Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda ametoa ufafanuzi kuhusu suala la uandikishaji katika daftari la
kudumu la wapigakura na siku maalum ya kupiga kura.
Amebainisha
kuwa kutokana na hali ilivyo, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ndio itakayotoa
ratiba kamili kuhusu hatma ya upigaji kura ya maoni.
Aidha, katika
mgogoro na mgomo wa wafanyabiashara unaoendelea, amewataka wafungue maduka yao
kwa kuwa tayari Serikali imeanza kushughulikia na kuyafanyia kazi malalamiko
yao.
Akizungumza
bungeni jana wakati wa kuhitimisha shughuli za mkutano wa 19 wa Bunge, alisema
Serikali inatambua kuwa muda uliobaki kufikia siku ya kupiga kura ni mfupi,
lakini Tume ndiyo yenye mamlaka kwa sasa ya kutoa ratiba kamili kuhusu tukio
hilo.
“Tunatarajia
Tume itatoa taarifa ya Ratiba itakayotumika kutuwezesha kukamilisha zoezi la
uandikishaji pamoja na kutoa taarifa siku za hivi karibuni kuhusu upigaji wa
Kura ya Maoni. Ni dhahiri muda uliobaki
kuanzia sasa ni mfupi lakini Tume ndiyo itakayotujulisha ratiba kamili,”
alisisitiza.
Alisema
Serikali kwa upande wake, imehakikisha fedha yote kwa ajili ya ununuzi wa BVR
8,000 zimelipwa kwa NEC na matarajio ni
kwamba kazi ya kuandikisha katika mikoa mingine itaanza na kuendelea kwa kasi.
Pia, alisema
wakati tume inajitahidi kufikia malengo
hayo, Serikali inaendelea na mipango ya kuelimisha wananchi kupitia redio, televisheni, magazeti mbalimbali
kuhusu umuhimu wa Katiba inayopendekezwa ili kila mwananchi aielewe vizuri na
kuweza kuipigia kura kwa matakwa yake mwenyewe bila kurubuniwa muda
utakapofika.
Alisema tume
hiyo imelenga kuandikisha wapiga kura milioni 21 na inakadiriwa kutakuwa na
vituo 36,164, kila kituo kitaandikisha kwa siku saba hadi 11 kutokana na idadi
ya watu na vituo vitafunguliwa kuanzia saa mbili hadi saa 12 jioni.
Akizungumzia
suala la mgogoro wa wafanyabiashara Pinda, alisema katika kushughulikia suala
hilo, Serikali ilikutana na wafanyabiashara hao na kukubaliana kuwa kwa sababu
Serikali imeonesha nia ya kushughulikia malalamiko na changamoto zinazowakabili
wafanyabiashara nchini ni mgomo huo ukasitishwa.
“Serikali
inathamini sana mchango wa wafanyabiashara katika kukuza Uchumi na kuchangia
mapato ya Serikali. Napenda kuwahakikishia wafanyabiashara na wananchi wote
kwamba, Serikali ipo tayari kukaa pamoja na wafanyabiashara kuzungumzia
changamoto zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi wa haraka,” alisisitiza.
Akizungumzia
suala la mauaji ya watu wenye ulemavu (albino), alisema itaendelea kuchukua
hatua mbalimbali za kiuchunguzi na kiupelelezi na kuwakamata wote wanaohusika
na mauaji hayo yaliyojirudia tena nchini na kuwachukulia hatua za kisheria.
Alisema kwa
sasa jumla ya watuhumiwa 181, wakiwemo Wanaume 171 na Wanawake 10 walikamatwa
na kuhojiwa, kati yao watuhumiwa 133 walifikishwa mahakamani na kufunguliwa
kesi za mauaji na 46 kwa makosa ya
kujeruhi.
“Chanzo kikubwa cha mauaji hayo ni imani za
kishirikina. Aidha, Matukio 41 kati ya 43 yametokea katika Ukanda wa Ziwa na
Magharibi, kwani hadi sasa yametokea matukio 13 ya Mauaji Mwanza, Kagera
matukio sita (6), Tabora matukio matano (5), Mara matukio manne (4), Geita
matukio manne (4), Kigoma matukio Manne (4) Simiyu matukio matatu (3) na
Shinyanga matukio mawili (2)” alisisitiza.
Kuhusu
Mahakama ya Kadhi, alisema katika Mkutano wa 18 wa Bunge Serikali ilikusudia
kuwasilisha bungeni Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali na sehemu ya
tano ya muswada huo, ilikusudia kurekebisha Sheria ya Tamko la Sheria za
Kiislamu.
Alisema
muswada huo ni miongoni mwa Miswada minne ambayo haikupata nafasi ya kujadiliwa
na Bunge. “Serikali itatumia fursa kuendelea kushirikisha wadau mbalimbali kwa
lengo la kupanua uelewa juu ya maudhui na madhumuni ya Muswada huu”.
Pia, Waziri
Mkuu alitoa pole kwa ajali zilizotokea na maafa yaliyotokana na mvua katika
mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara na Kahama mkoani Shinyanga.
Spika wa
Bunge, Anne Makinda, alilazimika kuvunja kikao cha asubuhi cha Bunge majira saa
nne, baada ya wabunge wa vyama vya siasa vya upinzani kugoma mijadala mingine
isiendelee hadi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, atakapotoa kauli juu ya mustakabali
wa uandikishwaji wapiga kura na hatima ya kura ya maoni.
Wabunge
hao, pamoja na kujibiwa na Spika kuwa suala hilo, litatolewa maamuzi wakati
Waziri Mkuu akihitimisha hoja ya kuahirisha Bunge, waligoma kukaa na wote
wakasimama bungeni, na kuanza kuimba wakiwa wamewasha vipaza sauti huku
wakigonga meza wakitaka hoja yao ijibiwe kwanza.
Chanzo cha
vurugu kilianza pale, Mbunge wa Kisarawe Selemani Jafo (CCM), alipoomba
mwongozo wa Spika, akitaka Bunge hilo lisitishe shughuli zilizopangwa na
kujadili suala la kura ya maoni na namna ya kutengeneza Katiba ya mpito kwa
ajili ya uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Katika hoja
yake hiyo, Jafo alisema kutokana na hali ilivyo ya uandikishaji katika daftari
la kudumu la wapiga kura, ni wazi kura ya maoni haiwezi kufanyika Aprili 30,
kama ilivypangwa.
Alisema ni
wakati sasa Bunge hilo, lianze kujadili vipengele kama vile mgombea binafsi,
kupinga matokeo ya urais mahakamani, kuwepo kwa tume huru ya uchaguzi na umri
wa wabunge na Bunge ili viingizwe na kupitishwa kwenye kikao cha 20 cha Bunge
ili Katiba ya Mpito ipitishwe.
Wakati Jafo
akitoa maelezo yake kuhusu mwongozo huo, baadhi ya wabunge wa upinzani walikuwa
wamesha vipaza sauti wakimpinga kwa madai kuwa, suala analotaka siyo la dharura.
Baada ya
maelezo hayo ya Jafo, mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) naye aliomba
mwongozo kwa kanuni ya 47 (1) inayohusu kusimamisha shughuli za Bunge
zilizopangwa kwa siku hiyo ili jambo la dharura lijadiliwe.
“Mheshimiwa
Spika uandikishaji wapiga kura nchi nzima, haujakamilika hata katika mkoa wa
Njombe, Watanzania wapo katika sintofahamu ni lini wataandikishwa kwenye
daftari la kudumu la wapiga kura,” alisema.
Alisema
suala hilo ni la dharura na lilishaombewa miongozo zaidi ya mara moja bila majibu,
hivyo si vyema Bunge hilo likaahirishwa bila kupatiwa majibu juu ya hatma ya
uandikishaji huo wa wapiga kura na kura ya maoni.
“Tusitishe
shughuli zote tuhakikishe tunajali, majibu yapatikane leo katika mkutano huu wa
Bunge, nimeomba miongozo juu ya jambo hili mara mbili na mara zote Serikali
haitoi majibu, sasa hakieleweki hapa hadi tupatiwe majibu,” alisema Mnyika.
Alisema
“Waziri Mkuu yupo hapa anaweza kutoa majibu hapa na tukajadili jambo hili
hapa,” alisema Mnyika.
Baada ya
Mnyika kumaliza kuomba Mwongozo, Spika Makinda alibainisha kuwa hoja hiyo ya
Mnyika haina tofauti na Jafo, na zote zipatiwa majibu na Waziri Mkuu wakati akitoa
hoja ya kuahirisha Bunge.
Hata hivyo,
jibu hilo la Spika halikukubaliwa na wabunge hao wa upinzani na ndipo mbunge wa
Kasulu Mjini, Moses Machali, alipowasha kipaza sauti bila ruhusa ya Spika na
kusema “Hoja hii haifanani na hoja ya
kwanza, ile ya kwanza inataka majibu mkutano wa 20 na hoja hii ya pili inataka
majibu mkutano huu.”
Wabunge
wote wa upinzani wa vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi na CUF, walisimama na
kuwasha vipaza sauti huku wakiongea kwa nguvu kuwa hoja hizo hazifanani na ni
lazima hoja yao ipatiwe majibu kabla ya shughuli nyingine za Bunge kuendelea.
Machali
alidakia tena na kusema, “Tunataka majibu, tumechoka kuburuzwa.”
Spika
Makinda aliwajibu kwa kusema “Anawaburuza nani, nimewaambia kwamba swali lile litajibiwa leo
(jana),au njooni basi nyie muendeshe hiki kikao, kama hamtaki kukubali majibu
yangu tokeni nje.”
Huku
wabunge hao wakiwa bado wamesimama na kuimba kuwa wanataka majibu, Spika
alimwita Msemaji Kambi ya Upinzani kwenye Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na
Teknolojia, ili asome maoni ya kambi hiyo juu ya Mswada wa Sheria ya Miamala ya
Kielektroniki ya mwaka 2014 na ule wa Makosa ya Kimtandao wa mwaka 2015, lakini
hakutoka.
Aidha Spika
aliendelea na kumtaka Katibu ataje shughuli inayofuata, ambaye aliisoma kwa
mara ya kwanza Miswada ya Shera ya Kupata Habari wa mwaka 2015, wa Sheria
Vyombo vya Habari wa mwaka 2015, wa Sheria ya Marekebisho ya Sheia ya Ushindani
wa mwaka 2015 na wa Sheria ya Tume ya Walimu wa mwaka 2015.
Wakati
akisema hivyo, baadhi ya wabunge wa upinzani waliendelea kusema kuwa
alichofanya siyo utaratibu.
Baada ya
hapo aliwafafanulia wabunge kuwa kwa mujibu wa kifungu cha 47 kinasema, iwapo
Spika ataridhika kwamba jambo hilo ni la dharura na lina maslahi kwa umma basi
ataruhusu hoja litolewe kwa muda dakika
tano, na mjadala wa hoja utawezekana kama Spika ataridhika.
Pamoja na
maelezo hayo, vurugu hizo za wabunge ziliendelea hadi alipoamua kuahirisha
kikao hicho hadi jioni.
No comments:
Post a Comment