WAZIRI AOKOA MAISHA YA MJAMZITO PORINI RUFIJI


Mbunge wa Rufiji ambaye pia ni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid, juzi alichangia kuyaokoa maisha ya Amina Bakari (20), mjamzito aliyesota porini kwa saa sita akisubiri usafiri wa kumfikisha hospitali ya wilaya iliyopo Utete kwenda kujifungua.

Kabla ya msaada wa mbunge huyo aliyekuwa katika ziara jimboni kwake, Amina alikodi pikipiki imwahishe hospitali, lakini baada ya umbali fulani, mama huyo alishindwa kuhimili mtikisiko na kuomba ashushwe kwa kuwa pia dalili za uchungu wa kujifungua zilikuwa zimeongezeka.
Dereva wa bodaboda, Mussa Idd alisema aliridhia kumsikiliza mteja wake na hivyo kumshusha katika eneo la Nyagolombe mpakani mwa kijiji cha Utungi na Nyamwage, lakini kwa zaidi ya saa sita mama huyo hakupata usafiri, huku akihangaika kutokana na kushikwa na uchungu.
 “Lakini tukiwa tumeshakata tamaa na kusubiri ajifungue tukiwa porini, lilitokea gari na nikasimamisha ili kuomba msaada. Kumbe lilikuwa na mbunge wetu, hakuwa na hiyana alitusaidia kumkimbiza mgonjwa hospitalini umbali wa kilometa 20…,” alisema.
Akiwa katika ziara hiyo, Dk Rashid aliyezungukia vijiji na miradi mbalimbali, aliwataka wananchi wa Jimbo la Rufiji kuthamini michango inayotolewa kwa ajili ya kuimarisha afya, umeme, shule na uboreshaji wa sekta ya mawasiliano katika wilaya ya Rufiji.
Akizungumza juzi na watendaji wa Serikali za Mitaa ngazi ya vitongoji katika  kijiji cha Garambe, Dk Rashid alisema mambo yaliyofanyika katika wilaya hiyo  ni mengi na yenye tija kwa kila mwananchi, hivyo waiheshimu michango hiyo kwa kuigeuza kuwa fursa za maendeleo.
Alisema wilaya ya Rufiji inaongoza kwa kuwa na magari ya kubebea wagonjwa  kuliko nyingine hapa nchini, pia wilayani humo kumejengwa kituo cha afya karibu kila kata pamoja na zahanati,kitu ambacho ni cha kujivunia katika uongozi wake.
"Hadi sasa wilaya ina magari saba ya kubebea na huenda yakaongezeka kutokana na kuendelea kuwashawishi wafadhili wa ndani na nje ili kusaidia  hilo, pia acheni kurubuniwa na watu wachache wanaosema kuwa sijafanya chochote  hapa jimboni," alisema.
Alisema katika kituo cha Afya Ikwiriri, kipo chumba cha upasuaji  kinamaliziwa kujengwa kwa gharama ya Sh milioni 150 ambacho kitakuwa cha kisasa na kitasaidia wakazi wa  wilaya hiyo pamoja na za jirani.

No comments: