WADAU WAMPINGA WAZIRI SITTA KUHUSU BOSI WA BANDARI


Wadau wa masuala ya kijamii nchini, wamepinga kitendo cha kusimamishwa kazi kwa aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Madeni Kipande.

Pia, wameomba Rais Jakaya Kikwete kuharakisha uteuzi wa haraka Mkurugenzi wa TPA, badala ya kuiachia taasisi hiyo kuongozwa na watu wanaokaimu nafasi ya ukurugenzi kwa muda mrefu.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Chama cha Kijamii (CCK), Costantine Akitanda alisema Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta (pichani) alipaswa kuchukua muda zaidi, kufahamu masuala mbalimbali yanayoendelea katika mamlaka hiyo.
Alisema kuwa Waziri alipaswa  kutumia muda zaidi kujifunza kinachoendelea hivi sasa ndani ya TPA kupitia Bodi ya Wakurugenzi ya mamlaka hiyo.
‘’Katika suala la zabuni  tumeelezwa na watu walioko ndani ya TPA kwamba Bodi hiyo kwa kushirikiana na menejimenti  chini ya Kipande, wamekuwa wakali kuepusha uwezekano wa watu wasio na sifa stahiki kushinda zabuni zinazotangazwa na Mamlaka ya Bandari,’’ alisema Akitanda.
Pia, alisema kwamba kwa muda mrefu wajanja wengi walikuwa wanajipenyeza kwenye zabuni na kufanikiwa kufanya kazi na TPA kutokana na udhaifu uliokuwepo kwenye usimamizi wa sheria.
Aliongeza kuwa ukali uliooneshwa na  Kipande kwa kushirikiana na Bodi hiyo, ndio uliofanya watu wasioitakia mema TPA, wajipenyeze haraka kwa Waziri Sitta na kumpotosha kuhusu utendaji wake.
“Sitta alipaswa kushirikiana na bodi ili kupata maelezo ya kutosha kuhusu utendaji wa Kipande na pia angemueleza tuhuma hizo na kumpa fursa za kujieleza badala ya kufanya maamuzi ambayo tunaweza kusema ni yasiyo sahihi,’’ alisema Akitanda.
Alisema katika kipindi alichofanya kazi Kipande, masuala ya wizi yamepungua TPA na kwamba mapato ya nchi yameongezeka hali ambayo inaleta aibu kwa kumsimamisha kazi.
Alifafanua kuwa aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Dk Harrison Mwakyembe wakati akisimamia mamlaka hiyo, bandari ilikuwa inahudumia tani milioni 14 kutoka tani milioni 12.5 mwaka juzi.
Pia, alisema wafanyabiashara wa ndani na nje, wamesikitishwa na hatua hiyo kutokana na kusimamishwa mara kwa mara kwa viongozi wa bandari.

No comments: