Waziri wa Nishati na Madini, George
Simbachawene ameomba aombewe afanye vizuri asipeleke aibu nyumbani, kwa kile
alichoeleza wizara anayoongoza ni ngumu.
Alisema ugumu wake unatokana na wizara hiyo
kubeba rasilimali za nchi.
“Niombeeni kwa Mungu, wizara hii inahusika na
rasilimali za nchi, ni wizara nzito, kazi ni kubwa tunalinda mafuta, madini,
gesi na umeme, sioni sababu ya kujisifu wala kustahili kuliko wengine. Mnisaidie kwenye maombi ili
nifanye vizuri nisilete aibu nyumbani,” alisema.
Simbachawene ambaye ni Mbunge wa Kibakwe
mkoani Dodoma, alitoa kauli hiyo juzi
wakati akizungumza na wananchi wa Mpwapwa na wapiga kura wake, waliojitokeza
kumlaki na kumpongeza kwa kuteuliwa
kushika wadhifa huo.
Alisema
kuteuliwa kushika wadhifa huo ni jambo moja na anahitaji maombi aweze kutekeleza wajibu,
kutokana na wizara hiyo kubadilishwa mawaziri na manaibu waziri kila mara.
Alisema kwenye wizara hiyo kuna watu wanaotaka
vitalu, kuna watu wanaopora maeneo na wanaotaka kupora mali za Watanzania,
licha ya wao pia kuwa watanzania.
“Pamoja na kulinda mali za Watanzania nina
wajibu wa kuhakikisha nishati inapatikana kwa watu wote na sasa serikali iko
katika mpango kamambe wa kusambaza umeme vijijini,” alisema.
Alisema dhamira ya serikali ni kuhakikisha
vijiji vyote vinakuwa na umeme kwa lengo la kuwafanya Watanzania kuwa na maisha
bora.
Licha ya kukabidhiwa zawadi mbalimbali wakati
wa mkutano wa hadhara uliofanyika Kibakwe,
pia wazee walimkabidhi Sh 100,000
kwa ajili ya kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea tena ubunge jimboni humo.
Aidha, viongozi wa dini walimfanyia maombi.
“Nashukuru kwa mapokezi makubwa na ukarimu mkubwa mliouonesha na nawaahidi sitawaangusha,” alisema.
Awali, kabla ya kufika Kibakwe, waziri huyo
alisimamishwa mara kwa mara njiani na wananchi waliokuwa wamebeba mabango.
Katika vijiji vya Lukole na Kilolo, wananchi
walisema wanahitaji umeme kwani maisha yao yamekuwa magumu kutokana na kutembea
umbali mrefu kutafuta mashine za kusaga.
“…Tunaomba utusaidie tupate umeme. Sisi akina
mama tunatembea umbali mrefu kwenda kusaga tunaporudi tumechelewa ugomvi moja
kwa moja ndani ya nyumba,” alisikika mama mmoja akilalamika.
Waziri alimtaka Meneja wa Shirika la Umeme
(Tanesco) Mkoa wa Dodoma, Zakayo Temu kuhakikisha kijiji hicho kinapatiwa
transfoma umeme uanze kusambazwa.
“Nimeshatoa maagizo na meneja kanihakikishia
hadi Juni mwaka huu, zoezi hilo litakuwa limekamilika,” alisema na kuwataka
wananchi kufanya haraka kufunga nyaya za umeme na taa kwenye nyumba zao.
Pia, wananchi wa Kijiji cha Kingiti waliziba
njia kwa mabango kuomba kupatiwa zahanati. Aidha, katika Kijiji cha Idunda
wananchi hao waliomba kupatiwa umeme kutokana na kuchoka kutumia koroboi.
Wananchi hao waliahidiwa kupatiwa umeme haraka
iwezekanavyo. Aliahidi kutoa mabati kwa ajili ya kuezeka zahanati ya Kingiti.
“Upatikanaji wa umeme vijijini utaimarisha
uchumi, kwani wananchi watakuwa na uwezo wa kuanzisha viwanda vya usindikaji,”
alisema.
Alisema licha ya serikali kutumia fedha nyingi
kusambaza umeme vijijini, changamoto kubwa iliyopo ni wananchi kushindwa
kuunganisha umeme unapofika kwenye maeneo yao.
“Tumieni
nishati kuboresha maisha yenu, jipangeni ili muweke umeme, umeme umefika kwenye
vijiji vingi lakini watu bado hawaunganishi kwenye nyumba zao wakati walitakiwa
kutumia fursa hiyo hata kuwa na viwanda vidogo vya usindikaji,” alisema.
No comments:
Post a Comment