ALIYEJIFANYA KATIBU WA IKULU ATIWA MBARONI DAR

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia mkazi wa Mbagala Rangi Tatu, Haroub Mtopa (44) kwa kujifanya mtumishi wa umma kupitia cheo cha Katibu wa Rais, Jakaya Kikwete, Prosper Mbena.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam, Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa juzi jioni.
Kova alisema Mtopa alikuwa na mazoea ya kujifanya mtumishi wa Ikulu kwa nia ya kudanganya watu kwamba anaweza kuwasaidia shida zao ili ajipatie fedha.
Katika kufanya kazi zake za kitapeli, Kova alisema mtuhumiwa huyo alikuwa akiingia na kutoka Ikulu mara kwa mara, huku akijifanya kuwa  na shida nyingi hivyo alikuwa akiomba msaada. 
‘’Huyu mtu ni tapeli wa muda mrefu sana, tulimkamata baada ya mwananchi mmoja kuzungumza na mtuhumiwa huyo na kuahidiana kumpa Sh 500,000 na kutanguliziwa Sh 250,000. Baadae aliitwa siku nyingine afuate fedha iliyobaki.
‘’Mwananchi huyo ambaye hakumtaja jina, alimhofia Mtopa ndipo alipotoa taarifa  Polisi kisha akamwambia mtuhumiwa huyo aende kuchukua fedha iliyobaki, hatua iliyosaidia Polisi kumkamata kwa urahisi,’’ alisema.
Kova alisema kuwa mtu huyo ni hatari kwa sababu kutumia cheo cha Katibu wa Rais wakati inamaanisha kwamba mtu huyo aliweza kutapeli watu wengi sana kupitia cheo hicho.
Kwa mujibu wa Kova, mtuhumiwa huyo amekuwa akizunguka katika wizara mbalimbali ikiwamo ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Maji  na taasisi nyingine zinazotoa huduma kwa jamii, kwa lengo la kuomba msaada.
Alisema kabla ya kumkamata, walishirikiana na Ikulu baada ya watu wengi kupeleka malalamiko yao kuhusu mtuhumiwa huyo.
Kova aliwaasa wananchi kuepuka kujifanya watumishi wa umma kwani ni kosa kisheria na kuongeza kuwa wameweka kikosi maalumu kitakachoshughulikia masuala ya watu wanaozunguka zunguka nje za ofisi za watu pasipo shughuli maalumu.

No comments: