Mtoto wa umri
wa miaka sita, mwenye ulemavu wa ngozi (albino), anayeishi Kijiji cha
Ndoleleji, amekoswakoswa na watu waliokuwa wakimvizia akiwa katika michezo,
baada ya watoto wenzake kuchukua uamuzi wa kumlinda.
Taarifa zilizomfikia
mwandishi, zilieleza kuwa ‘wawindaji’ hao waliokuwa na gari lililokuwa na vioo
vya giza, walionekana wakimfuatilia mtoto huyo Jumamosi ya wiki iliyopita
alipokuwa akiogelea mtoni na baada ya kumkosa, wakamfuatilia katika uwanja wa
mpira Jumatatu, ambako nako walimkosa.
Akizungumza na mwandishi,
diwani wa Kata ya Shagihilu wilayani Kishapu mkoani hapa, Mohamed Amani
alisema kumefanyika majaribio mawili ya
kutaka kumteka mtoto huyo (jina limehifadhiwa), lakini kwa msaada wa watoto
wenzake hayakufanikiwa.
Kwa mujibu wa
Diwani Amani, Jumamosi iliyopita watu watatu wakiwa kwenye gari hilo, walifika
kijijini hapo na kwenda mpaka mtoni, ambako mto huyo mwenye ulemavu wa ngozi
alikuwa akicheza na wenzake.
Baada ya kufika
mtoni, watu hao wote watatu waliteremka kwenye gari na kusogea katika eneo la
mto, hatua iliyowashitua watoto wenzake waliokuwa wakicheza wote mtoni.
Kwa mujibu wa
Amani, watoto hao wenye umri mkubwa zaidi ya mtoto huyo, walitambua hatari
iliyokuwa ikimkabili mwenzao mwenye ulemavu wa ngozi na
dalili za watu
hao waliokuwa hawawafahamu, waliokuwa wakizidi kuwasogelea.
Baada ya kuona
watu hao wakizidi kusogelea eneo lao la michezo, watoto hao walimshauri mwenzao
mwenye ulemavu wa ngozi, akimbilie nyumbani kwao na mtoto huyo akasikia ushauri
huo na kurudi nyumbani.
“Baada ya mtoto
(albino) kukimbilia nyumbani kwao, wale watu waliingia kwenye lile gari na
kuondoka,” alisema Amani na kuongeza kuwa hatua ya watu hao kutosema lolote kwa
watoto hao lilizidi kuwapa mashaka.
Jumatatu ya
wiki hii jioni wakati mtoto huyo alipokuwa na wenzake, wakiwemo wale aliokuwa
nao mtoni, wakicheza mpira wa miguu katika kiwanja cha kijijini hapo, gari hilo
lililoonekana mtoni, lilifika uwanjani hapo na kusimama.
Inaelezwa kuwa
baada ya kusimama, watu wale watatu walioonekana mtoni walishuka katika gari
hilo, wakaegemea gari na kuangalia watoto hao wakicheza mpira, akiwemo mwenzao
mwenye ulemavu wa ngozi.
“Safari hii
haikuwa mtoni, bali katika eneo jingine tena la wazi ambalo mtoto huyo alikuwa
akicheza mpira na wenzake… walipofika walisimama nje ya gari lao,” alisema
Diwani Amani.
Kutokana na
hali hiyo, watoto hao walihisi kuna hali ya hatari kwa mwenzao, baada ya watoto
hao kuona gari hilo kwa mara nyingine, na watu hao wakiwa wamewasimamia na
hawakuwa wakizungumza chochote.
Diwani huyo
alisema watoto hao walisitisha mchezo wao, na kumtaka mwenzao kwa mara nyingine
akimbilie nyumbani kwao, ili kusalimisha maisha yake kutokana na utata wa
usalama ulioanza kujitokeza hapo.
Akizungumza na mwandishi,
mama mzazi wa mtoto huyo, Regina Malando, alithibitisha kurejea nyumbani mara
mbili kwa mtoto wake huku akikimbia.
Regina alisema
baada ya kurejea nyumbani, mtoto huyo alimweleza kuwa kuna watu asiowafahamu
waliokuwa wamesimama kando ya uwanja waliokuwa wakifanyia mazoezi na kwamba
anawaogopa.
Mama huyo
alisema, baada ya kupewa taarifa hizo mara mbili, alimsihi mtoto wake aingie
ndani na atulie na akome kwenda kucheza mbali na nyumbani kwao na mtoto huyo
akatii ushauri wa mama yake.
Baba wa mtoto
huyo, Tito Shija, alisema aliposikia taarifa hiyo ya pili, alikwenda katika
uwanja huo na kukuta watu hao wakiingia kwenye gari na kuondoka kwa kasi.
Shija alisema
kwa bahati mbaya hakuweza
kuchukua namba
za usajili wa gari hilo, ila alishuhudia kuwa gari hilo lilikuwa na vioo vya
giza sehemu zote.
Kwa mujibu wa
Shija, kesho yake binti mmoja ambaye hakumtaja jina, alimwambia kuwa alipita
karibu ya hao watu wakamfokea na kumuuliza anatafuta nini huko na
kumwamuru
aondoke haraka karibu yao.
Shija alidai
kuwa binti huyo alimwambia kuwa wakati akiondoka, alisikia watu hao wakijadili namna ya kumpata mtoto
huyo, wakati alipokuwa akikimbilia kwao.
Diwani Amani
alisema, kutokana na hali hiyo alifikisha suala hilo kwenye Kikao cha Kamati ya
Maendeleo ya Kata na ikaamuliwa mtoto huyo mwenye ulemavu wa ngozi, apelekwe
kwenye kituo cha watoto wenye ulemavu wa ngozi, kilichopo Buhangija katika
Manispaa ya Shinyanga.
Mwandishi alifuatilia
utekelezaji wa uamuzi huo na kuhakikishiwa na Mkuu wa Kituo hicho cha
Buhangija, Peter Ajali, kwamba amempokea mtoto huyo na kuongeza kuwa idadi ya
watoto katika kituo hicho inaongezeka kila siku, na sasa wamefikia watoto 349 wenye ulemavu wa
ngozi.
Mwanzoni mwa
mwezi huu, mtoto mwingine wa kiume mwenye ulemavu wa ngozi, Baraka Cosmas (6)
aliyekuwa akiishi na wazazi wake kijijini Kipeta, Bonde la Ziwa Rukwa wilayani
Sumbawanga, alishambuliwa na kujeruhiwa vibaya kwa kukatwa kiganja cha mkono
wake wa kulia na watu wasiojulikana kisha kutokomea nacho kusikojulikana.
Mama mzazi
Prisca Shaaban (28), alisema tukio hilo lilimkuta saa saba usiku, wakati
akitaka kutoka nje kujisaidia.
“Nilikutana na
mtu akifungua mlango, akanipiga ni kitu kichwani kisha nikazimia, nilipozinduka
nikapiga kelele na majirani wakafika ndipo nilipogundua mtoto wangu amekatwa
kiganja cha mkono wa kulia,” alisema mama mzazi.
*Picha ya maktaba ya mtoto albino aliyekatwa kiganja Rukwa hivi karibuni.
No comments:
Post a Comment