara atachezesha.
Kwa mujibu wa Mwakibinga, waamuzi hao wa
kati ni miongoni mwa waamuzi wa kati 21 watakaochezesha ligi hiyo iliyopangwa
kufikia tamati Aprili 18, mwakani. Kutakuwa na waamuzi wasaidizi 46.
Mwakibinga alisema anategemea waamuzi hao
watachezesha mchezo huo kwa kufuata sheria 17 za soka bila kupendelea na kwa haki.
“Hiyo ndio orodha ya kwanza, kuna nyingine
itatoka kwani wapo wengi, na wasaidizi wao tayari, tuna imani watazingatia
maadili ya kazi yao,” alisema Mwakibinga.
Thursday, September 11, 2014
RASIMU YA KATIBA MPYA KUPIGIWA KURA SEPTEMBA 21
Wakati kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi
(Ukawa) likishinikiza Bunge Maalumu la Katiba lisitishwe haraka iwezekanavyo,
Bunge hilo limejiandaa kuwasilisha Katiba inayopendekezwa Septemba 21.
Hatua hiyo ya
Bunge Maalumu, inalenga kuwapa fursa wajumbe wa bunge hilo, kuipigia kura
Katiba hiyo.
Spika wa
Bunge hilo, Samuel Sitta alisema hayo jana. Aliongeza kuwa hatua hiyo
itadhihirisha kuwa kazi waliyopewa na taifa ya kuandika Katiba mpya, itakuwa
imekamilika.
Hatua hiyo ya
Bunge kufupisha ratiba zake, inatokana na uamuzi wa Serikali kuwa shughuli zote
za bunge hilo, ziwe zimekoma ifikapo Oktoba 4 mwaka huu na sio Oktoba 31.
Sitta
abainisha kuwa majadiliano ndani ya Bunge hilo yatakamilika kesho kutwa
Jumamosi na kuanzia Jumatatu ijayo kamati ya uandishi wa katiba, itaendelea na
kazi yake ambayo wataifanya kwa wiki moja na baada ya hapo watawasilisha
rasimu Septemba 21.
Ratiba
inafafanua kuwa baada ya katiba inayopendekezwa kuwasilishwa, wabunge
wataipitia kabla ya kuanza kupiga kura Septemba 26 mwaka huu.
“Nafurahi kuwaambia kwamba jana katika kikao
cha kamati ya uongozi, tumedhihirisha kwamba tunakwenda vizuri na kamati ya
uandishi, ambayo imekuwa ikitazama mambo yanavyokwenda na mjadala ulivyoanza
jana, tumejipanga kutupa rasimu ya mwisho tarehe 21 mwezi huu.
“Kwa hiyo ni
dhahiri kabisa kwamba lengo tulilopewa na taifa la kutoa katiba inayopendekezwa
tutalimudu ndani ya wakati huo,” alisema Sitta.
Sitta alisema
kwa sasa uongozi wa Bunge hilo, unaangalia utaratibu wa kupiga kura kwa
wale ambao wako nje ya Bunge kwa sababu mbalimbali ukiacha wale ambao walisusa
hasa wale ambao wako hospitali, ambao kanuni zinawaongoza utakapofika wakati wa
kupiga kura, waandaliwe utaratibu wa kufanya hivyo.
Alisema
wanafanya hivyo, kwa sababu akidi inahusu wabunge wote, ambao waliteuliwa na rais
kuwa wajumbe wa Bunge hilo na wajumbe wengine ambao wameingia kwa nyadhifa zao.
Upigaji kura
huo, pia utawahusisha wajumbe wa Bunge hilo ambao watakuwa safari nje ya nchi.
Baadhi ya wajumbe wanaenda Hijja huko Mecca, Saudi Arabia.
Katika
kuhakikisha kuwa wajumbe wengi wanachangia ndani ya muda ambao wamepewa,
uongozi wa Bunge hilo ulitoa mwongozo wa namna ya kuchangia na Sitta aliwataka
wajumbe kuhakikisha wanafuata muongozo huo ili kuokoa wakati.
“Jana kidogo
tuliongelea lakini leo mtaona kuna muongozo tumeugawa, kila mmoja ahakikishe
anao kwa sababu kiti kitaangalia tunakaa ndani ya muongozo huo, kwa leo nadhani
na kesho kwa sababu mjadala tuukamilishe kufikia siku ya Jumamosi hii
inayokuja, kwa hiyo tutakuwa tunagawa miongozo hii kuwawezesha waheshimiwa
wajumbe kujua tunalenga wapi,” alisema Sitta.
Mwongozo
alioutoa jana ulihusu Sura ya 2,3,4,5 ambao uliandaliwa na sekretarieti.
Alisema mwongozo huo ni muhtsari wa maoni, ambayo yalitoka ndani ya
kamati zote 12. Alisema kwa hali hiyo mwenendo huo, hautaruhusu kuibua upya
mjadala uliokuwapo ndani ya kamati.
Sitta
alifafanua kuwa kuna masuala mbalimbali ambayo rasimu ilisema na muhtasari
kamati zilijielekeza na kufikia muafaka na sehemu hawakufikia muafaka.
Aliwakumbusha wajumbe hao kuwa ni kazi yao sasa kuboresha yale yaliyopo
kwenye mwongozo huo.
Sitta alisema
kuhusu mambo ya imani ya dini, kamati kadhaa zilisema ibara hiyo ibaki kama
ilivyo kwenye rasimu ya katiba na nyingine zikaongezea kwamba uwepo
utaratibu wa kutambua na kuruhusu sheria na vyombo vya dini, kutambuliwa
kisheria.
“Sasa mjadala
wa jana ulifikia mahali kwamba kidogo uharibu mambo kwa sababu tumerejea tena
kuidai mahakama ya kadhi ndani ya katiba na wengine wanasema ndivyo ilivyo
Uganda wakati sio kweli, Zanzibar sio kweli mahakama kama hiyo inatambuliwa
ndani ya sheria, sio lazima ndani ya katiba.
“Tunachotunga hapa ni kuandika katiba, sio
sheria na kwa suala hili hapa kwa Tanzania Bara Kamati ya Pamoja ambayo
inasimamiwa na waziri mkuu imekuwa ikilishughulikia ili lifike mwisho wake, kwa
hiyo kulirejea tena na kusema kwamba ni jambo ambalo linazungumzwa ndani
ya katiba sio sahihi,” alisema Sitta.
Kwa hali hiyo
aliwaomba wajumbe, kuhakikisha kuwa hawarudii tena yale waliyoyajadili kwenye
kamati. Alisema kama hoja ilishindikana na ikawekwa pembeni, kutokana na
wajumbe kutofikia muafaka fulani; sio wakati wa kurejesha jambo hilo ndani ya
Bunge, kwani kufanya hivyo ni kuanzisha upya mjadala wakati kazi yao kwa
sasa ni kuboresha kile ambacho kinaweza kuleta muafaka.
Kutokana na
msimamo huo wa Sitta, baadhi ya wajumbe walimpinga na mjumbe wa kwanza kufanya
hivyo, alikuwa ni Ezekiah Oluoch aliyetaka apewe mwongozo, kwa sababu kuna
kifungu cha kanuni kinachotoa fursa kwa mjumbe yeyote wakati wa mjadala,
kuwasilisha marekebisho na maboresho au mabadiliko, ikiwa ni marekebisho
madogo, ambayo hayabadilishi msingi au maana.
“Kwa hiyo
mheshimiwa mwenyekiti tukiendelea tu na haya ambayo yamewekwa na kamati na
tusiongezee vingine, tutakuwa na shida kwa sababu tayari ulishapokea malalamiko
kwamba baadhi ya kamati hawakuweka hata vile vifungu, ambavyo vilikuwa
vimekubalika, kwa hiyo nilikuwa naomba nipate muongozo kwamba kwa nini hiyo
haki mjumbe asiitumie iliyopo kwenye rasimu na badala yake tutumie muongozo
tuliogaiwa asubuhi ya leo?” alihoji Oluoch.
Akijibu hoja
hiyo, Sitta alisema hilo ni jambo ambalo lipo wazi. Alionya kuwa taratibu wa
kuleta mabadiliko ni kitu kimoja, ambacho kitafumbua mjadala upya.
Alisema
mjadala huo ni kitu kingine na mambo yaliyokuwa ndani ya kamati ni kitu
kingine. Alisema yeye anajielekeza kwenye hilo la pili kuanzisha mjadala,
ambao tayari kwenye kamati walishazungumza.
Mwenyekiti
huyo alisema fursa za kuleta mabadiliko kwa maandishi, zinabaki palepale na
hata hatua ya kusoma ile rasimu kamili kuanzia ibara ya kwanza hadi ya mwisho,
ipo pale pale kwa mjumbe kuweza kupeleka pendekezo la mabadiliko ambalo
linaweza kupigiwa kura.
“Kwa hiyo
mimi sioni kama hayo mambo mawili yanapishana, hata kidogo, kuna kanuni za
mjadala ambazo lazima tuzizingatie, hatuwezi kurudia kazi tulizofanya kwenye
kamati kwa takribani wiki tatu tukairejesha kwenye mjadala, lakini kuleta
mapendekezo ya mabadiliko inaruhusiwa,” alisema.
Waziri katika
ofisi ya Rais asiyekuwa na Wizara Maalumu, Profesa Mark Mwandosya alionya kuwa
wajumbe walioko nje ya Bunge, ambao wanatarajia kuwa kuna katiba nyingine
itaandikwa baada ya mwaka 2015, wamechelewa.
Alisema
propaganda wanayoiendesha nje ya Bunge hilo kuwa mchakato huo utaanza
upya, hauna tija. Aliwahakikishia wananchi kuwa wajumbe wa bunge hilo,
wamefanya kazi kwa weledi mkubwa na watawapatia wananchi katiba mpya.
Wakati huo
huo, viongozi wa Ukawa waliitisha
mkutano na waandishi wa habari, Dar es Salaam
jana na kuendelea kumshinikiza Rais Jakaya Kikwete, atoe agizo mara moja
la kusitishwa kwa vikao vinavyoendelea vya Bunge Maalum la Katiba.
Aidha umoja
huo umependekeza katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2013, ifanyiwe
marekebisho na kuwekwa kipengele kitakachotoa amri kwa utawala ujao,
kuhakikisha unamalizia mchakato wa Katiba uliositishwa kwa kuendelea na hatua
ya Bunge la Katiba.
Mwenyekiti
Mwenza wa umoja huo, James Mbatia alisema katika mazungumzo yaliyofanyika hivi
karibuni kati yao na Rais Kikwete, walikubaliana mchakato huo wa Katiba kwa
sasa usitishwe.
“Tumeshakubaliana
kimsingi kwamba mchakato huu wa Katiba hautaweza kufikia hatua ya mwisho kwa
wakati huu ya uchaguzi, muda umekwenda sana na makubaliano hayo tumetiliana
saini wote hadi wenzetu wa CCM, ila tunashangaa kwanini Bunge hilo hadi sasa
linaendelea tena hadi Oktoba 4, haya ni matumizi mabaya ya fedha za umma,”
alisisitiza Mbatia.
Alisema
katika makubaliano waliyoyafikia kwenye vikao hivyo, vilivyofanyika Agosti 31
na Septemba 8, mwaka huu, yalizingatia maoni ya wadau na kukubaliana kwa pamoja
kuahirisha mchakato wa katiba ili kupisha maandalizi ya Bunge la kawaida.
“Hata hivyo,
pamoja na makubaliano haya, sisi kama Ukawa msimamo wetu ni Bunge linaloendelea
la Katiba lisitishwe ili tuanze kufanyia marekebisho Katiba ya sasa tuweze
kufanya uchaguzi kwa maridhiano na amani,” alisema.
Alimpongeza
Rais Kikwete kwa kuchukua uamuzi wa kukubali kukutana na umoja huo kwa
mashauriano hadi kufanikisha, hatua hiyo
aliyoiita nzuri ya kuwezesha kupata muafaka wenye maslahi mapana kwa taifa,
kuhusu suala la katiba na uchaguzi.
Katibu Mkuu
wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, alimtaka Sitta kuacha kutumia vibaya fedha za
umma na kusitisha mara moja Bunge hilo, vinginevyo kukitokea machafuko au
vurugu zinazotokana na mchakato huo wa Katiba atalaumiwa yeye.
Mwenyekiti
Mwenza wa Umoja huo kutoka CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema katika
marekebisho ya 15 ya Katiba ya sasa, walichopendekeza ni kuundwa kwa tume huru
ya uchaguzi, kuweka mgombea huru, Rais kuchaguliwa kwa zaidi ya asilimia 50 na
matokeo ya Urais kuhojiwa mahakamani.
Mwenyekiti wa
Chadema na Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, Freeman Mbowe, wakati akifungua uchaguzi
wa Baraza la Vijana wa chama hicho Dar es Salaam jana, alisisitiza juu ya Bunge
hilo kusitishwa mara moja kabla ya Oktoba 4, mwaka huu, vinginevyo wataingia
barabarani.
Subscribe to:
Posts (Atom)