Mwenyekiti wa Kamati ya Shule ya
Msingi Udasi mwambao mwa Ziwa Tanganyika, kata ya Kabwe wilayani Nkasi mkoani
Rukwa, Ismail Ndomboya (42) amenusurika kuuawa na mamba kwa kupambana kijasiri
na mnyama huyo kwa zaidi ya nusu saa.
Hata hivyo, licha ya kuokoa
maisha yake mnyama huyo katika
mapambano hayo alimng’ata na kumnyofoa
mkono wake wa kulia na
kutokomea nao ziwani.
Diwani wa Kata ya Kabwe, Asante
Lugwisha akizungumza na mwandishi wa habari hizi
kwa njia ya simu alithibitisha kutokea
kwa mkasa huo uliotokea juzi
saa moja na nusu jioni wakati Ismail
alipokuwa akioga katika Ziwa
Tanganyika kijijini Kabwe .
Akisimulia mkasa
huo, Diwani Lugwisha alibainisha kuwa jioni
hiyo ya tukio Ismail aliamua kwenda
kuoga ziwani wakati huo akiwa pekee ndipo
ghafla mamba alimvamia ghfla
na kumuuma mkono wake wa kulia.
“Kwa ujasiri mkubwa Ismail
alipambana kufa au kupona na mnyama huyo
kwa nusu saa huku akipiga yowe akiomba msaada
lakini hakuna aliyejitokeza kumsaidia kwa
sababu sehemu aliyokuwa akioga
ilikuwa mbali na makazi ya watu,“
alieleza.
Aliendelea kueleza kuwa
hatimaye mamba aliunyofoa
mkono wa kushoto wa Ismail na kutokomea
nao ziwani ndipo Ismail alipokimbia
kuelekea nyumbani kwake akiwa
uchi.
“Baadaye nilitaarifiwa kuwa Ismail ameshambuliwa
na mamba
wakati akioga ndipo nilipofika nyumbani kwake, na tulijipanga
tukamkimbiza katika Hospitali Teule ya
Wilaya (DDH) mjini Namanyere ambao tulifika saa
nne na nusu usiku ambako
amelazwa kwa matibabu “ alieleza.
Mtaalamu wa afya wa Hospitali ya Wilaya, ambaye alikiri kuwa si msemaji,
alikiri kupokelewa kwa
mgonjwa huyo aliyejeruhiwa
na mamba ambapo aliielezea hali yake kuwa inaendelea vizuri.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa ,
Jacob Mwaruanda amethibitisha kutokea
kwa mkasa huo na kwamba uchunguzi wa
tukio hilo unaendelea.
No comments:
Post a Comment