MAHAKAMA KUU YATUPA OMBI DHIDI YA KAMPUNI YA VIP


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imetupilia mbali ombi la kuitaka kampuni ya uwekezaji ya VIP Engineering and Marketing, kutoa majibu ya ziada kwa maswali ya awali katika kesi ya Sh bilioni 787 inayohusu kampuni ya ufuaji umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).

Jaji Salvatory Bongole alitoa uamuzi huo dhidi ya ombi lililowasilishwa na  kundi la mabenki linaloundwa na Standard Chartered Bank PLC, Standard Chartered Bank (Hong Kong)Limited, na ya Tanzania Limited pamoja na wafilisi wa Mechmar Corporation (Malaysia) Berhad.
Akitoa uamuzi huo Jaji Bongole alisema  amri iliyotolewa Januari 27, mwaka huu na Mahakama hiyo kuhusu wahusika wengine katika kesi hiyo, Wartsila NederlandBV na Wartsila Tanzania Limited, ambao pia walidai kupewa majibu ya maswali hayo ya ziada, pia inazihusu benki hizo pamoja na wafilisi wa MechmarCorporation.
Katika amri hiyo, Jaji Bongole alisema hawezi kuruhusu utoaji wa majibu zaidi kwa sababu haitakuwa kwenye mazingira ya kutenda haki katika kutoa uamuzi wa shauri hilo au kusaidia kupunguza gharama.
Jaji Bongole alisema baada ya kuzingatia ombi la walalamikiwa na kiapo cha pingamizi kwenye majibu hayo, aligundua kuruhusu majibu zaidi katika hatua hiyo ya shauri kutasababisha kuivuruga kesi hiyo jambo ambalo haliruhusiwi kisheria.
Alisema kwa hatua hiyo kampuni ya VIP Engineeringand Marketing imewasilisha nyaraka zake za majibu kwa njia ya maandishi hivyo wamekamilisha nyaraka zote zinazohitajika na zile ambazo ziliombwa lakini hazijaletwa zitaombwa wakati wa kuhojiana kesi itapokuwa inaendelea.
Awali wakati wa usikilizwaji wa ombi hilo, Wakili wa kampuni ya VIP, Michael Ngalo, alidai kuwa ombi hilo kuhusu kupewa nyaraka zaidi halina msingi, ni ya kashfa na yenye kuwakandamiza na pia yameletwa bila ya kufuata taratibu za kimahakama.
Wakili Gasper Nyika, kwa niaba ya Kundi la Benki, alidai katika kiapo kinachounga mkono ombi hilo kuwa, kampuni ya VIP haijatoa vielelezo vya kutosha kama ilivyoamriwa na majibu yaliyotolewa hayakutosheleza.
Hata hivyo, Wakili Ngalo alidai wametoa majibu yanayotosha kwa maswali hayo hasa kama Standard Chartered ni mwezeshaji wa kifedha wa IPTL ambapo wamejibu kwa sasa hakuna muwezeshaji wa aina hiyo na pia benki ya Standard Charetered siyo mkopeshaji wa IPTL.
Katika shauri la msingi, kampuni ya VIP imefungua mashitaka dhidi ya walalamikiwa kwa kula njama za pamoja na kuhujumu maslahi yake katika kampuni ya IPTL aidha inawadai fidia ya dola milioni 490.9  za Kimarekani kwa kuiibia, kuhujumu haki zake na kuisababishia hasara katika maslahi yake ndani ya IPTL.
Aidha imeomba Mahakama itoe tamko kuwa benki hizo pamoja na mawakala wao hawajawahi kuwa wakopeshaji halali wa IPTL pia wamefanya makosa ya wizi, kutakatisha fedha, na kusababisha hasara kwa kampuni za IPTL na VIP kutokana na vitendo vyao.

No comments: