MWANAFUNZI WA CHUO KIKUU ASHINDA MILIONI 10 ZA MENGI


Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ardhi, Viana Mulokozi ameibuka mshindi wa Sh milioni 10 za shindano la 3N,  linaloendeshwa na  Mwenyekiti  wa Makampuni ya IPP, Dk Reginald Mengi.

Licha ya Viana ambaye ni mshindi kwa mwezi Februari, washiriki wengine tisa ambao waliingia 10 bora walikabidhiwa Sh milioni moja kila mmoja.  Baadhi ya vijana hao ni Irene Mateshi, Gelard Malamba, Edson Kashaija, Mjamaica Rabsa, Michael Emanuel  na Frank Mwasekagu.
 Shindano hilo ambalo linajulikana kama Nitabuni, Nitafanya na Nitafanikiwa (3N), limebuniwa na Dk Mengi kwa ajili ya kuwapa fursa vijana kubuni miradi ya kibiashara ambayo wanaweza kuiendesha.
Shindano hilo litaendeshwa kwa miezi sita na linaendeshwa kupitia Tweet na Mengi na kila mwezi Dk Mengi anatoa Sh milioni 19 kwa ajili ya washindi. Mwezi uliopita jumla ya tweeter zilizotumwa zilikuwa 5,069.
Viana katika wazo lake amesema ameanzisha mtandao maalum ambalo utatumiwa na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu kwa ajili ya kutafuta mashirika na kampuni ambazo wanaweza kwenda kufanya  mafunzo kwa vitendo.
Alisema wanafunzi wengi walioko vyuo vya elimu ya juu kila mwaka wanatakiwa kwenda kwenye mafunzo, lakini wengi wamekuwa wanaenda kwenye kampuni kubwa wakati kuna kampuni ndogo ambazo zinawahitaji lakini hawazifahamu.
 "Nimekuja na wazo hili kwa kutambua kuwa kuna kampuni zinahitaji wanafunzi lakini hazifahamiki, hivyo ninaamini kuwa kwa kutumia mtandao huu, wanachuo wote wataweza kupata mafunzo kwa vitendo kwa kulipia fedha kidogo badala ya kuzunguka mjini kusaka nafasi kwenye kampuni mbalimbali," alisema.
Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi hizo, Dk Mengi aliwataka vijana kuacha tamaa ya kutaka utajiri wa haraka kitendo ambacho kitawafanya waingie kwenye vitendo vya rushwa. Alisema utajiri wa namna hiyo una laana ya Mungu.
Alisema ameanzisha shindano hilo kwa ajili ya kuwafanya vijana waingie kwenye biashara ili waweze kuondoa ombwe la kiuchumi lilipo kati ya nchi hii ambayo ni tajiri lakini watu wake ni masikini. Aliwataka vijana hao wakifanikiwa wasisahau kuwasaidia wenzao ambao pia watakuwa ni wahitaji.
Pia, aliwataka vijana hao kuepuka kuingia kwenye masuala ya kusema uongo ili wafanikiwe na akaonya kuwa ni kufanya shughuli halali na kusema ukweli kutawafanya wafanikiwe katika maisha yao.

No comments: