Wakimbizi 115,138 wanaoishi
katika makazi ya Mishamo na Katumba mkoani Katavi, waliopewa uraia wa Tanzania,
wana haki zote kama Watanzania wa kuzaliwa ya kuwapigia kura madiwani , wabunge na rais ,
katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Makazi
ya Katumba wilayani Mlele, Athman Igwe katika
kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Rukwa (RCC).
Alisema hayo alipokuwa akijibu swali
la Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) mkoani humo, Laurent Magweshi, aliyetaka
kujua iwapo wakimbizi waliopewa uraia
nchini, wana sifa ya kupiga kura katika
uchaguzi mkuu ujao wa Oktoba mwaka huu.
“Wakimbizi hao sasa ni Watanzania
wapya na wana haki kama walizonazo Watanzania wa kuzaliwa ya kupiga kura
katika uchaguzi mkuu ujao,“
alifafanua.
Aliongeza kuwa wanayo haki pia ya kujiandikisha
katika daftari la kudumu la
wapiga kura na
aliwahamasisha kujitokeza kwa wingi,
kujiandikisha ili waweze kuipigia
kura Katiba inayopendekezwa Aprili 30 ,
mwaka huu .
“Watanzania hawa wapya wanayo haki
ya kuchagua na kuchaguliwa katika
nafasi zote za uongozi ikiwemo nafasi
ya ubunge, lakini hawaruhusiwi
kugombea nafasi ya urais,”
alisisitiza
Alibainisha kuwa wakimbizi wapatao
115,138 wanaoishi kwenye Makazi ya Mishamo na Katumba, wamepewa uraia wa
Tanzania, katika mpango wa ugawaji vyeti unaoendelea, ambapo 62,544 wanatoka makazi ya Katumba wilayani
Mlele na
52,594 makazi ya Mishamo wilayani
Mpanda.
Akiwasilisha taarifa ya ugawaji wa
vyeti vya Watanzania wapya waliokuwa wakiishi kwenye mkazi hayo, Ofisa
Maendeleo ya Jamii kutoka Sekretarieti ya Mkoa, Ignas Kikwala alisema makazi ya Katumba yalipokea wakimbizi 2,800 mwaka 1973 na mwaka 1978 Serikali
ilianzisha Kambi ya wakimbizi ya Mishamo ikiwa na wakimbizi 12,000 .
Ugawaji vyeti kwa Watanzania hao ulianza Novemba 26, mwaka jana na utakamilika Aprili 30 mwaka huu kwa makazi
ya Katumba na Mishamo na
Ulyankulu mkoani Tabora .
No comments:
Post a Comment