WATANO KORTINI KWA KUMDHALILISHA ASKARI POLISI


Wafanyabiashara watatu na wanachuo watano wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi  Singida wakikabiliwa na mashitaka ya kumdhalilisha kupindukia askari polisi wa kike  na kumsababishia maumivu makali mwilini.

Mwanasheria wa Serikali, Petrida Mutta alidai mbele ya Hakimu Joyce Minde, kwamba kwa pamoja, washitakiwa hao walimfanyia unyama askari huyo kwa kumvua nguo zote na kumwacha mtupu kisha kumshambulia na kumsababishia maumivu makali mwilini.
Waliopandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi, Joyce Minde, ni Jasmin  Iddi (40), Abdallah Hamduni (26), Ramadhani Bakari (32) wote wafanyabiashara wa mjini hapa pamoja na dereva, Saidi Saidi (50) .
Wengine ni Aurelia Adolf Mushi (20), Grace Daniel Paul (21), Happiness Kiluvya (23), Jackline John (20) na Constansia Masaki (21) wanaodaiwa ni wanachuo katika moja ya vyuo vya elimu ya juu mjini Singida.
Mwanasheria wa serikali, alidai  wakati wote wa kitendo hicho cha udhalilishaji, polisi huyo, alikuwa akichukuliwa picha za video huku akiwa mtupu na kuzisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.
Tukio hilo inadaiwa lilifanyika Februari 14, mwaka huu saa 11.30 jioni ambako kwa mujibu wa Mwendesha Mashitaka, inadaiwa polisi huyo wa kike alikutwa akiwa na mume wa mshitakiwa,  Jasmin wakiwa kando ya Ziwa Singidani wakivinjari siku hiyo ya Wapendanao.
Hata hivyo, mume  ambaye jina halikupatikana, inadaiwa  alitoroka. Mutta alidai mbele ya mahakama hiyo kuwa kitendo walichofanya washitakiwa ni kinyume na Kanuni ya Adhabu 138 A kifungu cha 16 cha Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama kilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Wote walikana mashitaka.

No comments: