KINONDONI YAPITISHA BAJETI YA SHILINGI BILIONI 50.1/-


Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imepitisha bajeti ya Sh bilioni 50.1 kwa mwaka 2015/2016,  ikiwa ni mapato ya ndani ya halmashauri hiyo kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya manispaa hiyo.

Akiwasilisha taarifa ya bajeti hiyo mbele ya wajumbe wa mkutano maalumu wa Baraza la Madiwani Dar es Salaam juzi Meya wa Manispaa wa Kinondoni, Yusuph Mwenda alisema mbali ya fedha hizo ambazo ni makusanyo ya ndani,  pia wanatarajia kupokea Sh bilioni 128.6 ikiwa ni ruzuku kutoka serikalini,  hivyo jumla yake ni Sh bilioni 180.01.
Akielezea mchanganuo wa fedha hizo, Mwenda alisema  kati ya Sh bilioni 128.6 za ruzuku ya serikali, Sh bilioni 101.4 ni kwa ajili ya mishahara, Sh bilioni 5.9 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida ikiwemo Sh bilioni 1.4 ya fidia ya vyanzo vilivyofutwa.
Aidha, Sh bilioni 11.3 ni fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo kutoka Hazina na Shi bilioni 9.9 ni ruzuku ya mfuko wa matengenezo ya barabara kutoka mfuko wa barabara (Tamisemi).
Meya Mwenda alisema mpango huo umelenga kufikia dhima ya dira ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa kutekeleza malengo ya Huduma ya Ukimwi na maambukizi mapya kupunguzwa, uboreshaji, uendelezaji na utekelezaji kikamilifu wa Taifa wa kupambana na Ukimwi.
Malengo mengine ni kuimarika kwa upatikanaji na ubora wa huduma za jamii, kuongezeka na kuboreka kwa huduma za kiuchumi na miundombinu ya halmashauri, kuimarika kwa utawala bora na utoaji wa huduma, kuimarika kwa uwezo wa kiuchumi na kijinsia na ustawi wa jamii.
Pia, kuimarika kwa uwezo wa kiuchumi na jinsia na ustawi wa jamii, kuimarika kwa usimamizi wa kujikinga na maafa na milipuko ya magonjwa na kuimarika kwa usimamizi wa maliasili na mazingira.
Mwenda alisema kuwa makadirio ya Sh bilioni 180.01 ni ongezeko la kiasi cha Sh bilioni 44.5 ambayo ni sawa na  asilimia 33 ya Bajeti ya 2014/2015, pia Sh bilioni 128.6 za fedha za ruzuku ya Serikali sawa na ongezeko la asilimia 32 na Sh bilioni 51.2,  sawa na ongezeko la asilimia 45.
Meya Mwenda aliwataka vijana na akina mama wenye sifa za kukopesheka, ikiwemo kutimiza masharti ya mikopo, wajitokeze kwa ajili ya kukopeshwa fedha zitakazoelekezwa katika kila Kata, ambazo ni zaidi Sh  milioni 100 katika Sh bilioni 3.4 za mkopo wa Benki ya DCB.

No comments: