BUNGE LATAKA WAHUNI WA MITANDAONI KUBANWA ZAIDI


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imependekeza kwa Serikali iongeze adhabu ya faini kutoka Sh milioni tatu na kifungo kisichopungua miezi sita na kuwa faini ya Sh milioni tano na kifungo kisichopungua miezi sita kwa wale wote watakaotuma katika mtandao taarifa za uongo.

Aidha, kamati hiyo imependekeza katika adhabu kwa watu wanaonyanyasa wenzao kupitia mtandaoni, adhabu yao iongezwe kutoka kifungo cha mwaka mmoja na kuwa kifungo cha miaka mitano.
Akiwasilisha maoni ya Kamati hiyo kuhusu Muswada wa Sheria ya Uhalifu wa Mtando wa mwaka 2015, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Peter Serukamba alisema adhabu zilizowekwa katika sheria hiyo hazitoshelezi kulingana na athari za makosa hayo.
“Kamati imeona umuhimu wa kuongeza adhabu hizi katika maeneo haya, kutokana na ukweli kuwa kumekuwa na wimbi kubwa la watu wanaodhalilisha utu wa watu wengine katika mitandao ya kompyuta jambo lililoathiri watu wengi, familia, jamii na nchi kwa ujumla,” alisema Serukamba.
Alisema kamati hiyo, pia inashauri uwekwe utaratibu wa Serikali kuchukua hatua za ufuatiliaji kabla ya mtu aliyenyanyaswa kuripoti. “Hii ihusishe mfumo wa kuweza kumtambua mtu aliyesambaza picha ama taarifa hizo.”
Awali akiwasilisha maelezo ya muswada huo, Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, alisema  kutokana na kukua kwa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), kumesababisha kuwepo kwa changamoto mbalimbali ikiwemo kuibuka kwa makosa ya mtandao.
Alitaja makosa ya mtandao yaliyokithiri kwa sasa kuwa ni makosa dhidi ya faragha, usalama na upatikanaji wa taarifa za kompyuta na mifumo ya kompyutam makosa yanayohusu maudhui, makosa dhidi ya mifumo ya kompyuta na makosa ya kawaida yanayofanywa kwa kutumia mitandao.
Alisema waathirika na waathirika wa makosa hayo ni pamoja na Serikali, sekta binafsi, watu binafsi na jamii kwa ujumla na takwimu kutoka jeshi la polisi zinaonesha kuwa makosa ya uhalifu wa mtandao yaliyoripotiwa na kuchunguzwa kati ya mwaka 2012 hadi Agosti mwaka jana ni 400.
Alisema katika kipindi cha mwaka 2010 hadi mwaka 2013, makosa ya uhalifu wa mitandao yalisababisha hasara ya zaidi ya Sh bilioni 9.8 kwenye taasisi za fedha pekee.
Pia alisema kitengo cha kudhibiti makosa ya uhalifu wa mtandao kiliripoti kukamatwa kwa watu zaidi ya 500 wakiwemo raia wa kigeni  kwa makosa hayo ya uhalifu wa mtandao.
Alisema sheria hiyo, inapendekeza kuweka utaratibu wa kuzuia na kudhibiti uhalifu wa mitandao, kuainisha makosa na adhabu dhidi ya uhalifu wa mtandao, kuainisha kanuni na taratibu za upelelezi na uendeshaji wa mashaka ya makosa ya uhalifu wa mtandao na kuweka utaratibu wa ukusanyaji wa vielelezo, ushahidi na kumbukumbu za makosa ya halifu huo wa mtandao.
Sheria hiyo katika eneo la adhabu kwa wahalifu wa mtandao pamoja na wasambazaji wa picha za utupu na ngono, wasambazaji wa taarifa za uongo, za kibaguzi na matusi na watu wengine wanaofanya udanganyifu unaohusu kompyuta, adhabu ni kwenda jela hadi miaka 10 au kulipa faini isiyopungua Sh milioni 50.
Katika sheria hiyo, pia mtu atakayesambaza ponografia ya watoto kupitia mtandao wa kompyuta atawajibika kulipa faini isiyopungua Sh milioni 50 au mara tatu  ya faida iliyopatikana kinyume cha sheria au kifungo kisichopungua miaka saba jela au vyote kwa pamoja. Mkosaji pia ataamriwa kumlipa mwathirika fidia.

No comments: