Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU) imesema imejipanga kikamilifu kuhakikisha
inashughulikia vitendo vya utoaji na upokeaji rushwa katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Akizungumza jana wakati
wa ufunguzi wa jengo la taasisi hiyo mkoani Kigoma lililogharimu Sh bilioni
1.2, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hosea alisema anasubiri kuanza kwa
ratiba ya Tume ya Uchaguzi ili iweze kuanza kutekeleza jambo hilo kwa kufuata
sheria za uchaguzi.
Alisema taasisi yake
imeshaanza kuona viashiria vya utoaji rushwa vinavyofanywa na baadhi ya watu
walioonesha nia ya kugombea katika uchaguzi mkuu ujao kwa kutoa vitu mbalimbali
zikiwemo fulana, chupa za chai na vitu vinavyofanana na hivyo.
Hata hivyo, alisema kwa
sasa haitaweza kuwakamata wala kuwahoji watu hao kwa kuwa si wagombea rasmi kwa
mujibu wa taratibu za uchaguzi, lakini alibainisha kuwa vijana wake
wanafuatilia kwa karibu nyendo zinazofanywa na watu hao.
Sambamba na kujipanga,
Hosea alitoa wito kwa wananchi kuchukia vitendo vya kupokea rushwa wakati wa
mchakato wa uchaguzi mkuu kwani vinawapotezea haki ya kuchagua mgombea mwenye
sifa badala yake hushawishiwa kuchagua kwa rushwa.
Katika hatua nyingine, Dk
Hosea alisema serikali imeokoa kiasi cha Sh bilioni 39 ambazo zilikuwa zilipwe
kwa watu mbalimbali ambao hawakufuata sheria na taratibu za malipo na manunuzi.
Awali, Katibu Tawala wa
mkoa Kigoma, Dk John Ndunguru alisema kuboreshwa kwa mazingira ya kufanyia kazi
katika maeneo yenye mazingira magumu kunatoa unafuu kwa watu wanaopangwa maeneo
hayo kuripoti na kufanya kazi.
Akizungumzia uchaguzi
mkuu ujao, Ndunguru aliitaka Takukuru kutoa elimu kwa jamii kujiandikisha na
kupiga kura kwa wagombea watakaosimamia maendeleo yao, badala ya
kuchagua wagombea wanaotoa rushwa.
Naye Mkuu wa Takukuru
mkoani Kigoma, Susan Lyimo alisema pamoja na mafanikio mbalimbali, ofisi ya
taasisi hiyo mkoani Kigoma inakabiliwa na changamoto ya mashahidi
kushindwa kujitokeza kutoa ushahidi katika kesi za rushwa.
Alisema jumla ya kesi
tisa za watu wanatuhumiwa vitendo mbalimbali vya utoaji na upokeaji wa rushwa
zipo mahakamani zikiwa katika hatua mbalimbali.
No comments:
Post a Comment