Wanafunzi watano wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
(UDSM), ni miongoni mwa watu 50 waliokufa katika ajali ya basi la Majinja,
lililogongana na lori katika eneo la Changarawe Mafinga mkoani Iringa.
Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandala alisema waliopoteza
maisha ni wanafunzi watatu wa mwaka wa
tatu na wawili wa mwaka wa pili, wote kutoka kitivo cha Sayansi ya Jamii (BA
Education, COHU).
Alitaja wa mwaka wa tatu kuwa ni Killeo Eric, Sosten Daud na Chiwangu
Didimo na wa mwaka wa pili katika kitivo hicho ni Watson Jeremiah na Mbaule
Frank aliyekuwa mwaka wa pili katika Chuo Kikuu Kishiriki cha UDSM cha Elimu
cha Dar es Salaam (DUCE).
Alisema miili ya marehemu hao imeshachukuliwa na familia zao na kusafirishwa
kwa ajili ya maziko.
Profesa Mukandala alitaja waliojeruhiwa kuwa ni Tupate Mosigwa, ambaye
yuko mwaka wa kwanza, ambaye awali alilazwa katika Hospitali ya Wilaya ya
Mafinga na sasa amehamishiwa kwenye
Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kwa matibabu zaidi.
Mwanafunzi mwingine aliyejeruhiwa ni Rafael Norbert, aliyekuwa mwaka wa
kwanza DUCE, aliyetibiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mafinga na kuruhusiwa
kurejea nyumbani kwa matibabu zaidi.
Profesa Mukandala alisema uongozi wa chuo hicho unatoa pole kwa familia
za wanafunzi hao pamoja na jamii nzima ya UDSM kwa kupoteza wapendwa hao.
Alisema chuo hicho kitaendelea kuwasiliana na mamlaka za Mkoa wa Iringa
kufahamu kama kuna majeruhi au marehemu wengine kutoka katika jamii hiyo, na
kutaka wanafunzi kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu kwa kuombea familia
za wapendwa waliokufa na waliojeruhiwa.
Uongozi wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
(Daruso), pia katika taarifa yake iliyotolewa na Waziri Mkuu wake, Gibson
George iliwashukuru wanachuo wote waliokuwa bega kwa bega katika kutambua
wenzao.
Alisema UDSM imepoteza wanachuo
wanne na chuo kishiriki cha DUCE, kimepoteza mmoja na kufanya jumla yao kuwa watano.
Kwa mujibu wa George, utaratibu wa rambirambi unasimamiwa na Serikali ya
Wanafunzi katika ngazi ya Shule Kuu, chini ya usimamizi wa wenyeviti na wabunge
na mratibu ni Massawe Chrisostom ambae
ni Mwenyekiti wa Kitivo kilichopoteza wanafunzi wanne.
Alisema kwa niaba ya Daruso
wanatoa pole kwa msiba huo na kushukuru uongozi wa chuo kwa kushiriki katika
misiba na kuwatuma wawakilishi kutoka chuoni hapo.
Ajali hiyo ilihusisha lori aina ya Scania namba T 689 APJ mali ya Cipex
Company, lililokuwa likiendeshwa na Maka Sebastian (26), ambaye amelazwa katika
Hospitali ya Mkoa wa Iringa akiendelea na matibabu na basi aina ya Scania namba
T438 CED mali ya kampuni ya Majinja lililokuwa likiendeshwa na Baraka Gabriel
(38) aliyekufa papo hapo.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi amesema chanzo cha
ajali hiyo ni ubovu wa barabara katika eneo la ajali na mwendo kasi.
Baada ya magari hayo kugongana, kontena lililokuwa limepakiwa katika
lori hilo lilifyatuka na kupiga basi hilo, hali iliyosababisha mauti kwa watu
50 na majeruhi wengi.
No comments:
Post a Comment