Sunday, August 31, 2014

BINTI MDOGO KUTOKA MTWARA ASHINDA SHILINGI MILIONI 50 SHINDANO LA TMT



Mshiriki kutoka Mtwara, Mwanaafa Mwinzago ameibuka kidedea katika Shindano la Tanzania Movie Talents (TMT) lililofanyika usiku wa kuamkia leo kwenye Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.
Katika shindano hilo ambalo washiriki 10 walikuwa wakizitolea macho Shilingi milioni 50, Mwanaafa aliweza kuzoa kura nyingi zaidi na hivyo kujiwekea kibindoni mamilioni hayo na kuwatimulia vumbi washiriki wengine.
Awali kabla ya kutangazwa mshindi, Mwenyekiti wa Kampuni ya Proin Promotions, Johnson Lukaza alitoa ahadi kwamba kampuni hiyo itajitolea kumsomesha mtoto Mwanaafa ili aweze kufanikiwa kufikia malengo yake.
Mwanaafa ndiye mshiriki mdogo kuliko wote katika shindano hilo lililoandaliwa na Proin Promotions ambapo miongoni mwa majaji watatu, wawili walikuwa waigizaji maarufu nchini, Single Mtambalike ‘Ritchie Rich’ na Yvonne Cherie ‘Monalisa’. Jaji Mkuu alikuwa Roy Sarungi.
Mara baada ya kutangazwa mshindi, Mwanaafa aliangua kilio cha furaha kuonesha kutoamini kwamba amefanikiwa kunyakua mamilioni hayo huku akihaha huku na kule kumtafuta mama yake jukwaani.
Hata baada ya kuitwa na kukabidhiwa hundi ya Shilingi milioni 50 na Mwenyekiti wa Proin Promotions, Mwanaafa aliendelea kububujikwa machozi ya furaha kuonesha kabisa kutoamini kinachotokea usiku huo.

Saturday, August 30, 2014

MAJAMBAZI WATANO WAUAWA KWA KUZAMISHWA KWENYE MAJI


Watu watano wanaosadikiwa kuwa majambazi, wamepigwa kwa mawe hadi kufa wakijaribu kutoroka nguvu za umma kwa kutumia Mto Mara, wilayani Tarime huku wakiwa na bunduki mbili zinazotumika vitani aina ya sub machine gun (SMG). 
Tukio hilo lilithibitishwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Tarime/Rorya, Lazaro Mambosasa. 
Kamanda Mambosasa alisema watu waliouawa katika tukio hilo la juzi mchana hawajafahamika kwa majina wala uraia wao. 
Hata hivyo alisema siku ya tukio, majambazi hao wakiwa na silaha za kivita, walionekana wamejificha vichaka karibu na makazi ya wananchi wa kitongoji cha Nyabirongo, kijiji cha Gibaso katika Kata ya Nyarukoba, Tarafa ya Ingwe iliyopo jirani na hifadhi ya Serengeti. 
Lakini baada ya kushitukiwa, walizingirwa na wananchi wenye silaha za jadi zikiwemo mawe, marungu na mapanga huku wakipiga mayowe ambapo majambazi hao walijibu kwa kurusha risasi hovyo ili wananchi wasiwakaribie. 
Wakati wakirusha risasi hizo zilimjeruhi mwananchi mmoja, Kagore Paul begani, na kuwaongezea hasira wananchi walioendelea kuwasakama katika eneo walilojificha. 
Mayowe waliyopiga yaliwaleta watu wengi zaidi muda ulivyokuwa unakwenda kiasi cha majambazi hao kuzidiwa na  kuamua kukimbia kwa kupitia Mto Mara, ili waende upande wa pili wa wilaya ya Serengeti. 
Kamanda anasema: "Wakazi wa kijiji hicho na vijiji jirani walijitokeza kwa wingi kwani ilikuwa mchana na kupambana na watu hao huku wakikimbilia mto Mara kutaka kuvuka mto huo  kwenda  wilaya ya Serengeti kuingia mbugani, lakini juhudi zao za kutaka kuvuka hazikifanikiwa. 
“Wananchi wa vijiji vya upande wa pili Wilaya ya Serengeti nao walijitokeza na kuziba njia hali iliyowalazimu watuhumiwa kuingia mtoni na kutaka kuogelea huku wakitupa silaha walizokuwa nazo majini  na hapo ndipo walipopigwa mawe na marungu wakiwa majini na kufa. 
“Jeshi letu la Polisi lilifika na kusaidia kuopoa miili ya watu hao watano ambapo mmoja alikutwa na risasi 11 mfukoni na mwingine alikutwa na risasi nne na fedha za Kenya Sh 350 (sawa na fedha za Tanzania sh 7,000) ambapo inasadikiwa huenda watuhumiwa wakawa raia wa nchi jirani ya Kenya.” 
Kwa sasa, miili ya watu hao imehifadhiwa katika chumba cha maiti cha Hospitali ya Wilaya Tarime huku jeshi la polisi likiendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo. 
Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya Tarime, Dk Bernard Makonyu amethibitisha kupokea miili ya watu watano iliyofikishwa hospitali hapo na gari la polisi huku matumbo ya marehemu yakionekana kuvimba kutokana na kunywa maji mengi kabla ya kufikwa na mauti. 
Hilo ni tukio la pili katika kipindi cha wiki tatu ambapo Agosti 3 mwaka huu watu wanne, wakiwemo raia watatu wa Kenya na Mtanzania mmoja waliuawa kutokana na matukio ya ujambazi katika kijiji cha Mriba.

MAKUBWA YAIBUKA UTAFITI WA NGONO ZA UTOTONI DAR



Sampuli tathmini ya matokeo ya mradi wa PREPARE uliokuwa na lengo la kuangalia uwezekano wa vijana kupunguza ngono, imebainisha haja ya elimu ya afya ya uzazi kukabili hali ya sasa ya tabia hatarishi zinazowakabili vijana wadogo.
Matokeo ya awali ya mradi yalionesha kuwa asilimia 10 ya vijana wenye umri wa miaka 12 mpaka 14 ambao ni darasa la tano na sita waliofanyiwa utafiti walikuwa wameshawahi kufanya ngono na asilimia kubwa ikiwa ni kwa kutumia njia ya haja kubwa.
Kauli hiyo imetolewa na mmoja wa watafiti wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi shirikishi cha Muhimbili, Kitengo cha magonjwa na afya ya akili, Lusajo Kajula.
“Vijana wengi walionekana wakifanya ngono ya uke na ya mdomo ikifuatiwa na ngono ya njia ya haja kubwa kwa wale ambao wameshawahi kufanya ngono, asilimia 6.3 wamefanya ngono ya njia ya haja kubwa wakati asilimia 93.7 hawajawahi.”
Aidha alisema utumiaji wa kondomu ulionekana kuwa mdogo kwa vijana wadogo ambao wameanza kufanya ngono.
“Asilimia 68 ya wale walioanza kufanya ngono hawajawahi kutumia kondomu kabisa wakati asilimia 32 wamewahi kutumia kondomu.”
Alisema utafiti huo ni sehemu ya utafiti wa miaka minne ulioshirikisha Vyuo Vikuu vya Makerere cha Uganda, Cape Town na Limpopo vya Afrika Kusini, Bergen na Oslo vya Norway, Maastricht cha Uholanzi na Sussex cha  nchini Uingereza.
Alisema utafiti umeonesha haja ya kutolewa elimu ya afya ya uzazi kwa vijana wadogo ambao hawajaanza ngono ili kuchelewesha kuanza ngono kwa mfumo wa kisaikolojia ili waweze kujitambua na kuacha kufuata nadharia za kisayansi pekee ambazo ndizo zinazotumika katika shule mbalimbali kuwaeleza mabadiliko ya miili yao.
Katika utekelezaji wa utafiti huo, idadi ya wanafunzi 5,099 walichaguliwa mwanzoni mwa mradi kufanyiwa utafiti huo ambapo wanafunzi 4,783 (asilimia 93.9) walifuatiliwa kwa miezi 6 na wengine 4,370 (asilimia 85.8) walifuatiliwa kwa miezi 12.
Utafiti ulionesha elimu inayojishughulisha na masuala ya jinsia na afya ya uzazi kwa vijana wadogo itumie mtazamo mpana utakaoleta mabadiliko ya msingi kwenye misingi ya virekebisho vya mabadiliko ya tabia.
Mradi huo wa PREPARE ulitekelezwa kwenye shule 38 kutoka manispaa ya Kinondoni zilizochaguliwa kwa kutumia taratibu sampuli mtawanyiko zilizopangwa katika makundi mawili ya shule za mwingilio yaani ilikotolewa elimu hiyo zilizokuwa 19 na za kulinganisha zilizokuwa 19.
Ili kuweza kupata matokeo yaliyokusudiwa mradi ulitoa mafunzo kwa walimu watano wakufunzi wa wakufunzi; ulitoa mafunzo kwa walimu watekelezaji 76,  na waelimishaji rika wanafunzi 132 na kuelekeza watoa huduma 8 wa afya katika kliniki za huduma rafiki kwa vijana ili kutekeleza muingiliano.
Tathmini iliyotoa majibu ya jinsi utendaji unavyoendelea na ya matokeo ilihusisha shule zote na wanafunzi zaidi ya 6,000 waliowekwa kwenye muingiliano, huku uchambuzi wa tathmini ukihusisha wanafunzi wenye umri wa miaka 12-14, wenye kujua kusoma na kuandika.
Matokeo yaliyotathminiwa ni mabadiliko katika masuala ya ngono (kuanza ngono) na kutumia kondomu wakati wa  kujamiiana kwa wale waliokwisha anza ngono.
Kwa wastani mradi uliona kwamba mwingilio wa PREPARE ulipunguza uwezekano wa vijana wadogo (wavulana  na wasichana) kuanza ngono na kuongeza uwezekano wa kutumia kondomu kwa wale walioanza. 
Hata hivyo, katika utekelezaji wa mradi mabadiliko katika uchukuaji wa hatua yalionekana zaidi miongoni mwa wasichana waliopata mwingilio ukilinganisha na wale ambao hawakupata mwingilio. 
Uchukuaji wa hatua ulisababisha tabia ya kutumia kondomu miongoni mwa wanafunzi wa kiume, lakini siyo miongoni mwa wanafunzi wa kike. 
“Kimsingi tunataka kuwaambia wanahabari kuwa miongoni mwa  mafanikio makubwa ya mradi wa PREPARE  ni kuchelewesha kuanza ngono miongoni mwa wanafunzi wa kiume na wa kike wenye umri wa miaka 12-14 katika mkoa wa Dar es Salaam, Tanzania; 
“Kuongeza uchukuaji wa hatua ulio chanya katika kutumia kondomu kwa jinsia zote na taarifa za ongezeko la utumiaji wa kondomu miongoni mwa vijana wa kiume. “ 
Mradi huu uliofadhiliwa na Umoja wa Nchi za Ulaya, Programu ya utafiti wa afya umelenga kuangalia mwingiliano ulio katika misingi ya utamaduni na jinsia, endelevu, kijamii ili kukuza ujinsia na afya ya uzazi miongoni mwa vijana wenye umri kati ya miaka 12-14 kwa kutumia shule kama njia ya kufundishia.

WATU 10 WAFARIKI MBEYA BAADA YA HIACE YAJIBAMIZA KWENYE FUSO



Watu kumi akiwemo mama na mtoto wake  wamekufa papo hapo na wengine wanane kujeruhiwa baada ya gari aina ya Toyota Hiace waliyokuwa wanasafiria kugongana na lori katika mji mdogo wa Mbalizi, Wilaya  ya Mbeya Vijijini.
Ajali hiyo imetokea majira ya saa 6:00 mchana  imehusisha gari aina ya Toyota Hiace lililokuwa likitokea Jijini Mbeya na Fuso lililokuwa likitokea katika kituo cha mafuta na kuingia barabara kuu ya kutoka Mbeya kwenda Tunduma.
Akizungumzia ajali hiyo, Muuguzi Mkuu wa Hospitali teule ya wilaya ya Mbeya, Sikitu Mbilinyi alisema kuwa wamepokea  maiti 10 wakiwemo wanawake wanne, wanaume  wanne na watoto wawili.
Alisema katika majeruhi wanane waliopokelewa hospitalini hapo, watano ni  wanaume na watatu ni wanawake na kwamba madaktari baada ya kubaini hali za majeruhi hao kuwa mbaya walishauri wapelekwe katika hospitali ya rufaa Mbeya .Tayari majeruhi watatu akiwemo mwanamke mmoja wamehamishiwa katika hospitali hiyo.
Aliwataja waliokufa katika ajali hiyo  ambao  wametambuliwa na ndugu zao kuwa ni pamoja na Mariam Mashambwe na mtoto wake Hamis Chaula, Rebeca Keneth, Petro mgogo, Haruna Jamison na Martin Mwasolikoto.
Aliwataja majeruhi waliofikishwa hospitalini hapo na kulazwa kuwa ni pamoja na kondakta  wa Hiace, Justin Chaula(28)mkazi wa Mabatini, kondakta wa lori Joseph Stephano (22)  mkazi wa Mbalizi , aliyekuwa abiria wa roli Ziona Goa  (20), Newton Patrick na dereva wa lori,  Amoni Mwakoko.
Mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo,  Ziona Goa alisema kuwa Hiace waliyokuwa wamepanda ilikuwa na hitilafu katika breki na kusababisha gari kwenda kwa mwendo wa kasi na dereva kushindwa kulidhibiti na kuligonga lori ambalo tayari lilikuwa limeingia barabarani.
“Tulimsikia dereva akisema breki hazifanyi kazi huku gari likiwa kwenye mwendo kasi na ghafla mbele yetu kukawa na lori limekwisha ingia barabarani na tukaligonga ubavuni,” alisema.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba uchunguzi wa ajali hiyo unaendelea ili kubaini  chanzo cha ajali  hiyo.