KINANA ASEMA WIZI SERIKALINI UMEIGHARIMU CCM


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, amesema wizi ndani ya Serikali ni moja ya mambo mawili yanayoangusha chama hicho na amewataka wanachama wake kutoka kimya na badala yake, kupigia kelele vitendo vya wizi kwa watendaji wa Serikali.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu huyo ameeleza kukerwa na dhana ya utawala bora, ambayo amesema imekuwa ikitumiwa kama kivuli cha kulinda wezi wa mali ya umma, kwa maelezo kuwa ni ngumu kuwafukuza madarakani au kuwaadabisha bila kufuata sheria.
Alisema hayo alipozungumza na wanaCCM wa Jimbo la Kibakwe mkoani Mpwapwa, akiwa katika ziara ya kutembelea Mkoa wa Dodoma kukagua shughuli mbalimbali za maendeleo, ikiwemo utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2010.
"Yapo mambo yamewaudhi Watanzania wengi. Kwanza ni suala la wizi serikalini. Eti mtu kaiba halafu sisi tunaanza kupiga maneno mara ooh kaiba au hajaiba? Aondoke asiondoke?
“Tumwadhibu tusimwadhibu? Ukweli ni kwamba mtu akituhumiwa, tuhuma peke yake inatosha kumfanya aondoke na kama hataki basi tumuondoe kwa nguvu na si kuleta maneno,” alisema na kuongeza kuwa enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, dhana hiyo haikupewa nafasi kwa wezi.
"Lazima niseme wazi, Watanzania wametushangaa sana katika hili, mwingine akiiba kuku si sawa… wakubwa serikalini wanasema afungwe, lakini huyu aliyeiba fedha nyingi za umma tunasema utawala bora!
“Lazima tulikatae hili kwa nguvu zote na mtu wa kwanza
anayepaswa kukasirika ni mwanaCCM, kuweni wakali acheni kabisa kulindana," alisema Kinana.
Akionesha wazi kukerwa na hali hiyo, Kinana alisema kinachosikitisha zaidi ni kuona mtendaji ndani ya Serikali anapoiba, wanajitokeza wanaCCM wengine ili kumkingia kifua asichukuliwe hatua, jambo ambalo limekuwa likiwakera Watanzania wengi.
"Mtu ameiba wazi kabisa, wanatokea wanaCCM wenzake utasikia oooh hakujua, ooh tumuonee huruma. Jamani huyu mtu hakujua kwani hana macho kuona anachokifanya ni wizi?
“Nawaomba wanaCCM simamieni uadilifu, mmechaguliwa na wananchi kutokana na imani yao kwenu na kama tunavyofahamu imani huzaa imani, nataka niahidi CCM tutakuwa wakali sana ukiiba lazima uondoke," alisema Kinana.
Akielezea kukerwa na matumizi ya dhana ya utawala bora, Kinana alisema dhana hiyo katika siku za hivi karibuni imeanza kutumiwa, ili kulinda wezi wa mali ya umma wasichukuliwe hatua na kuadhibiwa kwa makosa wanayoyafanya.
"Siku hizi kuna hiki kitu kimezuka kinaitwa utawala bora. Wakati mtu anaiba hafuati utawala bora, lakini akishaiba na kukamatwa utasikia lazima tufuate utawala bora, mara tuunde Tume, mara mpeni muda wa kujitetea, huyu mtu keshaiba unapompa nafasi na tena kama ana fedha alizoiba anaweka mawakili hata wanne.
"Huu utawala bora ni lazima sasa tuutazame kwa macho mawili maana ni kama umeegemea upande mmoja. Mtu anaiba kuku hakuna utawala bora, lakini anaiba mali ya umma, unaambiwa kuna utawala bora! Mwizi dawa yake ni jela si maneno, lazima tujenge utamaduni wa kuwajibishana.
"Lazima tuige wakati wa utawala wa Baba wa Taifa, yeye alisema ukikosea iwe ni sawa na kugusa moto, ukigusa moto adhabu ni palepale, ilikuwa ukibainika tu unastaafishwa kwa manufaa ya umma, lakini sasa unaambiwa utawala bora. Mtu akiiba anahamishwa…
chama chenye misingi imara siku zote kitaheshimika, kitaaminiwa na kitakaa madarakani kwa muda mrefu.
"Mkilindana wanaCCM na Iyena Iyena zenu hamtafika mbali, ni lazima sasa tuwe wakali. Wengi wa wanaCCM ni masikini, na wachache kama 100 au 20 hivi ndio matajiri.  Wanaiba, matajiri wachache wanaoishi maisha ya mbinguni, adhabu wanapata masikini wengi wanaoishi duniani, hili halikubaliki.
"WanaCCM jumla yetu tupo milioni saba lakini hawa wezi wapo kama 100 au 20, tusiyumbishwe na watu hawa wachache, mimi ni Katibu Mkuu wa Chama cha wakulima
masikini na wafanyakazi masikini sitakubali kuona chama changu kinageuzwa dampo la walanguzi," alisema Katibu Mkuu huyo wa CCM.
Kwa upande mwingine aliwataka wanaCCM kutembea kifua mbele kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2010, kutokana na mambo mengi yaliyoahidiwa katika Ilani hiyo kutekelezwa japo alikiri kuwepo kwa changamoto kadhaa.
"Kama kuna kasoro waite wananchi waambie, kama tunapongezwa kwa mazuri tuliyoyafanya ni lazima tukubali kuulizwa maswali kwa yale ambayo hatujayatekeleza. Sio unataka upongezwe kwa mazuri tu lakini mabaya tunayakwepa," alisema Kinana.

No comments: