Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imetoa
hati ya kukamatwa kwa Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma anayekabiliwa na kesi ya kupokea Sh
milioni 323.4, kwa kuwa hajafika mahakamani.
Aidha imetoa hati kwa wadhamini wa
Mujunangoma kufika mahakamani kujieleza kwa nini wasichukuliwe hatua kutokana
na kitendo chao na mshitakiwa kutofika mahakamani.
Hakimu Mkazi Emmilius Mchauru
alitoa hati hizo jana wakati kesi hiyo ilipotajwa kwa ajili ya kusikiliza
pingamizi, lililowasilishwa na upande wa utetezi.
Awali, Wakili kutoka Taasisi ya Kuzuia
na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai aliiomba mahakama kutoa hati
hizo kwa kuwa mshitakiwa na wadhamini wake hawajafika mahakamani bila kutoa
taarifa.
Hakimu alikubali ombi hilo na
kuahirisha kesi hiyo hadi Mei 4, mwaka huu, kesi itakapotajwa tena. Mujunangoma
anadaiwa kupokea rushwa ya Sh milioni 323.4 kutoka kwa Mkurugenzi wa VIP
Engineering and Marketing, James Rugemalira.
Kwa mujibu wa taarifa
zilizopatikana nje ya mahakama kutoka kwa watu wanaodai ni ndugu wa mshitakiwa,
Mujunangoma alipata shinikizo la damu akiwa njiani kuja mahakamani hivyo
alipelekwa katika Hospitali ya Arafa, Tabata, na kulazwa.
Ilidaiwa kuwa walitoa taarifa kwa
mdhamini ili afike mahakamani kutoa taarifa lakini alichelewa na kukuta kesi
imeshatajwa na hati hizo zimetolewa.
Mujunangoma anadaiwa Februari 5,
2014 katika Jengo la Benki ya Mkombozi, alipokea rushwa ya Sh milioni 323.4
kutoka kwa mmiliki wa Kampuni ya kufua Umeme ya VIP Engineering and Marketing
ambaye pia alikuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya IPTL, James Rugemalira.
Inadaiwa Mujunangoma, alipokea
fedha hizo kupitia akaunti 00120102602001 kama tuzo baada ya kushughulikia
masuala ya Kampuni ya IPTL kama mfilisi, bila kumtaarifu mkuu wake wa kazi
ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Tume
ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
No comments:
Post a Comment